Jumamosi, 22 Januari 2022

WATUMISHI TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA TIMIZENI MALENGO YA TAASISI: JAJI KIONGOZI

 Na Lydia Churi- Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustapher Siyani amewataka watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kuwa na nidhamu ya hali na kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao ipasavyo ili waweze kutimiza malengo ya Taasisi hiyo.

Akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama uliofanyika jijini Dodoma, Jaji Kiongozi ambaye pia ni Mjumbe wa Tume hiyo amesema Taasisi yoyote ambayo watumishi wake hawana nidhamu ni ngumu kutimiza malengo yake.

“Nidhamu ni muhimu sana kwa watumishi na hasa wa Tume hii, bila nidhamu malengo ya taasisi hayawezi kutimizwa, na watumishi wasipokuwa na nidhamu husababisha malalamiko kuongezeka”, alisisitiza Jaji Kiongozi.

Aliwataka watumishi wa Tume hiyo kutofanya kazi kwa mazoea na badala yake wawatumikie wananchi kwa kuwa nafasi za kazi walizonazo ni dhamana waliyopewa.

Aidha, Jaji Siyani aliwapongeza watumishi wa Tume hiyo kwa kazi nzuri wanayoifanya na kuwataka kuendelea kutoa miongozo na kanuni kanuni mbalimbali ili Mahakama ya Tanzania itekeleze majukumu yake ya utoaji haki ipasavyo na kwa kwa mujibu wa sheria.

“Kila Mtumishi wa Mahakama aweke malengo ya kazi na kuyatimiza, Tume ya Utumishi wa Mahakama itaendelea kusimamia kuona watumishi wanatekeleza majukumu yao na isiwavumile wale wachache wanaosababisha malalamiko kuongezeka”, alisema.

Kuhusu matumizi ya Tehama, Jaji Kiongozi aliwataka watumishi hao kuongeza kasi katika matumizi hayo ili kurahisisha utendaji kazi na kuongeza uwazi katika shughuli za utoaji wa haki. Alisema hivi sasa Mahakama ya Tanzania inaendelea na ujenzi wa majengo ya bora na ya kisasa ya Mahakama ambayo yanazingatia uwekaji wa miundombinu ya Tehama.

Naye Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ambaye pia ni Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka watumishi wa Tume hiyo kutekeleza majukumu yao kwa nidhamu na kufahamu kuwa tume hiyo ndiyo inayosimamia utendaji kazi wa Mahakama.

“Mjikite zaidi kwenye matumizi ya Tehama yatakayowasaidia kupunguza mzigo wa kazi na kuongeza uwazi zaidi. Mwezi Februari mwishoni tutaingia kwenye matumizi ya Ofisi Mtandao pamoja na mifumo mingine ya Tehama”, alisema.

Alisema Mahakama itaboresha maslahi ya watumishi wa Tume hiyo na kufanya jitihada za kuongeza idadi ya watumishi. Tume ya Utumishi wa Mahakama inapaswa kuwa na idadi ya watumishi 34, hivyo hivi sasa kuna upungufu wa watumishi 15.

Kuhusu Uviko 19, Mtendaji Mkuu wa Mahakama amewataka watumishi hao kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huo na kuwashauri kupata chanjo na kutokuwa na hofu za chanjo hiyo bila ya sababu za msingi.

Tume ya Utumishi wa Mahakama imeanzishwa kwa mujibu wa Ibara ya 112 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ikisomwa pamoja na Sheria ya Uendeshai wa Mahakama Na. 4 ya mwaka 2011.

 

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustapher Siyani (katikati) ambaye pia ni Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama akiwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (Katibu wa Tume) wakiimba pamoja na watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wimbo wa Mshikamano wakati wa Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume hiyo uliofanyika jijini Dodoma. Jaji Kiongozi alifungua Mkutano huo.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel ambaye pia ni Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama akisikiliza hoja mbalimbali za Watumishi wa Tume hiyo.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustapher Siyani (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama mara baada ya kufungua Mkutano wa Baraza. Wa pili kushoto ni  Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (Katibu wa Tume), na wa pili kulia ni Katibu Mtendaji wa Tume hiyo Bibi Enziel Mtei.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustapher Siyani (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Wanawake mara baada ya kufungua Mkutano wa Baraza. Wa pili kushoto ni  Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (Katibu wa Tume), na wa pili kulia ni Katibu Mtendaji wa Tume hiyo Bibi Enziel Mtei.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni