Na Innocent Kansha – Mahakama.
Mtendaji
wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Bw. Solanus Meinrad Nyimbi amewaasa viongozi wa Chama cha Ushirika cha Akiba na Mikopo cha Mahakama ya Tanzania (Mahakama Saccos) kutumia ujuzi wa wataalam wa fani mbalimbali ambao ni wanachama
wa Saccos waliopo ili kuboresha shughuli za chama ziendane na mabadiliko ya Kitaasisi,
kwa kutambua Mahakama ya Tanzania inaendelea na mageuzi makubwa ya kimifumo
kuendana na karne ya 21.
Akifungua
mkutano mkuu wa mwaka wa Mahakama Saccos leo tarehe 4 Desemba, 2021, katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Jijini Dar es salaam kwa niaba ya Jaji Mkuu
wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Bw. Nyimbi alisema viongozi wanapaswa kutumia fursa ya
kila kunapotokea mafunzo ya waajiriwa wapya wa Mahakama kuwashawishi kujiunga na
chama ili kuongeza idadi ya wanachama kwani ndio njia bora ya kuimarisha Saccos hiyo.
“Nafahamu
kuwa Chama hiki kina umri wa miaka 51 tangu kupata usajili wake mwaka 1970,
hivyo nawapongeza kwa kudumu muda wote licha ya changamoto zinazoendelea
kujitokeza. Kudumu kwa chama kunatokana na aina ya viongozi wanaochaguliwa,
kuaminiana kati ya wanachama wenyewe na misaada halikadhalika faida ya mikopo
mbalimbali inayotolewa na Saccos kwa wanachama wake”, alifafanua Mtendaji Nyimbi.
Akiongelea
suala la kushawishi wanachama wapya kujiunga na Mahakama Saccos, Mtendaji
Nyimbi alisema, "niwahakikishie kumfikishia salamu Jaji Mkuu kuhusu
kuwashawishi Majaji na Viongozi wengine waandamizi wa muhimili
kujiunga katika umoja huo ili iwe chachu kwa watumishi wengine wa ngazi
mbalimbali."
Aidha,
Mtendaji huyo aliwaasa viongozi kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na
kuzingatia sheria za nchi kwa maana kama wakiaminiwa na wao wanatakiwa waaminike. Alisema kuwa utendaji wa
shughuli za chama uendane na mabadiliko hasa mageuzi ya mfumo wa TEHAMA ili
kutobaki nyuma na kuleta ufanisi kwenye huduma.
Aliongeza
kuwa wanachama wanaoomba mikopo wahakikishe wanachukua kwa malengo mahususi
hasa kuwekeza kwenye shughuli za kiuchumi, huku akikitaka Chama kuangalia uwezekano wa
kuwekeza kwenye miradi ya uzalishaji mali ili kuongeza mtaji.
Kwa
upande mwingine, Mtendaji Nyimbi aliwatia shime Viongozi na wanachama kuendelea
kutoa hamasa kwa watumishi wasio wanachama ili wajiunge katika kujiimarisha
kiuchumi kupitia utaratibu wa kujiwekea akiba.
Wakati huo huo,
Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Mahakama Saccos, Bi. Stephania Bishobe, akisoma
hotuba yake kwa Mgeni rasmi alisema lengo la umoja huo wa Saccos ni kuinuana
watumishi kiuchumi, hivyo basi huduma mama inayotolewa kwa wanachama ni mikopo
ya aina mbalimbali ikiwemo, mkopo wa maendeleo, wa dharula, sikukuu, mkopo wa viwanja
na pia mkopo wa kuanzia maisha kwa mwanachama wa ajira mpya.
Makamu
Mwenyekiti huyo alisema kuwa licha ya kupata mafanikio ndani ya mwaka 2021, pia
Chama kinachangamato kadhaa ambazo ni pamoja na uchache wa wanachama
ukilinganisha na idadi ya watumishi. Kwa sasa chama kina idadi ya asilimia sita
kati ya watumishi wote wapatao 5,800. Ukosefu wa ofisi ya kutosha kutekeleza majukumu ya chama na Mahakama Saccos kuonekana kama sio sehemu ya Mahakama.
Aidha,
Bi. Bishobe akataja marajio ya chama kwa mwaka 2022 kuwa ni kuanzisha mfumo wa
kielektroniki wa uendeshaji wa shughuli za za chama, kufanya utafiti na kuona
uwezekanao wa kupunguza riba ya mkopo kuwa chini ya asilimia 10, kutoa gawio la
faida kwa wanachama kwa mujibu wa sera na sheria na kuendelea kuongeza hisa za
wanachama.
Ushirika huu wa akiba na mikopo Mahakama ulianzishwa miaka 51 iliyopita na kusajiliwa tarehe 1 Agosti, 1970 kwa jina la Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo Mahakama ya Tanzania (Mahakama Savings and Credit Cooperative Society Limited). Hadi kufikia tarehe 30 Septemba, 2021 Chama kina jumla ya wanachama 425, sawa na asilimia sita ya watumishi 5,800 wa Mahakama.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni