Na Evelina Odemba - Morogoro
Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe amelaani vikali ubakaji
na ulawiti kwa watoto ambao umekithiri katika jamii ambapo ameonya vitendo
hivyo havitavumiliwa.
Mhe. Ngwembe ametoa
msimamo huo jana tarehe 29 Machi, 2022 alipokuwa akitoa elimu ya masuala
mbalimbali ya kisheria kwa wananchi ambao walifika katika Kituo Jumuishi cha
Utoaji Haki mkoani hapa kupata huduma za
Mahakama.
Mahakama Morogoro
imeanzisha utaratibu wa kutoa elimu kwenye masuala mbalimbali ya kisheria kwa
wananchi siku za Jumanne, Jumatano na Alhamisi kuanzia saa 2.00 mpaka saa 3.00
asubuhi kabla ya kuanza shughuli za kimahakama ambapo siku ya jana mada ilihusu
ulinzi kwa mtoto.
Akizungumza na wananchi waliofurika kwenye Kituo hicho kwenye kipindi cha utoaji wa elimu, Mhe. Ngwembe alisema kuwa amefanya
utafiti mkoani Morogoro na kugundua uwepo wa wimbi kubwa la matukio ya ubakaji
kwa watoto chini ya umri wa miaka 18.
Kwa mujibu wa Jaji Mfawidhi
huyo, takwimu zinaonesha kwa mwaka 2021 mashauri yaliyofikishwa mahakamani yanayohusu
ubakaji wa watoto chini ya miaka 18 yanafika 200 na kati ya hayo mashauri 35 yanahusisha
ulawiti kwa watoto na hayo ni kwa Mkoa wa Morogoro peke yake.
“Matukio haya ni ya
kikatili na aibu kubwa, hayavumiliki katika jamii na jambo hili linakemewa vikali
hata katika Mihimili ya Dora nchini ikiwemo Bunge, Serikali na Mahakama, hivyo kila
mmoja katika jamii anawajibika kumlinda mtoto mahali kokote anapokuwa,” alisema.
Mhe. Ngwembe alikumbushia
kuwa ikibainika mtu yeyote ametenda kosa la namna hiyo hupata adhabu kubwa
inayoanzia kifungo cha miaka 30 au kifungo cha maisha jela bila kusahau adhabu
zingine ikiwemo kuchapwa viboko.
Hivyo, Jaji Mfawidhi
huyo amewaasa wananchi wote kujiepusha na vitendo hivyo ili kuwalinda watotot
na kutotumbukia kwenye madhira ya kukumbana na adhabu kali zinazotolewa na
Mahakama kwa mujibu wa sheria zilizopo.
Akimjibu mwananchi mmoja
baada ya kutoa nafasi ya kuuliza maswali, Mhe. Ngwembe aliionya jamii
kutowatumia watoto kutoa ushahidi wa uongo mahakamani kwa lengo la kulipiza
kisasi au chuki kwa watuhumiwa kwani ikigundulika hatua kali za kisheria
zitachukuliwa dhidi ya walalamikaji.
Mwananchi huyo alieleza
changamoto ambayo hujitokeza kwa baadhi ya watu kutunga ushahidi kwa lengo la
kukomoa au kulipiza kisasi, hivyo alitaka kujua hatua zinaweza kuchukuliwa kwa kubambikiwa
kesi za ubakaji na ulawiti kwa watoto.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni