Ijumaa, 1 Aprili 2022

JAJI MFAWIDHI SHINYANGA AHIMIZA KASI UJENZI MAHAKAMA ZA WILAYA YA ITILIMA, BUSEGA

 Na Emmanuel Oguda-Mahakama, Shinyanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe Athuman Matuma amemtaka Mkandarasi anayejenga Mahakama za Wilaya ya Itilima na Busega Mkoani Simiyu kukamilisha kazi hizo kwa wakati na kiwango kinachotakiwa kwa mujibu wa Mkataba.

Akiongea na Wasimamizi wa Mkandarasi huyo, United Builders Limited (UBL), katika ziara ya kukagua miradi hiyo tarehe 30 Machi, 2022, Mhe. Matuma amehimiza kukamilishwa kwa wakati ujenzi wa Mahakama hizo ili kusogeza huduma karibu na wananchi.

Amesema hatua hiyo itatoa fursa kwa wakazi wa Wilaya husika kupata huduma za kimahakama katika maeneo yao tofauti na hali ilivyo sasa ambapo wanalazimika kusafiriki umbali mrefu na kutumia gharama kubwa kutafuta haki katika Wilaya ya Bariadi Mkoani Simiyu.

‘’Lengo la Jaji Mkuu wa Tanzania ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kimahakama katika maeneo wanayoishi pasipo usumbufu na bila gharama yoyote’ alisema Jaji Matuma.

Aliwaeleza Wasimamizi wa Mkandarasi huyo kwenda na kasi ya Mahakama ya kutoa huduma kwa wananchi kwa wakati na kwa kiwango kinachoridhisha, hivyo anatakiwa kutumia nguvu zake zote ili kuikamilisha kazi hiyo kwa haraka.

‘’Mkandarasi aongeze nguvu kazi kwa kuwa muda wa mkataba uliobaki ni mchache ikilinganishwa na nguvu kazi iliyopo hivi sasa,’’ aliongeza Jaji Matuma.

Aidha, Jaji Mfawidhi huyo alimuagiza Hakimu Mkazi Mfawidhi na Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu kusimamia kwa karibu makubaliano ya ujenzi wa Mahakama hizo na kuhakikisha unakamilika mwezi Aprili, 2022 kulingana na Mkataba ili Mahakama hizo zianze kutoa huduma kwa wananchi.

Awali, wananchi wa Wilaya ya Busega ambao husafiri takribani kilometa 130 kupata huduma za kimahakama mjini Bariadi walimueleza Jaji Mfawidhi huyo adha wanayoipata kutokana na kukosekana kwa huduma za Mahakama ya Wilaya Busega.

Mahakama ya Tanzania inatekeleza ujenzi wa Mahakama za Wilaya mbalimbali kupitia Mpango wa Uboreshaji wa Mahakama uliopo ndani ya Mpango Mkakati wa Mahakama (JSP) Awamu ya pili wa mwaka 2020/2021 – 2024/2025 ambapo ujenzi wa Mahakama za Wilaya ya Itilima na Busega ni sehemu ya mpango huo.


Muonekano wa jengo la Mahakama ya Wilaya Busega linaloendelea kujengwa katika Wilaya ya Busega Mkoani Simiyu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe Athuman Matuma (kulia) akipata maelezo ya mradi wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Itilima kutoka kwa msimamizi wa mradi huo wakati alipotembelea mradi huo hivi karibuni.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu, Bw. Gasto Knyairita (kulia) akitoa maelezo ya mradi wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Busega Mkoani Simiyu kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Shinyanga, Mhe Athuman Matuma alipoembelea maendeleo ya ujenzi wa Mahakama hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzanua, Kanda ya Shinyanga Mhe. Athuman Matuma (kushoto) akipata maelezo ya mradi wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Busega kutoka kwa Msimamizi wa mradi huo wakati alipotembelea ujenzi wa Mahakama hiyo mwezi Machi, 2022.

Sehemu ya wananchi kutoka Wilaya ya Busega waliofika Mahakama ya Wilaya ya Bariadi kupata huduma wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga (hayupo katika picha) wakati alipotembelea Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu.


Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu, Mhe. Martha Mahumbuga (aliyesimama) akitoa taarifa ya utendaji kazi kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe Athuman Matuma wakati alipotembelea Mahakama hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Mhe Faiza Salim akiongea jambo na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athuman Matuma (hayupokatika picha) alipotembelea jengo la Mahakama ya Wilaya ya Itilima linaloendelea na hatua za ujenzi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe Athuman Matuma, (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Mhe. Faiza Salim (wa tatu kulia). Wengine ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga, Mhe Hussein Mushi, wa kwanza kulia, Hakimu Mkazi Mfawidhi Wilaya ya Bariadi Mhe. Caroline Kiliwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga Bi. Mavis Miti, Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu Bw. Gasto Kanyairita na Msaidizi wa Sheria wa Jaji Mhe. Zawadi Ndudumizi.







Hakuna maoni:

Chapisha Maoni