Jumatano, 2 Februari 2022

RAIS SAMIA AIPONGEZA MAHAKAMA KWA PROGRAMU YA KUTAFSIRI SHERIA

  Na Lydia Churi-Mahakama

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kujikita katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ikiwemo kutafuta program maalum ya kutafsiri sheria kwa lugha ya Kiswahili kwa lengo la kuimarisha matumizi ya lugha hiyo katika kutoa huduma za kimahakama.

Akizungumza kwenye kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika kitaifa leo tarehe 2 Februari, 2022 katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, Rais Samia amesema program hiyo itakayotumiwa na Mahakama katika kurahisisha shughuli za utoaji haki pia itatoa nafasi kwa lugha ya Kiswahili kupata tafsiri na unukuzi kwa lugha ya Kiingereza pamoja na lugha nyingine za kigeni.

Rais Samia ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo alisema Serikali inaunga mkono kikamilifu jitihada zinazofanywa na Mhimili wa Mahakama katika kuwekeza kwenye Teknolojia na kuwataka viongozi wa Mahakama kuongeza kasi kwenye matumizi hayo ili kurahisisha shughuli za utoaji haki.

Alisema Mahakama ya Tanzania imepiga hatua kubwa kwenye matumizi ya TEHAMA hususani katika kutengeneza mifumo yake mbalimbali ya kurahisisha kazi ya utoaji haki ukiwemo ule wa kuhifadhi maamuzi mbalimbali yanayotolewa na Majaji (Tanzlii) na kuongeza kuwa mfumo huu utasaidia kuongeza uwazi wa uamuzi wa Mahakama unaotolewa kwenye mashauri mbalimbali.

Aidha, Rais Samia ametoa wito kwa Sekta ya Sheria nchini kuwatayarisha wahitimu na kuwaongezea ujuzi wanasheria walioko makazini ili waendane na wimbi la ukuaji wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.

“Dunia iko kwenye Mapinduzi ya Nne ya Viwanda yanayoongozwa na matumizi ya TEHAMA, hivyo uchumi wa dunia pamoja na shughuli mbalimbali zikiwemo za utoaji haki zinaendeshwa kwa kutumia Teknolojia hiyo”, alisema Rais Samia.

Amezitaka wizara za Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari pamoja na Wizara ya Elimu, Sayansi na Vyuo Vikuu vyote kuhakikisha wanafunzi kuanzia shule za msingi hadi vyuo vikuu wanapatiwa ujuzi ili kuwaandaa kufanya kazi zinazohitaji ujuzi unaolingana na matakwa ya mabadiliko ya Teknolojia.

Alisema wakati tulionao sasa unahitaji mabadiliko makubwa ya kifikra na kuzalisha nguvu kazi yenye ujuzi linganifu na mabadiliko ya teknolojia duniani. “Tanzania haiwezi kubaki nje ya Mapinduzi ya Nne ya Viwanda ambayo yanaendelea kubadilisha mizani ya ushindani katika shughuli zote za kibinadamu zikiwemo za uwekezaji na mazingira ya biashara”, alisema.         

Rais Samia pia amewataka Majaji na Mahakimu kutekeleza wajibu wao kwa kuzingatia Sheria na Katiba ya nchi na kutenda haki kwa watu wote bila kuangalia hali ya mtu kiuchumi na kijamii.

Naye Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi ameziomba Wizara za Nishati na ile ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kutoa huduma za uhakika ili kuiwezesha Mahakama ya Tanzania pamoja na sekta ya sheria kwa ujumla kutumia Tehama katika kurahisisha shughuli za utoaji haki.

Alizitaja faida za kutumia Teknolojia hiyo kuwa ni pamoja na kuokoa muda na gharama, kuhifadhi kumbukumbu na kupata taarifa za mashauri kwa urahisi. Aliongeza kuwa safari ya uboreshaji wa kimtandao haina budi kushirikisha wadau wote ili kuleta ufanisi.

             
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia kwenye kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na siku ya Sheria nchini yaliyofanyika leo katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Sehemu ya Waheshimiwa Majaji wa Mahakama ya Rufani pamoja na Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa kwenye kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na siku ya Sheria nchini yaliyofanyika leo katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Sehemu ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania na wadau waliohudhuria sherehe za kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na siku ya Sheria nchini iliyofanyika leo katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akizungumza wakati wa sherehe za kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na siku ya Sheria nchini leo katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Rais wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) Mhe. Prof. Edward Hosea akizungumza wakati wa sherehe za kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na siku ya Sheria nchini leo katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Sehemu ya Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini leo katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa katika picha ya pamoja na Wakuu wa Taasisi waliohudhuria kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na siku ya Sheria nchini leo katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma. Wa tatu kulia ni Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Tulia Ackson na wa tatu kushoto ni Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.
Wakuu wa Ulinzi na Usalama nchini wakiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan wakati wa sherehe za kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na siku ya Sheria nchini leo katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.

Waheshimiwa Majaji Wastaafu wa Mahakama ya Rufani pamoja na Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Waheshimiwa Mawaziri waliohudhuria Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini wakiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.















Hakuna maoni:

Chapisha Maoni