Ijumaa, 19 Novemba 2021

TANZANIA NA UINGEREZA WABADILISHANA UZOEFU UTOAJI ADHABU

 Na Magreth Kinabo – Mahakama

Jaji wa Mahakama Rufani ya Tanzania, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo jana  tarehe 18 Novemba, 2021 amefungua kongamano namna ya utoaji adhabu, ambapo amewaomba washiriki kubadilishana uzoefu ili kuweza kutatua changamoto wanazozikabili wakati wa utoaji adhabu kwa wakosaji mahakamani.

Kongamano hilo ambalo limeandaliwa Mahakama Tanzania kupitia Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa ushirikiano wa Ubalozi wa Uingereza na Taasisi ya Majaji Wastaafu nchini Uingereza (Slynn Fundation) limefanyika  katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam.

“Kama vile tunavyofahamu kwamba katika uendeshaji na usikilizaji wa mashauri inapofikia hatua ya mwisho wa utoaji adhabu ni kipindi kigumu na kinachangamoto,’’ Mhe. Dkt Kihwelo aliwaambia washiriki wa kongamano hilo.

Aliongeza kuwa kutokana na ugumu huo ni vizuri mafunzo juu ya suala hilo yakatolewa mara kwa mara au wakati wa mafunzo elekezi ili kuweza kuwa na uelewa mpana na uwiano wa adhabu ambazo zinaweza zikatolewa.

Hivyo, Jaji huyo wa Mahakama ya Rufani alisema kuwa kupitia  kongamano hilo Jaji Mstaafu Nic Madge kutoka Taasisi ya Majaji Wastaafu ya Uingereza atatoa uzoefu wa nchi ya Uingereza kwenye utoaji wa adhabu na uzoefu wa Tanzania utatolewa na Jaji Mstaafu  wa Mahakama  Kuu ya Tanzania, Mhe. Robert Makaramba, kupitia Mwongozo wa Utoaji adhabu Tanzania.

Dkt. Kihwelo aliongeza kwamba mwongozo huo umetayarishwa kwa msaada kutoka Ubalozi wa Uingereza. Aliushukuru Ubalozi wa Uingereza kwa msaada iliyoutoa kwa kuwezesha mafunzo hayo kufanyika, ambapo jumla Majaji 14 na Mahakimu wanne wamehudhuria kongamano hilo.

Jaji Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Paul Kihwelo (wa pili kulia) akiwa katika picha ya Pamoja mara baada ya kufungua kongamano hilo. Wengine ni washiriki wa kongamano hilo.

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo akifungua kongamano la namna ya Utoaji adhabu  lililofanyika  jana kwenye Hoteli ya Serena,  jijini Dar es Saalam.

Jaji Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt.Paul Kihwelo (wa pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji na Mahakimu walioshiriki Kongamano mara  baada ya kufungua. 

Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe.Robert Makaramba  akitoa uzoefu wa namna ya kutoa adhabu katika nchi ya Tanzania wakati wa Kongamano hilo.

Jaji Mstaafu kutoka Taasisi ya Majaji Wastaafu ya Uingereza (SYLNN FOUNDATION) Mhe. Nic Madge akitoa uzoefu wa namna ya utoaji adhabu  katika  nchi yake.

 

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza wakati alipotembelewa na ujumbe kutoka Sylnn Foundation leo ofisini kwake jijini Dar es salaam. Jaji Mkuu alisema, hivi sasa Sheria zinafanyiwa marekebisho ikiwemo Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai pamoja na Sheria ya Kanuni ya adhabu.  Alisema pia ni vizuri Taasisi hiyo ikaendeleza ushirikiano na Mahakama ya Tanzania katika kutoa mafunzo kwa Majaji, Mahakimu na wadau wanaofanya kazi na Mahakama ya Tanzania. 

Sehemu ya wajumbe kutoka Taasisi ya Sylnn Foundation ya Uingereza wakiwa ofisini kwa Jaji Mkuu walipomtembelea leo jijini Dar es salaam. 

Jaji Mstaafu kutoka Taasisi ya Majaji Wastaafu ya Uingereza (SYLNN FOUNDATION) Mhe. Nic Madge akiangalia kitabu cha Mpango Mkakati Mpya wa Mahakama ya Tanzania mara baada ya kukabidhiwa na Jaji Mkuu.

 

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe kutoka Taasisi ya Sylnn Foundation walipomtembelea leo ofisini kwake jijini Dar es salaam. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) Mhe. Dkt. Paul Kihwelo

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni