Jumatano, 19 Januari 2022

JAJI MKUU MSTAAFU AWAFUNDA MAHAKIMU WAKAZI WAPYA

 Na Rosena Suka - Lushoto

Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Mohamed Chande Othman amewashauri Mahakimu wapya kusimamia kikamilifu Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania na uboreshai wa huduma unaoendelea ili kuleta mabadiliko chanya kwa wananchi.

Mhe. Chande alitoa ushauri huo tarehe 18 Januari, 2022 alipokuwa akifungua mafunzo elekezi kwa Mahakimu Wakazi 35, wakimwemo wapya walioapishwa hivi karibuni na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahimu Hamis Juma. Mafunzo hayo yanayoendeshwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ambayo yatafanyika kwa muda wa siku tano.

Jaji Mkuu Mstaafu aliwaambia Mahakimu hao kuwa Mahakama ya Tanzania inawategemea katika kusimamia mpango mkakati huo na uboreshaji wa huduma zinazotolewa mahakamani ili kuleta mabadiliko chanya yanayotarajiwa kwa wananchi.

Mhe Chande aliwaeleza Mahakimu kuwa taswira nzuri ya Mahakama za Mwanzo wanazoenda kuhudumu ambazo kwa sasa zimebadilika, hivyo akawaomba waendelee kuzibadilisha na kuzifanya bora zaidi ili ziweze kutoa huduma nzuri zaidi na kwa wakati kwa wananchi.

“Mahakama za Mwanzo ndio zinatoa fursa kubwa zaidi juu ya haki kwa Watanzania kuliko ngazi zingine za Mahakama kwa sababu zimetapakaa Tanzania nzima”, alisema Mhe. Chande.

Aidha, Jaji Mkuu mstaafu huyo hakusita kuwakumbusha Mahakimu hao kuwa makini kwenye nguzo muhimu ya uhuru wa kila hakimu na uhuru wa Mahakama kwa ujumla. Aliwasisitiza kuamua mashauri yaliyo mbele yao kwa kuzingatia sheria, bila woga wala shinikizo. 

“Watanzania wanataka Mahakama huru inayotoa haki kwa wakati, Mahakama adilifu, Mahakama ambayo inauwezo na Mahakama ambayo haina gharama kubwa, ”aliongeza Mhe. Chande.

Aliwaasa Mahakimu hao kujua na kufuata taratibu zilizowekwa na Mahakama wakati wa uendeshaji wa mashauri hadi kutoa uamuzi unaoongozwa na sheria bila kusahau kupata maoni kutoka ya Wazee wa Baraza na kuainisha sababu walizozingatia kufikia uamuzi huo.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha IJA, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, alisema Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ni kitovu cha mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi wa kada mbalimbali wa Mahakama na wadau wa sheria nchini.

Mkuu huyo wa Chuo alisema mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Mafunzo ya Taifa ya 2013 na Mpango Mkakati wa Mahakama (2021/22-2024/25), Sera ya Mafunzo ya Mahakama ya Tanzania ya mwaka 2019 ambayo inaelekeza kila mtumishi anayeajiriwa, kupanda cheo au kuteuliwa apate mafunzo elekezi kabla hajaanza majukumu mapya kwa lengo la kuboresha huduma za Mahakama.

Mhe. Dkt.Kihwelo aliwaomba Mahakimu hao kujitahidi kutoa huduma nzuri na kujiepusha na vitendo rushwa kwani kwa sasa Mahakama zimeboreshwa kwa kuwa na majengo mazuri sana na hivyo huduma ziendane na uzuri wa majengo hayo.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt ameupongeza uongozi wa Mahakama kwa programmu za uboreshaji wa huduma zinazofanyika, ikiwepo kuwekeza kwenye raslimali watu ambapo Chuo  kimekuwa kikifanya kwa vitendo kuwajengea uwezo watumishi mbalimbali ili kuwawezesha kufanya kazi zao kwa ufanisi na weledi.

Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Mohamed Chande Othman akifungua mafunzo elekezi kwa Mahakimu Wakazi Wapya leo tarehe 19 Januari, 2022 yanayoendeshwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.

Mkuu wa Chuo cha IJA, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani akitoa neno la utambulisho kwa washiriki hayo.

Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt akitoa utambulisho wa vingozi mbalimbali waliohudhuria nufunguzi wa mafunzo hayo.

Sehemu ya washirikiwa mafunzo elekezi kwa Mahakimu Wakazi Wapya (pichas ya juu na tatu za chini) yanayoendeshwa na Chuo cha IJA wakiwa wanafuatilia  hotuba ya ufunguzi kutoka kwa Mhe. Mohamed Chande Othman (hayupo katika picha).





Mhe. Chande Othman Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania akiwa katika picha ya pamoja na wawezeshaji Mafunzo Elekezi kwa Mahakimu Wakazi Wapya yanayoendeshwa na Chuo cha UongoziwaMahakamaLushoto. Waliokaa kushoto ni Mkuu wa Chuo cha IJA, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na kulia Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni