Ijumaa, 3 Desemba 2021

MAFUNZO ELEKEZI YA SIKU TANO KWA NAIBU WASAJILI NA WATENDAJI WA MAHAKAMA YAKAMILIKA

Na Faustine Kapama, Mahakama-Lushoto

Mafunzo elekezi yaliyokuwa yanayotolewa kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) yamekamilika leo tarehe 2 Decemba, 2021 huku viongozi hao wakihimizwa kuzingatia yote waliyoshirikishwa, ikiwemo kudumisha ushirikiano, umoja, upendo na kuboresha huduma za utoaji haki kwa wananchi.

Akizungungumza wakati anafunga mafunzo hayo, ambayo ni ya kwanza kuwashirikisha Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama, Mkuu wa Chuo hicho, Mhe, Dkt Paul Kihwelo, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani alibainisha kuwa heshima, upendo pamoja na ushirikiano sehemu za kazi ikawe ndio dira yao katika kutekeleza majukumu mbalimbali za kimahakama.

“Waha wanamsemo kuwa samaki anaoza kuanzia kichwani. Ninyi ni kichwa cha Mahakama, hivyo msikubali kuoza kwani mtawaharibu walio chini yenu. Ni tegemeo la kila mmoja wetu kuwa nyinyi ndio mtakuwa kioo cha tabia njema na sio kinyume chake. Nawaasa kwa mara nyingine mkawe wasimamizi wazuri wa maadili na nidhamu katika maeneo yenu ya kazi,” alisema.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa chuo, moja ya sifa kubwa iliyopo mahakamani ni upendo, udugu na mshikamano, hivyo hakuna shaka kuwa viongozi hao watapata ushirikiano wa kutosha kutoka kwa watangulizi wao pamoja na wale watakaowakuta vituoni. “Naamini ninyi pia mtatoa ushirikiano na niwaase pia kuwa msisite kuwafundisha mambo mapya ambayo hawayajui lakini pia muendelee kuwa wanafunzi wazuri kwani Wahaya wanamsemo usemao Experience is a Good Teacher,” alisesma.

Aliwakumbusha washiriki wa mafunzo hayo kuwa wakati wa ufunguzi walihusiwa mengi na viongozi mbalimbali, akiwemo Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani, aliwaeleza kuwa Mahakama na umma wa watanzania kwa ujumla una matarajio na imani kubwa kwao na kwamba watapimwa kupitia nguzo tatu za Mpango Mkakati wa Mahakama. Hivyo anaamini kuwa baada ya mafunzo hayo imani waliyonayo wananchi, wadau na Mahakama kwao itazidi kuongezeka kutokana na kuimarika kwa utendaji wao wa kazi.

Mhe. Dkt Kihwelo aliwaambia kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof Elisante Ole Gabriel pia wakati wa ufunguzi aliwakumbusha kuwa hawakupata nafasi hizo kama zawadi bali kupitia tanuru. “Nirudie kwa kusema hamkupata nafasi hizi kwa bahati bali mnastahiri kutokana na sifa zanu, ikiwemo utendaji kazi uliotukuka na sina shana kuwa mtatumikia nafasi hizi kwa bidii na uadilifu huku mkiheshimu mamlaka, madaraka na majukumu mliyonayo na yale ya wale mnaofanya nao kazi,” alisema.

Aidha, Mkuu huyo wa Chuo aliwakumbusha pia viongozi hao kuwa kwa upande wake wakati akiwawezesha mada Jaji Mkuu Mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman aliwaeleza juu ya umuhimu wa kufanya kazi kwa kushirikiana ili kuifanya Mahakama iweze kustawi zaidi.

“Katika hilo aliwasisitiza juu ya C tatu ambazo ni consultation, coordination na cooperation. Ni matumaini yangu kuwa baada ya kuwasikiliza nyote mtazingatia ushirikiano kwa kuwa umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Kwa vile sote tunajenga nyumba moja basi hatuna sababu ya kugombea fito,” alisema. 

Wakitoa neno la shukrani kwa niaba ya washiriki kwa nyakati tofauti, Naibu Msajili Mwandamizi, Mahakama ya Rufani, Mhe. Happiness Ndesambiro na Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Tanga, Bw. Tutubi Mangazeni waliushukuru uongozi wa Mahakama ya Tanzania pamoja na IJA kwa ujumla kwa kuandaa mafunzo hayo ambayo ni ya kwanza kuwashirikisha Naibu Wasajili na Watendaji. Waliahidi kutekeleza yote waliyojifunza kwa siku zote tano ili kuboresha huduma za utoaji haki kwa wananchi kwa kuwa mada zilizowasilishwa zimekuwa na manufaa makubwa sana kwao.

Mapema kabla ya kufika kileleni cha mafunzo hayo, Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. John Kahyoza, ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma na Mhe. Cyprian Mkeha, ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Biashara, walikuwa miongoni mwa wawezeshaji waliowasilisha mada mbalimbali kwa washiriki.

Mhe. Kahyoza alijikita katika kutoa maelezo ya kina kuhusu mamlaka ya ziada ya kwa Mahakimu katika kusikiliza mashauri ya Mahakama Kuu, ambapo Mhe. Mkeha aliwapitisha Naibu Wasajili hao kwenye eneo linalohusu namna ya kushughulikia maombi ya gharama za malipo baada ya kuendesha mashauri ya madai.

Wawezeshaji wengine waliotoa mada zao ni Bi. Sadaka Gandi, ambaye ni Mwanasaikolojia Mshauri Nasaha na Namna ya Kuishi, alitoa mada juu ya ustawi wetu, maisha yetu katika usawa mbele ya washiriki wote, huku mwezeshaji mwingine, Bw. Bwai Biseko kutoka Wakala wa Maji Vijijini, akiwasilisha mada juu ya kuendesha mashauri ya kinidhamu mbele ya Watendaji wa Mahakama.

Kabla ya kuhitimisha mafunzo hayo, Mkuu wa Chuo, Mhe, Dkt Kihwelo aliwakabidhi vyeti na zawadi mbalimbali Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama wote kama ishara ya kushiriki na kuonesha nidhamu ya hali ya juu wakati wote wa mafunzo hayo.

 


Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe, Dkt Paul Kihwelo, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani akizungumza wakati akifunga mafunzo elekezi yaliyokuwa yanayotolewa na chuo hicho kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama. Mafunzo hayo yamehitimishwa leo tarehe 3 Desemba, 2021.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma, Mhe. John Kahyoza akiwasilisha mada juu ya mamlaka ya ziada kwa Mahakimu kusikiliza mashauri ya Mahakama Kuu leo tarehe 3 Desemba, 2021 katika siku ya tano na ya mwisho  ya mafunzo yaliyokuwa yanayotolewa kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).


Sehemu ya Naibu Wasajili (picha ya juu na chini) wakimsikiliza Mhe. Kahyoza wakati akiwasilisha mada yake.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Biashara, Mhe. Cyprian Mkeha akiwasilisha mada mbele ya Naibu Wasajili kuhusu namna ya kushughulikia maombi ya gharama za malipo baada ya kuendesha mashauri ya madai.  
Sehemu nyingine ya Naibu Wasajili (picha ya juu na chini) wakimsikiliza Mhe. Mkeha wakati akiwasilisha mada yake.

Bi. Sadaka Gandi, ambaye ni Mwanasaikolojia Mshauri Nasaha na Namna ya Kuishi, alitoa mada juu ya ustawi wetu, maisha yetu katika usawa mbele ya washiriki wa mafunzo hayo.
Sehemu ya Naibu Wasajili wakimsikiliza Bi. Gandi.

Bw. Bwai Biseko kutoka Wakala wa Maji Vijijini, akiwasilisha mada juu ya kuendesha mashauri ya kinidhamu mbele ya Watendaji wa Mahakama (picha mbili chini).







Naibu Msajili Mwandamizi, Mahakama ya Rufani, Mhe. Happiness Ndesambiro (picha juu) na Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Tanga, Bw. Tutubi Mangazeni (picha chini) wakitoa neno la shukrani mara baada ya kuwezeshwa kwenye mada mbambali walizoshirikishwa katika mafunzo elekezi yaliyomalizika leo tarehe 3 Desemba, 2021.






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni