Jumatatu, 7 Februari 2022

JAJI MLACHA AFANYA UKAGUZI MIRADI YA UJENZI WA MAHAKAMA KIGOMA

Na Festo Sanga, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu- Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha amekagua Miradi ya Ujenzi wa Mahakama tarajiwa za Wilaya ya Uvinza, Buhigwe na Kakonko  inayoendelea kujengwa  katika Kanda hiyo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo aliyofanya tarehe 05 Februari, 2022, Mhe. Jaji Mlacha alimsisitiza mkandarasi wa Miradi hiyo ambaye ni ‘Lucas Construction CO LTD’ kuongeza kasi katika ujenzi kwa kuzingatia ubora.

“Kazi inakwenda vizuri japo mpo nyuma ya ratiba, tafadhali ongezeni kasi na kuzingatia viwango vya ubora” alisema Jaji Mlacha.

Miradi hiyo ya Ujenzi iliyoanza kujengwa rasmi tarehe 15 Oktoba, 2021 inatarajiwa kukamilika tarehe 30 Aprili mwaka huu.

Ujenzi wa Mahakama tatu (3) za Wilaya ya Buhigwe, Uvinza na Kakonko utawaondolea adha wananchi wa Wilaya hizo ambapo awali walikuwa wakisafiri umbali mrefu kufuata huduma za Mahakama Buhigwe (Kasulu), Uvinza (Kigoma) na Kakonko (Kibondo).

Aidha; majengo hayo yanayojengwa yatakuwa wezeshi katika miundombinu ya TEHAMA ikiwa ni utekelezaji wa Mpango Mkakati mpya wa Mahakama ya Tanzania wa miaka mitano (5) (2020/2021-2024/2025).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (kushoto) akisikiliza maelezo kuhusu ramani ya ujenzi wa Mahakama ya Wilaya Uvinza kutoka kwa  Fundi Mchundo Bw. Edwin Lucas alipotembelea Mradi huo. Katikati ni Mtendaji wa Mahakama Kuu- Kanda ya Kigoma, Bw. Moses Mashaka.

 Msimamizi wa Mradi 'Site Manager', Bw. Kusundwa Kusundwa akitoa ufafanuzi wa mradi wa Ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Buhigwe mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Jaji Lameck Mlacha. Wa kwanza kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Kigoma, Bw. Moses Mashaka na wa pili  kushoto ni Naibu Msajili, Mhe. Gadiel  Mariki.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck  Mlacha akikagua mradi wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe. Mbele yake Msimamizi wa Mradi 'Site Manager', Bw. Kusundwa Kusundwa wakati alipotembelea huo tarehe 05 Februari, 2022.

Mtendaji wa Mahakama Kuu-Kanda ya Kigoma, Bw. Moses Mashaka akielezea jambo mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Jaji Lameck Mlacha (katikati) na Wakandarasi wa 'Lucas Construction Co LTD'  alipotembelea mradi wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya Uvinza.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni