Jumatatu, 24 Januari 2022

PROF. JUMA AHAIDI KUENDELEZA USHIRIKIANAO WA KARIBU NA MAHAKAMA ZANZIBAR

Na Innocent Kansha – Mahakama Dodoma.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amemuhakikishia Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi kuwa Mahakama ya Tanzania itaendelea kushirikiana kwa ukaribu na Mahakama ya Zanzibar katika maeneo mbalimbali ikiwemo kubadilishana uzoefu, mafunzo na uboreshaji wa huduma hususani matumizi ya teknolojia ili kurahisisha utoaji wa haki kwa wananchi.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Sheria nchini leo tarehe 23 Januari, 2022 katika Viwanja vya Nyerere Square Jijini Dodoma, Mhe. Prof. Juma alisema, katika eneo la kubadilisha uzoefu, kumbukumbu zinaonyesha mahusiano hayo yalianza mwaka 1965 hadi 2000 ambapo baadhi ya Mahakimu na Majaji kutoka Bara waliazimwa kufanya kazi huko visiwani Zanzibar.

“Upo umuhimu wa kurudisha ubadilishanaji huo wa uzoefu baina ya Mahakama za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mahakama ya Zanzibar ili kuimarisha mahusiano yenye tija katika kuwahudumia wananchi wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania” alisema Jaji Mkuu.

Mhe. Prof. Juma, alimpongeza Rais Mwinyi kwa hatua zake madhubuti za kutumia rasilimali ya bahari na faida ya umbo la kijiografia la Zanzibar, kujenga Uchumi wa Bluu kwa faida na manufaa ya wananchi ambapo uchumi wa bluu hugusa sekta mbalimbali, ambazo zinaingiliana na kutegemeana na sekta hizo zinaongozwa na kuratibiwa na sheria mbalimbali. Amesema kuwa baadhi ya sheria hizo zitahitaji kufanyiwa mabadiliko ili zifanikishe uchumi wa bluu na kusimamia ustawi wa rasilimali hizo.

Kwa mujibu wa Jaji Mkuu, kama Wanasheria wakizielewa sera na mipango ya ujenzi wa uchumi wa bluu, watakuwa katika nafasi nzuri ya kushauri na kushughulikia aina mpya kabisa ya mashauri ambayo yanaweza kuibuka na kuhitaji ujuzi na maarifa tofauti na yaliyozoeleka.

Akizungumzia Wiki ya Sheria nchini inayoadhimishwa kitaifa Jijini Dodoma, Jaji Mkuu Prof. Juma alisema kuwa kuna wananchi wachache kutoka nchi nyingi duniani ikiwemo Tanzania wanaofahamu kuwa Sheria inasimamia na kuongoza mambo mengi katika maisha yao ya kila siku, mahusiano miongoni mwao na baina yao na serikali, hivyo Mahakama ya Tanzania hutumia nafasi katika Wiki ya Sheria kuwakumbusha wananchi baadhi ya sheria na taratibu za kimahakama ambazo ni muhimu katika maisha yao ya kila siku.

“Hebu tujaribu kujiuliza swali, maisha yatakuwaje endapo kwa siku moja,tutakuwa hatuna sheria, polisi, Mahakama, Magereza, na vingine vya mfano huo. Jibu ambalo tutapata ni kuwa, kazi kubwa ya sheria ni kuondoa yale yote yanayoweza kutokea endapo nchi itakuwa haina sheria au imepoteza utulivu,Aamani udugu na mshikamano”, Jaji Mkuu alisema.

Akifafanua kuhusu kauli mbiu ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria nchini, Mhe. Prof. Juma alisema, katika kwenda sambamba na mapinduzi ya Nne ya Viwanda, Mahakama ya Tanzania imeazimia kupata mfumo wa akili bandia

utakaosaidia kuchukua mwenendo na ushahidi mahakamani, kuweka katika mfumo wa maandishi na kutafsiri kwa lugha ya kingereza au kiswahili pale inapohitajika “transcription and translation software”.

“Akili Bandia hii inalenga kumaliza changamoto kubwa uchukuaji na uandishi wa mwenendo na ushahidi kwa mkono pamoja na kutafsiri mwenendo au ushahidi huo kwa kuwatumia Majaji na Mahakimu” aliongeza Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu akaongeza kuwa programu mpya ya Akili Bandia itaondoa changamoto zinazowakabili Mahakimu na Majaji kwa kutumia muda mwingi kuchukua na kuandika ushahidi kwa mkono, itapunguza gharama za usikilizaji wa mashauri na itaongeza uwazi na hivyo kurejesha imani ya wananchi kwa Mahakama.

Kwa upande wa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Jaji Mkuu akasema, "Mahakama ya Tanzania inaendelea kupiga hatua kubwa katika matumizi ya TEHAMA sio tu katika shughuli za utoaji haki, bali katika kutoa huduma nyingine. Wananchi wanakaribishwa katika Wiki ya Sheria kujionea namna Mahakama ya Tanzania ilivyowekeza katika mifumo ya TEHAMA ambayo yamefanikisha maboresho makubwa."

Katika mabanda ya maonesho, wananchi watajionea mfumo wa Usajili, Usimamizi na Utambuzi wa Mawakili (Mjue Wakili Wako - eWakili), mfumo huu unawapambanua mawakili wenye leseni hai na hivyo kustahili kutoa huduma za uwakili.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akitoa hotuba kwenye uzinduzi wa Wiki ya Sheria nchini Jijini Dodoma leo tarehe 23 Januari, 2022. Kulia aliyesimama ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Martin Chuma.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi akiwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali, taasisi na Mahakama ya Tanzania, akiwemo Jaji Mkuu, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kushoto kwa Rais Mwinyi) wakipasha moto misuli kabla ya kuanza rasmi matembezi ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria nchini Jijini Dododma.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi (katikati) akiwa na Viongozi mbalimbali wa serikali, Taasisi na Mahakama ya Tanzania wakipoza moto misuli kwa kufanya mazoezi mepesi ya viungo mara baada ya kuhitimisha matembezi ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria nchini Jijini Dododma.

Meza Kuu wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mbalimba wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Sheria nchini Jijini Dododma.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)





 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni