Jumatano, 2 Februari 2022

WADAU WASIACHWE NYUMA KATIKA SAFARI YA MAHAKAMA MTANDAO: JAJI MKUU

Na Innocent Kansha – Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewaambia wadau wa haki nchini kwamba katika zama za mapinduzi ya nne ya viwanda matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika utoaji haki hayaepukiki kwa kuwa suala hilo ni mtambuka.

Akizungumza katika kilele cha siku ya Sheria nchini, leo tarehe 2 Februari, 2022 katika Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma, Mhe. Prof. Juma alisema, wadau wote katika mnyororo wa haki wana jukumu la kuhakikisha TEHAMA inatawala mchakato mzima wa utaoji haki katika hatua zote za uendeshaji wa mashauri na Mahakama ikitembea yenyewe haitafika mbali.

“Safari ya kuelekea Mahakama Mtandao haiwezi kamwe kufikiwa ikiwa wadau wa Mahakama watabaki nyuma. Nichukue fursa hii kuwapongeza wadau wote wa Mahakama ambao wameanza kuchukua hatua ya kuelekea katika matumizi ya TEHAMA”, alisema Jaji Mkuu

Mhe. Prof. Juma aliwaomba wadau wote wa Mahakama nchini kuchukua hatua za makusudi sio tu kuunga mkono juhudi za Mahakama katika matumizi ya TEHAMA bali nao watumie mfumo huo katika kutoa huduma zao.

Aidha, Jaji Mkuu alikiri kuwa pamoja na jitihada za Mahakama za kutumia TEHAMA katika utoaji haki, bado zipo sheria nyingi zinazokinzana na matumizi ya mfumo huo katika utoaji haki nchini. Miongoni mwa sheria hizo ni sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Madai na Sheria ya Ushahidi kwa kutaja chache.

“Nimeshamuomba Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwasiliana na Uongozi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kuangalia uwezekano wa kuzifanyia marekebisho sheria hizo ziendane na hali ya sasa”, alisema Jaji Mkuu

Mhe. Prof. Juma alisema, Mahakama imefanya marekebisho ya kanuni kadhaa za Jaji Mkuu na kutunga kanuni mbili yaani Kanuni za ufunguaji wa mashauri kwa njia ya mtandao “The Judicature and Application of laws Electronic Failing Rules 2018”. Pamoja na Kanuni za usikilizaji wa Mashauri kwa njia ya mtandao “The Judicature and Application of laws Remote Proceedings and Electronic Recording Rules 2021”.

Jaji Mkuu aliongeza kuwa, Mahakama inaufanyia maboresho makubwa mfumo wake wa Menejimenti ya Mashauri (JSDS II) ili kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia. Mfumo huu mpya utakuwa na hadhi ya “Advanced Case Management”. Mfumo huo hautaruhusu ufunguaji wa mashauri kwa njia ya kawaida.

Mfumo huo utakuwa na uwezo wa kutengeneza jalada la ki – elektroniki la shauri “Electronic case file” na utawezesha ubadilishanaji wa majalada ya mashauri kwa njia hiyo na kuweka saini ya ki – elektroniki kwenye kumbukumbu “Digital Signature”, mfumo huo unatarajiwa kutumiwa hadi ngazi za Mahakama za Mwanzo.

“Mategemeo yetu ni kuwa mafanikio ya mikakati yetu hiyo miwili itatufikisha katika hatua ya kutotumia karatasi “Paperless Court” mpango ambao tumeuanza kwa majaribio katika Mahakama ya Wilaya Kigamboni na kupata mafanikio na tumejifunza maeneo ya kuboresha”, alisisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Prof. Juma akadokeza mpango wa Mahakama wa kuanzisha kambi za mahema ya utoaji haki “Justice Tents Camp” zitakazo tumika hasa katika maeneo yaliyopo mbali na huduma za Mahakama  na kwamba yatakuwa na uratibu  wa kuwekwa kwa ratiba  maalum kutokana na mahitaji. Amesema kuwa Mahakama hizo zitakuwa na Mahakimu na Majaji wasiokuwa na mipaka “Borderless Judges and Magistartes” hii nikutambua kuwa kuna makundi ambayo sio rahisi kufikiwa na huduma za Mahakama kutokana na jiografia yao na shughuli zao.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akihutubia katika kilele cha Maadhimisho ya siku ya Sheria nchini yaliyofanyika kitaifa katika Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali leo tarehe 2 Februari, 2022. Na Mgeni rasmi katika Maadhimisho hayo alikuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

  

Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Mkuu ya Tanzania, wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akihutubia katika kilele cha Maadhimisho ya siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma.


Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan (aliyekaa katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania. Waliokaa kutoka kulia kwa Rais Samia ni Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. George Simbachawene. Kutoka kushoto kwa Rais Samia ni Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Kaimu Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija.



Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson akitoa salamu katika maadhimisho hayo.

Mwansheria Mkuu wa Serikali Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akihutubia katika kilele cha Maadhimisho ya siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma.

 Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan (aliyekaa katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania. 


 Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akikagua gwaride      lililoandaliwa na Jeshi la Polisi Tanzania kuashiria kuanza rasmi kwa shughuli za kimahakama kwa mwaka 2022.


Sehemu ya wananchi na viongozi wengine wa Mahakama ya Tanzania na taasisi zingine wakifuatilia matukio mbalimbali kwenye maadhimisho hayo.


Jaji Mkuu wa Tanzania Mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman (kulia) akiwa pamoja na maafisa waandamizi wa Mahakama ya Tanzania wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria leo tarehe 2 Februari, 2022 jinini Dodoma. Kutoka kulia kwa Mhe. Chande ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili Mkuu, Mhe. Wilbert Martin Chuma na Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Kevin Mhina. 

Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan (aliyekaa katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu wa wanafunzi kutoka Shule ya Sekondari Msalato waliohudhuria maadhimisho hayo


 Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania walishiriki katika Maadhimisho hayo

Kikundi cha Kwaya ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Masijala Kuu kikitumbuiza katika maadhimisho hayo.

(Picha na Innocent kansha na Mary Gwera - Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni