Jumamosi, 2 Aprili 2022

JAJI MDEMU AHIMIZA MAHAKIMU WAFAWIDHI KUZINGATIA MAADILI, NIDHAMU KATIKA KAZI

 Na Angel Meela-Mahakama, Arusha

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu amewahimiza Mahakimu Wakazi Wafawidhi kuendelea kuzingatia maadili na Nnidhamu ya hali ya juu wanapotekeleza majukumu yao ya utoaji haki kwa wananchi.

Mhe. Mdemu alitoa wito huo jana tarehe 1 Aprili, 2022 alipokuwa akifungua mafunzo ya siku mbili kwa viongozi hao wa Mahakama yanayofanyika katika ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Arusha. Jaji Mdemu alimwakilisha Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani katika ufunguzi huo.

Alisema ni ukweli usiopingika kwamba uadilifu ndio chachu ya mafanikio na utendaji bora katika sehemu yeyote ya kazi, hivyo maadili na nidhamu kwa mtumishi ni muhimu kwa mustakabali wa taasisi inayotarajia mafanikio, kwani mambo hayo hujenga imani kwa wadau wake.

“Kwa vyombo vya utoaji haki kama Mahakama kukosa uadilifu hupelekea kuvunjika kwa imani ya wananchi na hivyo kuathiri dhana nzima  ya utawala na sheria. Hivyo basi kujenga  na kuimarisha maadili ya maafisa wa mahakama ni jukumu la msingi la taasisi ya Mahakama kama ilivyo kwa taasisi nyingine yeyote duniani,” Jaji Mfawidhi huyo alisema.

Akinukuu maneno ya  mwanazuoni mmoja na Rais wa Mahakama ya Katiba ya Poland kuhusu maadili Mhe. Mdemu alisema, "kuwa Hakimu au Jaji ni nafasi nzuri na inayopendwa kama ilivyo kuwa daktari au mwanazuoni.

“Lakini Ujaji au Uhakimu sio kazi nzuri kwa watu wasio na maadili ya kitaaluma au binafsi, uaminifu, historia safi ya maisha yao ya nyuma, ujuzi wa taaluma na utendaji bora, ukomavu binafsi, kifamilia na jamii kwa ujumla, ili kuweza kuwajibika kwa kila maamuzi wanayotoa kulingana na sheria na dhamira zao binafsi."

Jaji Mfawidhi huyo aliendelea kwa kusema kuwa ni dhahiri mtu anaefanya kazi ya Uhakimu hana budi kuishi maisha ya kujizuia, kinyume na mtu mwingine wa kawaida kwa vile jamii inatarajia Jaji au Hakimu kuwa mtu mwenye kiwango cha juu kabisa cha uadilifu ili aweze kuaminika katika kazi yake ya kutoa haki.

“Hivyo ninyi kuchagua kuwa Mahakimu, mmekubali pia kuwa maisha yenu hatatakua binafsi. Wananchi wana haki ya kufuatilia mienendo yenu na kutoa maoni iwapo hawajaridhika na mienendo yenu,” alisema.

Mhe. Mdemu alieleza kuwa maadili ya Mahakimu ni eneo pana ambalo linahusu maisha ya kila siku wakati wa kazi. Mhe Jaji aliwakumbusha kwamba suala la maadili ya maafisa wa Mahakama ni mojawapo ya vipaumbele katika progamu ya uboreshaji wa Mahakama Tanzania unaolenga kujenga imani ya wananchi na ushiriki wa wadau.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu (wa nne kulia) ikiwa katika picha ya pamoja na seheme ya Mahakimu Wakazi Wafawidhi.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu (wa nne kulia) ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Arusha pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Arusha.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu (wa nne kulia) (picha ya juu na chini) ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji na Naibu Msajili .

Mkuu wa Kitengo cha Uboreshaji Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha akifafanua jambo wakati wa mafunzo hayo. 
Sehemu ya washiriki wakifuatilia mafunzo hayo.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni