Jumatatu, 21 Machi 2022

MAHAKAMA KANDA YA MUSOMA KUNG’ARISHA MAJENGO MAHAKAMA ZA MWANZO

 Na. Francisca Swai - Musoma

Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Musoma, inaendesha zoezi la kuboresha majengo ya Mahakama za Mwanzo kupitia fedha za matumizi ya kawaida ili kuimarisha miundombinu hiyo na kuweka mazingira bora ya kufanyia kazi yanayochochea usikilizaji wa mashauri kwa urahisi na haraka kwa wananachi.

Hayo yalibainika katika siku ya tatu ya ziara anayofanya  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, kukagua shughuli mbalimbali za kimahakama na kujionea ukarabati wa majengo hayo unaoendelea.

Akiwa katika Mahakama ya Mwanzo Ngoreme, Mhe.  Mtulya amempongeza Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma, Bw. Festo Chonya kwa usimamizi mzuri wa rasilimali fedha ambao umeleta matokeo chanya na mabadiliko makubwa katika miundombinu na mazingira ya Mahakama kwa ujumla.

Mahakama ya Mwanzo Ngoreme iliyopo wilayani Serengeti ambayo ilikuwa katika hali mbaya ni moja kati ya Mahakama tatu zilizokuwa katika mpango wa uboreshaji wa miundombinu kupitia fedha za matumizi ya kawaida (OC) kwa mwaka 2021/2022 uliowekwa na uongozi wa Kanda ya Musoma.

Baadhi ya Mahakama zilizofanyiwa ukarabati mkubwa kupitia fedha za hizo ni pamoja na Mahakama ya Mwanzo Bunda Mjini, Mahakama ya Mwanzo Kukirango na Mahakama ya Mwanzo Ngoreme. Pia zipo Mahakama zilizofanyiwa uboreshaji mdogo mdogo, ikiwemo ili kuimarisha miundombinu yake.

Mahakama hizo ni Mahakama ya Mwanzo Musoma Mjini, Mahakama ya Mwanzo Kabasa, Mahakama ya Mwanzo Kinesi pamoja na Mahakama ya Mwanzo Nyaburongo.

Aidha, Jaji Mfawidhi huyo amewapongeza Mahakimu na watumishi kwa utendaji kazi mzuri unaoridhisha na kuwasisitiza Mahakimu kusikiliza mashauri kwa kufuata taratibu na kuyamaliza kwa wakati.

Amemwelekeza Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma, Mhe. Frank Moshi kuwaandikia barua za pongezi Mahakimu wote wanaofanya kazi vizuri katika eneo hilo, huku akielekeza kuandikiwa barua Mahakimu wote wanaobaki nyuma ili waeleze changamoto walizonazo ziweze kutatuliwa kwa pamoja.

Akipokea pongezi hizo zilizotolewa, Mtendaji huyo wa Mahakama Kuu wa Kanda aliwashukuru na kuwapongeza maafisa Tawala na Utumishi wa maeneo husika kwa usimamizi wa karibu wa uboreshaji huo.

Alitolea mfano wa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Ngoreme, Mhe. Peter Malima na Mlinzi wa Mahakama hiyo, Bw. Chacha Nsaho ambao wamekuwa msaada mkubwa na waaminifu katika kusimamia mafundi pamoja na vifaa vinavyotumika katika ujenzi huo.

Alimhakikishia Jaji Mfawidhi kuwa ukarabati wa majengo ya Mahakama katika Kanda yake utaendelea kadri upatikanaji wa fedha unavyoruhusu.

Muonekano wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Ngoreme ambapo ujenzi unaendelea kwa kutumia fedha za matumizi ya kawaida (OC).

Muonekano wa zamani wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Ngoreme lililokuwa na changamoto ya paa na uchakavu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akikabidhi vitendea kazi kwa HakimuMkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Ngoreme, Mhe. Adam Malima (kushoto) na Mlinzi wa Mahakama hiyo, Bw. Chacha Nsaho (kulia). Watumishi hawa walipongezwa kwa uaminifu katika usimamizi wa ujenzi unaoendelea wa Mahakama ya Mwanzo Ngoreme.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya ( kulia) akiongea na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Nyamwaga akiwemo Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mhe. Adeline Kashushura (wa tatu kulia) na Msaidizi wa Ofisi, Bw. Jasper Mrema (mwenye shati jeupe). Amewapongeza kwa utunzaji mzuri wa mazingira na kulinda mipaka ya eneo la Mahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Kenyana, Mhe. Ileon Ponella (kushoto) na Diwani wa Kata ya Ring’wani iliyopo Mahakama hiyo, Mhe. Hellena Chacha.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akimwelekeza jambo fundi msimamizi wa ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Ngoreme, Bw. Alex Kicha (kulia) wakati wa ukaguzi wa ujenzi unaoendelea mahakamani hapo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya akiteta na viongozi wa Kanda pamoja na Mahakama wa Wilaya ya Tarime alipotembelea Mahakama ya Mwanzo Nyamongo.








Hakuna maoni:

Chapisha Maoni