Jumapili, 23 Januari 2022

ONDOENI KESI ZISIZO NA USHAHIDI MAHAKAMANI


Na Magreth Kinabo- Mahakama

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Lubigija Ng’wilabuzu, ameiomba Mahakama ya Tanzania kuondoa kesi zisizokuwa na ushahidi mahakamani, isipokuwa zile zenye mazingira ya kiusalama, mfano kuua au kubaka ili kuweza kupunguza mlundikano wa mahabusu  magerezani.

Bw. Ng'wilabuzu, ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Ilala, ametoa ombi hilo leo tarehe 23 Januari, 2022 baada ya kushiriki katika matembezi ya uzinduzi wa maadhimisho ya Wiki ya Sheria, ulioandaliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam kwenye viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.Matembezi hayo yalianzia Mahakama Kuu ya Tanzania mpaka mahakama hiyo.

Ameviomba vyombo husika kushirikiana na Mahakama kuziondoa kesi hizo kwa kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza idadi ya mahabusu katika magereza.

‘‘Uondoshaji wa mashauri haya yasiyokuwa na ushahidi mahakamani utasaidia kupunguza idadi ya mahabusu magerezani, pia utasaidia Serikali kupunguza gharama za kuwahudumia. Hatua hii itawapa fursa Majaji au Mahakimu kupata fursa ya kusikiliza mashauri mengine,’’ alisema Ngw’ilabuzu.

Aliongeza kuwa njia nyingine ya kupunguza mlundikano huo ni vyema mtuhumiwa kupelekwa mahakamani wakati ushahidi ukiwa umeshakamilika.

Kaimu Mkuu wa Mkoa huyo alisema siku za nyuma walikuwa wanapokea malalamiko mengi kuhusu mashauri kukaa muda mrefu mahakamani au kutoridhishwa na uamuzi wa Mahakama, lakini hivi sasa malalamiko hayo hayapo.

Hata hivyo, alisema kuwa changamoto iliyopo ni mashauri ya ardhi, hivyo alishauri wanasheria wa Serikali, Mawakili na Mabaraza ya Ardhi kushirikiana ili kuweza kutatua suala hilo. Pia alisema Serikali itaendelea kushirikiana na Mahakama ili kuboresha miundombinu chakavu.

Aliwaomba wananchi kufika katika viwanja hivyo, ambapo maadhimisho hayo yameaanza leo tarehe 23 Januari, 2022 na yatamalizika tarehe 29 Januari, 2022, ili kupata elimu ya mambo mbalimbali kuhusu masuala ya kisheria. Kauli mbiu ya maashimisho hayo ni ‘Zama za Mapinduzi ya Nne ya Viwanda: Safari ya Maboresho kuelekea Mahakama Mtandao’.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma alisema Kanda hiyo imeweza kusajili zaidi ya mashauri 1,871 kati ya mashauri 2,225 yalisajiliwa kwa njia ya mtandao ambayo ni sawa na asilimia 84. Aidha alisema kwa kipindi cha mwezi Desemba pekee jumla ya mashauri 798 yalisikilizwa kwa njia ya ‘Video Conference’ katika ngazi zote za Mahakama.

Alifafanua kuwa Kanda hiyo iliongoza kwa kusikiliza mashauri mengi kwa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) mwezi Desemba, ambapo ilisikiliza mashauri 6,352.

‘‘Kanda ya Dar es Salaam katika ngazi zote za Mahakama iliingia na jumla ya mashauri 13, 448 yaliyokuwa yamebakia kipindi cha mwaka 2020, huku jumla ya mashauri 39,031 yalifunguliwa na mashauri 40,146 yalisikilizwa na kubakiwa na mashauri 12, 333. Kati ya mashauri yaliyobakia hadi kufikia mwaka 2021 ni asilimia 15,’’ alisema Jaji Mruma.  

Jaji Mruma alisema ufanisi huo wa kazi umetokana na malengo ya kusikiliza mashauri ndani ya muda uliopangwa


  Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Lubigija Ng'wilabuzu  akizungumza              jambo, wakati akifungua Maadhimisho ya Wiki ya Sheria  kwa  Mahakama Kuu ya            Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam leo kwenye viwanja kwenye viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam. 
Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma akizungumza   , wakati akitoa hotuba yake kwenye mazungumzo ya  Maadhimisho ya Wiki ya Sheria  kwa  Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam leo kwenye viwanja kwenye viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya watumishi wa Mahakama ya Tanzania na wadau wa Mahakama wakiwa katika matembezi hayo.

Bendi ya polisi ikitumbuiza matembezi hayo.
Watumishi hao na wadau wakifanya mazoezi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni