Jumatatu, 17 Januari 2022

JAJI KIONGOZI ASISITIZA UADILIFU KWA MAHAKIMU

 Na Faustine Kapama, Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani amewataka Mahakimu kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu mkubwa, hivyo kuijenga Mahakama inayoaminika na isiyo na doa la rushwa.

Mhe. Siyani ametoa wito huo leo tarehe 17 January, 2022 katika hafla ya kuwaapisha Mahakimu Wakazi wapya 29 katika ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki-Temeke mkoani Dar es Salaam. Katika hafla hiyo iliyohudhuriwa na maafisa mbalimbali, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alikuwa mgeni rasmi.

Akizungumza baada ya uapisho huo, Jaji Kiongozi aliwaambia Mahakimu hao kuwa kazi waliyoiomba inahitaji uadilifu wa hali ya juu, huku akiamini kuwa kila mmoja wao ni muumini wa dini fulani ambapo dini zote hapa nchini zinahubiri suala hilo la uadilifu.

Aliwapitisha kwenye Bibilia, Kumbukumbu la Torati 1:16-17 na Sura ya 4 ya Quran, Aya ya 135 na kusema, “ukiwa Mkristo au Mwislam, vyovyote itakavyokuwa, ili ufanye kazi ya uhakimu unahitaji kuwa mwadilifu. Usipokuwa mwadilifu basi utakuwa umekosea kuwa mahali hapa na hautadumu.”

Ili kuonesha umuhimu wa uadilifu kwa kazi ya uhakimu, Mhe. Siyani alimnukuu mwanazuoni mmoja kutoka Nigeria ambaye aliwahi kusema, “Afisa wa Mahakama asiye mwadilifu ana madhara makubwa kwa jamii kuliko mtu anayekimbia hovyo katikati ya mtaa uliofurika umati wa watu akiwa na upanga mkononi.

“Kwa kuwa wakati mtu huyo anaweza kuthibitiwa kwa nguvu, Afisa wa Mahakama asiye mwadilifu kwa makusudi huharibu msingi wa maadili ya jamii aliyomo na kuleta madhara yasiyoweza kutatuliwa kwa wananchi kwa matumizi mabaya ya madaraka ya ofisi yake na wakati huo huo akiitwa Mheshimiwa.”

Hivyo, Jaji Kiongozi aliwaomba Mahakimu kutambua ukubwa na thamani ya kazi ambayo Taifa limewapa na kuwataka kwenda kuchapa kazi kwa uadilifu na kuijenga Mahakama inayoaminika na isiyo na doa la rushwa.

Aidha, Mhe. Siyani aliishukuru Tume ya Utumishi wa Mahakama na Serikali kwa ujumla kwa kuendelea kuajili watumishi mbalimbali, wakiwemo Mahakimu walioapishwa.

Alibainisha kuwa bado kuna upungufu mkubwa wa watumishi, hivyo ni imani yake Mahakimu hao watasaidia kupunguza upungufu uliopo. Jaji Kiongozi aliwapongeza Mahakimu wote waliokula kiapo na kuwakaribisha katika familia ya Mahakama ya Tanzania.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akitoa nasaa kwa Mahakimu Wakazi wapya 29 (hawapo pichani) walioapishwa leo tarehe 17 Januari, 2022.

Baadhi ya Mahakimu Wakazi wapya 29 walioapishwa wakimsikiliza Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (hayupo kwenye picha) wakati akizungumza katika hafla ya Uapisho huo.

Meza Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Mahakimu Wakazi wapya mara baada ya kula kiapo (picha ya juu na chini). Waliokaa katikati niJaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani na kuliani Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki -Temeke, Mhe. Ilvin Mugeta.


Mmoja kati ya Mahakimu Wakazi 29 (picha ya juu na chini) wakila kiapo mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma wakati wa hafla ya uapisho.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni