Jumamosi, 2 Aprili 2022

NAIBU MSAJILI SUMBAWANGA AHIMIZA WADAU HAKI JINAI KUSHIRIKIANA

 Na Mayanga Someke – Mahakama, Sumbawanga.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Maira Kasonde ametoa rai kwa wadau wote wa Haki Jinai Mkoa wa Rukwa kushirikiana ili kumaliza mlundikano wa mashauri yaliyopo mahakamani.

Akizungumza katika kikao cha kusukuma mashauri kilichofanyika hivi karibuni kwenye ofisi yake, Mhe.Kasonde aliwaaasa wadau wote kutimiza wajibu wao ili kutokwamisha mnyororo wa upatikanaji haki pindi mashauri yanapokuwa yamewasilishwa mahakamani.

Ninyi nyote mliopo hapa hakikisheni mnashirikiana ili kuharakisha upatikanaji wa haki kwa wakati kwa wananchi. Mahakama peke yake haiwezi kufanya kazi bila kushirikiana na wadau wengine. Mmoja wenu atasababisha wengine kukwama kama atashindwa kutimiza wajibu wake,” alisema.

Aliwaambia wadau hao kuwa ni aibu kuona mashauri yamekwama kusikilizwa kwa sababu mmoja ameshindwa kutimiza wajibu wake, hivyo ni muhimu kushirikiana kwa pamoja ili mashauri hayo yamalizike kwa haraka.

“Lazima tufanye kazi kwa maslahi mapana ya utoaji haki kwa wadau wetu ili kulinda taswira na heshima ya Mahakama,” alisema.

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Rukwa, Bi. Veronica Myovela aliwaambia wajumbe wa kikao hicho kuwa wameweka mikakati yao hadi kufikia tarehe 30 Aprili,2022 upelelezi wa kesi zilizokuwa zikijadiliwa utakuwa umekamilika.

Naye Kaimu Mkuu wa Waendesha Mashtaka katika Mkoa huo, Bw, Simon Peres amewahakikishia wadau wa haki jinai kuwa maazimio yote yaliyofikiwa na Kikao hicho yanayohusu Ofisi ya Taifa ya Mashtaka yatatekelezwa kikamilifu.


 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Maira Kasonde akizungumza na wadau wa Haki Jinai katika kikao cha kusukuma mashauri ya mlundikano mahakamani.
sehemu ya wadau wa Haki Jinai (picha ya juu na chini) wakimsikiliza Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Maira Kasonde.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni