Na Faustine Kapama, Mahakama
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 20 Januari, 2022 amekutana
na viongozi wapya wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (JMAT) na kuahidi kuwapa
ushirikiano ili waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu na pia kushughukikia,
pamoja na mambo mengine, changamoto mbalimbali zinazowakabili, ikiwemo suala la
mishahara na maslahi mengine.
Akizungumza
na viongozi hao ofisini kwake Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam
walioongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma,
Mhe. John Kahyoza, Jaji Mkuu alizitaja baadhi ya changamoto hizo ikiwemo hoja inayohusu
mishahara na maslahi kwa Majaji na Mahakimu.
“Mmeahidi
kuleta ulinganifu wa mishahara ya Majaji na Mahakimu kutoka Kenya, Uganda,
Zanzibar ili tunapopeleka mapendekezo yetu serikalini tuanishe kiwango kinachoweza
kukidhi kazi ngumu ambayo mnafanya. Kwa hiyo, mimi naahidi kuwa nitapokea
changamoto zenu na nitaziwasilisha mbele ya Tume ya Utumishi wa Mahakama ambayo
itazifikisha kwenye mamlaka inayohusika na maslahi na mishahara,” amesema.
Jambo
jingine la msingi ambalo liliongelewa na kuwasilishwa kwake, ambapo ameahidi
kulifanyia kazi, ni baadhi ya Mahakama za Mwanzo na Wilaya kuwa katika maeneo
ya mbali yenye changamoto ya usafiri na ugumu wa kupatikana mitandao, jambo
ambalo viongozi wa chama hicho wameomba eneo hilo kuangaliwa, hasa katika kurahisisha
utendaji kazi kwa kuzingatia Mahakama kwa sasa inatumia zaidi mifumo ya
teknolojia.
Kwa
mujibu wa Mhe. Prof. Juma, eneo jingine lilioongelewa linahusu kujiendeleza kwa
kuzingatia Mahakimu wengi walijiunga na Mahakama ya Tanzania kwa miaka mingi
iliyopita na hawajapata fursa ya kujiendeleza, hivyo wakaomba Mahakama ichukue
jukumu la kuwaendeleza kuhakikisha mara baada ya kustaafu wawe katika kiwango
kizuri cha elimu.
“Jambo
hili tumelipokea na tutalifanyia kazi,” Jaji Mkuu alisema na kubainisha hoja
nyingine inayohusu uboreshaji wa huduma za kimahakama zinazoendelea ikiwepo kubadilisha
mfumo uliokuwepo ili kuwawezesha Mahakimu wenye Shahada ya Sheria kuanza
kusikiliza Mashauri katika Mahakama za Mwanzo, hatua ambayo imesababisha wengi
wa Mahakimu waliokuwa wakihudumu katika Mahakama hizo kwa muda mrefu ambao
hawana hiyo sheria kubaki katika ngazi zile zile za kimshahara.
“Ingawa
uboreshaji huu ni mzuri kwa nchi na kwa Mahakama, lakini umewasahau. Kwa hiyo,
mmesisitiza kuangalia eneo hili kuhakikisha hawa Mahakimu ambao wamefanya kazi kwa
muda mrefu na kwa uaminifu mkubwa hawabaki katika ngazi ya kusahaulika kimshahara
na kimaslahi. Nahidi masuala yote ambayo mmeyaibua yatajadiliwa na Tume ya
Utumishi wa Mahakama na tutawapa mrejesho,” alisema.
Amewapongeza
Majaji na Mahakimu kwa kuwapata viongozi wapya ambao wataongoza chama hicho kwa
muda wa miaka mitatu ijayo. Jaji Mkuu alibainisha kuwa yeye kama mlezi wa chama
hicho ataendelea kushirikiana na JMAT na kuwaunganisha na vyama vingine vya
Majaji na Mahakimu wa Afrika Mashariki na katika Jumuiya ya Madola.
Viongozi
wa JMAT waliochanguliwa tarehe 18 Desemba, 2021 kuogoza chama hicho kwa kipindi
cha miaka mitatu na vyeo vyao kwenye mabano ni Mhe. Kahyoza (Rais), Mhe. Shaibu
Mzanda (Makamu wa Rais), Mhe. Lazaro Magai (Katibu), Mhe. Frank Lukosi (Mweka Hazina)
na Mhe. Nemes Mumbuli (Katibu Mwenezi).
Awali,
Rais wa JMAT, Mhe. Kahyoza alielezea madhumuni ya kukutana na Jaji Mkuu wa Tanzania,
ambaye ndiye Mlezi wa chama hicho, ikiwemo kujitambulisha kama viongozi wapya,
kupata maelekezo na matarajio kutoka kwake katika kipindi chao cha uongozi na
kuomba ushirikiano kwa mambo mbalimbali ili waweze kutekeleza kikamilifu
malengo ya kuanzishwa kwa chama hicho.
Aliyataja
baadhi ya malengo hayo kama kukuza na kulinda uhuru wa Mahakama. Amesema kuwa
anaamini wanachama wakifanya kazi katika mazingira ambayo ni huru wataweza
kutekeleza majukumu yao kwa ukamilifu, ikiwemo kulinda haki za binadamu na raia.
Mhe. Kahyoza alisema pia kuwa chama chao kinahakikisha wanachama wake
wanazingatia maadili, ndiyo maana mwaka 1984 JMAT iliweka kanuni za maadili kwa
wananchama wake.
Hata
hivyo, alibainisha kuwa jambo hilo kwa sasa limechukuliwa na Mahakama ya
Tanzania yenyewe ambapo imetoa kanuni kwa Majaji na Mahakimu, hivyo kufanya
kanuni za JMAT za mwaka 1984 kuacha kutumika. Amesema katika eneo hilo ambalo kuna
kanuni mpya zilizotayarishwa chama kitachukua jitihada za kuwaelemisha
wananchama wao ili wazielewe na kuzitumia katika kutekeleza majukumu mbalimbali.
Mhe.
Kahyoza alielezea lengo lingine la kuanzishwa kwa chama hicho ni kukuza,
kutetea na kulinda maslahi na haki za wanachama, kwa kuzingatia Majaji na
Mahakimu hawapo katika vyama mbalimbali vya wafanyakazi vinavyojishughulisha na
kupigania haki na maslahi ya wafanyakazi hapa nchini.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni