Jumatano, 30 Machi 2022

MAHAKAMA KUSHINDANISHWA UTOAJI HUDUMA BORA KWA WANANCHI

 Na Emmanuel Oguda-Mahakama, Shinyanga

Mahakama ya Tanzania imeandaa mpango mahsusi wa kushindanisha viwango vya utoaji huduma kwa wananchi ili kupata Mahakama ambayo ni bora katika utendaji kazi (Court of Excellence Performance).

Hayo yamebainishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athumani Matuma wakati akiongea na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kahama jana tarehe 29 Machi, 2022 katika siku ya pili ya ziara yake kukagua shughuli mbalimbali za kimahakama.

Mhe. Matuma amewafahamisha watumishi wa Mahakama hiyo kuwa kuna vigezo ambavyo vimeandaliwa vitakavyotumika kushindanisha ubora wa huduma zotolewazo kati ya Mahakama moja na nyingine ambapo mshindi atatambuliwa na kutangazwa.

Amewataka watumishi kutambua kuanzia sasa huduma wanazotoa katika maeneo yao ya kazi zitapimwa kwa vigezo maalum vilivyoainishwa katika muongozo kupima utendaji kazi bora wa kila Mahakama ambapo ile itakayofanya vizuri itatambuliwa na kupewa cheti maalum katika ngazi ya Kitaifa.

Kadhalika, Mhe. Matuma amewafahamisha watumishi kuwa, pamoja na kushindanishwa kitaifa, kutakuwa na ushindani ndani ya Kanda ambapo mshindi anayefanya vizuri katika kutoa huduma bora atatambuliwa na kupewa tuzo maalum.

“Kila mmoja wenu afahamu sasa anayo kazi ya kuhakikisha Mahakama anayofanyia kazi inakuwa ya kwanza katika utendaji kazi na utoaji wa huduma bora kwa wananchi,” alisema Jaji Mfawidhi huyo.

Jaji Matuma amebainisha baadhi ya vigezo vitakavyotumika kupima utendaji bora ni kiwango cha kusikiliza na kumaliza mashauri kwa wakati, kumaliza mlundikano wa mashauri mahakamani, kusikiliza na kutatua malalamiko ya wananchi kwa haraka na  kuhuisha takwimu za mashauri katika mfumo wa JSDS II.

“Hivyo ni fursa kwa kila Mtumishi kujipima na kujitathmini na kuona kuwa kila mmoja ana mchango mkubwa katika kufikia utendaji kazi bora katika eneo lake,” amesema.

Kwa upande wao, watumishi wa Mahakama hiyo wamemuahidi Mhe. Matuma kuwa watafanya kazi kwa nguvu zao zote na kwa ubora unaohitajika ili kuifanya Mahakama ya Wilaya ya Kahama kuwa mfano kwa Mahakama zilizopo Kanda ya Shinyanga na nyinginezo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe Athuman Matuma (katikati) akifafanua jambo wakati wa kikao na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kahama. Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kanda ya Shinyanga, Mhe. Hussein Mushi na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama katika Kanda hiyo, Bi Mavis Miti.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Kahama ambao wameahidi kufanya vizuri kuboresha huduma za Mahakama katika Wilaya ya Kahama.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athuman Matuma akikagua uchapaji wa mienendo ya mashauri katika Mahakama ya Wilaya ya Kahama.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni