Jumatano, 9 Machi 2022

WANAWAKE MAHAKAMA KANDA YA MUSOMA WATEMBELEA WATOTO MAHITAJI MAALUMU

Na Francisca Swai, Mahakama-Musoma 

Watumishi wanawake kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma jana tarehe 8 Machi, 2022 wameungana  na wanawake wote ulimwenguni kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kwa kutembelea vituo vyenye watoto wenye mahitaji maalumu. 

Wakiwa katika vituo hivyo, watumishi hao wametoa vitabu vinavyohusu haki za wanawake na watoto (Women Access to Justice) kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Mwisenge yenye watoto wenye ulemevu wa kuona na ngozi (Albino), Shule ya Msingi Mwembeni yenye watoto wenye ulemavu wa kusikia na Kituo cha kulelea watoto cha Jipe Moyo kilichoko Musoma Mjini.

Mbali na kutembelea vituo hivyo, watumishi hao wanawake wakiongozwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma, Mhe. Eugenia Rujwahuka pia waligawa vitabu hivyo kwa watumishi wengine wa Mahakama katika Kanda hiyo. 

Aidha, watumishi hao baada ya kutembelea vituo hivyo walishiriki katika maadhimisho ya siku ya wanawake duniani yaliyofanyika kimkoa katika Wilaya ya Butiama, hivyo kuungana na wanawake wengine waliohudhuria katika sherehe hizo kutoka taasisi mbalimbali ndani ya Mkoa wa Mara.

Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa Kamishna wa Ardhi Mkoa wa Mara, Bi. Happiness Mtutwa.

Watumishi wa Mahakama, Kanda ya Musoma wakitoa vitabu vya Haki za wanawake na watoto katika kituo cha Jipe Moyo Musoma.

Watumishi wa Mahakama Kuu musoma wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kupata vitabu hivyo. Waliokaa mezani katikati ni  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, kushoto ni  Jaji wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Frank Mahimbali na kulia ni mwakilishi wa TAWJA Kanda ya Musoma, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Mwanzo Musoma Mjini,  Mhe. Prisca Mkeha. 



Watumishi wa Mahakama wakionekana nyuma ya watoto wenye mahitaji maalumu katika Shule ya Msingi Mwisenge iliyopo Musoma Mjini.

Baadhi ya watumishi wa Mahakama Kanda ya Musoma walioshiriki siku ya wanawake duniani Wilayani Butiama.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma, Mhe. Eugenia Rujwahuka akishiriki tendo jema kwa kutoa msaada katika hospitali ya Nyasho iliyopo Musoma Mjini.
Muonekano wa keki (picha ya juu na chini) iliyoandaliwa na Watumishi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni