Jumatano, 2 Februari 2022

MAHAKAMA YA TANZANIA YAVUNA FAIDA LUKUKI MATUMIZI YA TEKNOLOJIA

Na Faustine Kapama – Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ameainisha faida lukuki ambazo Mahakama ya Tanzania imezipata kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa katika matumizi ya teknolojia, ikiwemo kuharakisha utoaji wa haki na pia kuokoa zaidi ya shilingi billioni 2.750 za Kitanzania, kiasi ambacho kingetumika wakati wa kusikiliza mashauri kwa njia ya kawaida.

Akizungumza leo tarehe 2 Februari, 2022 jijini Dodoma katika maadhimisho ya Siku ya Sheria, kuashiria mwanzo wa mwaka mpya wa shughuli za kimahakama nchini, Mhe. Prof. Juma amewasihi watumishi wa Mahakama na wadau wote katika sekta ya Sheria kuendelea kuvuna faida ya uwekezaji mkubwa katika teknolojia uliofanywa na Serikali katika Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano na Teknolojia.

“Uboreshaji unaoletwa kupitia teknolojia unaorahisisha upatikanaji wa haki kwa kila mtu una faida ya kusogeza huduma za utoaji haki na kuyafikia makundi yasiyojiweza, ambayo kwa kawaida huwa mbali na huduma za kisheria na utoaji haki. Kwa njia hii, haki itapatikana kwa mizani ya usawa. Baada ya kutungwa Sheria na Kanuni wezeshi, Mahakama ya Tanzania imeanza safari ya kuelekea Mahakama Mtandao kwa lengo kuu la kuleta ufanisi, uwazi na kuwapunguzia gharama wananchi na watumiaji wengine wa huduma za utoaji haki,” amesema.

Jaji Mkuu amemweleza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo kuwa uamuzi wa Mahakama wa kutumia teknolojia na kuvuna faida kutoka katika Mapinduzi ya Nne ya Viwanda, ni kuhakikisha kuwa Tanzania inajenga uchumi shindani na utoaji wa haki wenye viwango vinavyokidhi huo ushindani.

“Mahakama ya Tanzania haiwezi kufumbia macho yale yanayoendelea katika jamii wala kubaki nyuma au kuendelea kukumbatia mifumo ya kizamani ya uandishi wa mienendo mahakamani kwa mikono wakati Akili Bandia ipo kuweza kufanya kazi hiyo kwa wepesi na bila gharama. Mahakama ya Tanzania haiwezi kubaki katika zama za kianolojia iliyopitwa na wakati katika mfumo wa utoaji haki,” amesema.

Jaji Mkuu amesema kuwa muda huu kabla ya mwisho wa robo ya kwanza ya Karne hii ya 21 ndio wakati sahihi kwa Mahakama ya Tanzania, kwa kushirikiana na Mihimili ya Serikali na Bunge, kuanzisha mifumo ya kimahakama ya kidijitali kwa ajili ya utatuzi wa migogoro ya kibiashara inayofanyika kidijitali.

Amesema uwekezaji uliofanywa na Serikali ya Tanzania katika Mkongo wa Mawasiliano wa Taifa umewezesha Mahakama kuunganishwa vituo zaidi ya 157 kwenye Mkongo huo, ambapo kunganishwa huko kumepanua matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika ngazi zote za Mahakama ya Tanzania na imewezesha upatikanaji wa haki kwa wakati.

“Kupitia Mkongo (huu wa Taifa), Mahakama ya Tanzania imesogeza huduma (zake) karibu zaidi na wananchi. Aidha, mifumo ya kielektroniki imeweka mazingira ambayo yamewezesha kubadilishana taarifa kati ya Mahakama, taasisi na wadau katika mfumo mzima wa utoaji haki nchini,” Mhe. Prof. Juma amesema.

Amemweleza Rais Samia pia kuwa moja ya mafanikio makubwa ya matumizi ya TEHAMA katika shughuli za utoaji haki ni kuwepo kwa mfumo wa Kielekitroniki wa Kusajili na Kuratibu Mashauri (JSDS2) uliozinduliwa mwaka 2019 ambao umewezesha na kurahisisha usajili wa mashauri, Majaji na Mahakimu Wafawidhi kuwapangia Majaji na Mahakimu mashauri ya kusikiliza na utayarishaji wa kumbukumbu za mashauri kuanzia yanaposajiliwa hadi hatua ya kutolewa hukumu au uamuzi.

Kwa mujibu wa Jaji Mkuu, kumekuwepo na usajili wa mashauri kwa njia ya mtandao unaowawezesha wadaawa na wadau walio mbali na vituo vya Mahakama kusajili mashauri, nyaraka na viambatanishi wakati wowote ule na kusambaza taarifa za mashauri kwa wahusika kupitia ujumbe mfupi.

Amesema kuwa mbali na kuunganishwa na ule wa malipo ya Serikali (GePG) kuwezesha kulipa tozo, ada na faini kwa njia ya mtandao, mfumo wa JSDS2 umerahisisha ukusanyaji wa takwimu za mashauri yaliyofunguliwa katika ngazi yoyote ya Mahakama kwa njia za kawaida au mitandao pamoja na upakuaji wa taarifa zote zinazohusika, ikiwemo mlundikano, mashauri yaliyotolewa uamuzi, yanayoendelea na yale ambayo hayajapangwa kwa Majaji au Mahakimu.

Jaji Mkuu amesema pia kuwa uwekezaji katika TEHAMA umeiwezesha Mahakama kuwa na mfumo wa Usajili, Usimamizi na Utambuzi wa Mawakili ambao unawapambanua wenye leseni hai na kustahili kutoa huduma za Uwakili. Amebainisha kuwa huduma nyingine ni upatikanaji wa uamuzi unaotolewa na Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani kwa kupitia mfumo wa TANZLII na uwepo wa tovuti ya Mahakama yenye taarifa muhimu kwa wadau, wadaawa, watumiaji wa huduma za Mahakama na wananchi wengine kwa ujumla.

Amesema kuwa Mahakama ya Tanzania inatumia mfumo unaotekeleza majukumu mbalimbali yanayohusisha vikao kwa njia ya video bila wahusika kulazimika kukutana ana kwa ana, teknolojia ambayo hutumika kuendesha mashauri na kutoa mafunzo mbalimbali kwa watumishi na wadau wengine.

“Mfumo huu umesimikwa katika vituo vya Mahakama na pia katika baadhi ya Magereza. Kwa mwaka 2021 pekee, jumla ya mashauri 17,979 yalisikilizwa kwa kutumia mfumo huu. Matumizi ya (mfumo huu) yanakadiriwa kuokoa kiasi cha shilingi 2,750,092,736 za Kitanzania kwa mwaka kwa upande wa Magereza, Mawakili, Mahakama na wadau wengine,” amesema.

Baadaye, Jaji Mkuu alikagua gwaride maalum la heshima lililoandaliwa na Jeshi la Polisi Tanzania kuashiria kuanza rasmi kwa shughuli za kimahakama katika ngazi zote kwa mwaka 2022 kote nchini.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza na wananchi katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yalichofanyika kitaifa jijini Dodoma leo tarehe 2 Februari, 2022. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya siku hiyo.

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson akitoa salamu katika maadhimisho hayo.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani wakifuatilia matukio mbalimbali katika maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika kitaifa jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman (kulia) akiwa pamoja na maafisa waandamizi wa Mahakama ya Tanzania wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria leo tarehe 2 Februari, 2022 jinini Dodoma. Kutoka kulia kwa Mhe. Chande ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili Mkuu, Mhe. Wilbert Martin Chuma na Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Kevin Mhina. 

Sehemu ya wananchi na viongozi wengine wa Mahakama ya Tanzania na taasisi zingine wakifuatilia matukio mbalimbali kwenye maadhimisho hayo.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akikagua gwaride lililoandaliwa na Jeshi la Polisi Tanzania kuashiria kuanza rasmi kwa shughuli za kimahakama kwa mwaka 2022.
Kikundi cha Kwaya ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Masijala Kuu kikitumbuiza katika maadhimisho hayo.
Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan (aliyekaa katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania. Waliokaa kutoka kulia kwa Rais Samia ni Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. George Simbachawene. Kutoka kushoto kwa Rais Samia ni Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Kaimu Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija.
Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan (aliyekaa katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania. 

Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan (aliyekaa katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu wa wanafunzi kutoka Shule ya Sekondari Msalato waliohudhuria maadhimisho hayo

                       (Picha na Mary Gwera na Innocent Kansha - Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni