Jumapili, 3 Aprili 2022

JAJI MFAWIDHI KANDA YA MWANZA APONGEZA KASI YA KUMALIZA MASHAURI MKOANI GEITA

 Na Charles Philipo Ngusa- Mahakama  Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza, Mhe. Jaji John Kahyoza  amepongeza juhudi zinazoendelea kufanywa na Mahakimu katika Mkoa wa Geita, hususani katika kusikiliza mashauri kwa haraka, hivyo kutekeleza kwa vitendo azima ya Mahakama katika kutoa haki kwa wananchi kwa wakati.

Akizungumza na watumishi mkoani humo Mhe. Kahyoza amesema kuwa pamoja na mkakati uliowekwa na Kanda wa kumaliza mashauri katika Mahakama za Mwanzo ndani ya miezi mitatu, wao wameenda mbali zaidi kwa kujiwekea malengo kumaliza mashauri katika Mahakama hizo ndani ya mwezi mmoja, jambo ambalo wameliweza, hivyo kuwa mfano ndani ya Kanda hiyo.

“Mashauri mengi ndani ya Mkoa huu yamekuwa yakimalizika ndani ya wiki moja, jambo ambalo limewafanya wananchi kuona kuwa Mahakama imekuwa kimbilio la watu kwani mashauri yao yanamalizika haraka na kuruhusu waendelee na majukumu yao mengine,” alisema wakati alipokuwa kwenye ziara ya siku nne iliyoanza tarehe 28 Machi, 2022.

Alibainisha kuwa Mahakimu hao wamekubaliana shauri linapowasilishwa mahakamani  kabla halijakubaliwa lazima mashahidi na wahusika wawepo na mara baada ya kufunguliwa huanza kusikilizwa siku hiyo na kutolewa hukumu au uamuzi kwa haraka ili kila mmoja apate haki yake, hivyo kutoa fursa kwa wahusika kwenda kuendelea na shughuli zao za uzalishaji mali.

“Kwa kufanya hivyo wameifanya Mahakama kuwa kimbilio la watu kwani wanaamini wakifika mahakamani mashauri yao yanamalizika ndani ya muda mfupi bila kupoteza muda wao,” Mhe. Kahyoza alisema.

Akiwa katika ziara yake, Jaji Mfawidhi huyo alipata nafasi ya kumtembelea Mkuu wa Wilaya ya Geita, Mhe. Wilson Shimo, ambaye alimpongeza Mhe. Kahyoza kwa kusimamia maadili na uchapaji kazi ulio bora kwani kwa sasa Mahakimu wamekuwa wakitekeleza majukumu yao kikamilifu.

“Hatua hii imepunguza malalamiko katika ofisi yangu ikilinganishwa na siku za mwanzo ambapo tulikuwa tukipokea malalamiko mengi sana ndani ya wiki moja lakini kwa sasa tunaweza kupokea lalamiko moja au hamna kabisa,” alisema Mkuu huyo wa Wilaya.

Kadhalika, Mhe. Shimo alisema kuwa kutokana na wananchi kuridhishwa na huduma za kimahakama, wamekuwa na mwamko mkubwa katika ushiriki wa shughuli mbalimbali za Mahakama kama vile ujenzi na ukarabati wa miundombinu mbalimbali.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza, Mhe. Jaji John Kahyoza (aliyesimama) akielezea jambo kwa watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chato(hawapo pichani),akiwemo Hakimu Mkazi Mfawidhi Mhe. Amalia Mushi (kushoto) na Naibu Msajili Mfawidhi, Kanda ya Mwanza, Mhe. Chiganga Tengwa(wa pili kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Mkoa wa Geita, Bw. Nestory Mujunangoma(kulia).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza, Mhe. Jaji John Kahyoza (kulia) akiwa katika ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Geita, Mhe. Wilson Shimo (kushoto) alipomtembelea ofisini kwake wakati alipokuwa kwenye ziara yake ya Mahakama kukagua shughuli mbalimbali za kimahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza, Mhe. Jaji John Kahyoza (katikati) akiwa na baadhi ya watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Katoro wakati wa ziara yake.

Watumishi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita wakimsikiliza kwa makini Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza, Mhe. Jaji John Kahyoza  katika kikao cha majumuisho cha ziara yake.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni