Ijumaa, 29 Aprili 2022

JAJI MFAWIDHI MAHAKAMA MOROGORO ATETA NA VIONGOZI WA DINI

 Na Evelina Odemba – Mahakama Morogoro

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe hivi karibuni alikutana na viongozi mbalimbali wa dini mkoani hapo kujadili mambo kadhaa, hususani suala la kuzingatia maadili katika jamii ili kupunguza ongezeko la mashauri yanayofunguliwa mahakamani.

Katika kikao hicho ambacho pia kilihudhuriwa na Mkuu wa Mkoa, Mhe, Martin Shigela, viongozi hao wameahidi kushirikiana na Mahakama kwa kuendelea kusisitiza waumini wao kuzingatia maadili na kufuata sheria, hatua itakayosaidia kuwafanya waishi kwa hofu ya Mungu.

Kikao hicho kimefanyika kukutanisha uongozi wa Mahakama, wadau na viongozi wa dini mkoani hapa kwa lengo la kutoa tathimini ya hali iliyopo katika Mahakama pamoja na kuwashirikisha viongozi wa dini ili kufikia makundi mengi zaidi katika kuwaelimisha wananchi juu ya sheria.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao, Mhe. Ngwembe alisema kuwa Mahakama Morogoro inaamini kuwa jamii ikipewa elimu ya kutosha juu ya masuala ya sheria itasaidia kupunguza makosa mbalimbali yanayochangiwa na ukosefu wa elimu ya kutosha kuhusu jambo hilo.

Alisema kuwa idadi kubwa ya waliopo magerezani ni waumini wa dini ya Kikristo au Kiislam na wa chache ndio wapagani, hivyo kama elimu ya maadili na hofu ya Mungu itatolewa katika nyumba za ibada itatoa mchango chanya katika kupunguza matukio yanayoendelea kushika kasi ndani ya Mkoa wa Morogoro.

Mhe. Ngwembe alisema takwimu mkoani Morogoro zinaonesha uwepo wa makosa ambayo yanajirudia rudia, ikiwemo ubakaji wa watoto wa kike wenye umri chini ya miaka 18. Amesema kwa mwaka 2021 mashauri 199 yameripotiwa, huku kwa mwaka 2022 kuanzia Januari hadi Machi kuna mashauri 59 yameripotiwa.

Kwa mujibu ya Jaji Mfawidhi huyo, ulawiti kwa mwaka 2021 kulikuwepo na mashauri 32 na mwaka 2022 kuanzia Januari hadi Machi kuna mashauri matano ambayo tayari yamelipotiwa.

Ametaja makosa mengine kama dawa za kulevya ambapo kwa mwaka 2021 kulikuwepo na mashauri 188 na mwaka 2022 kuanzia Januari mpaka March kuna mashauri 52 ambayo  tayari yameshalipotiwa. Kosa lingine ni kukamatwa na nyara za serikali ambazo kwa mwaka 2021 kulikuwepo na mashauri 53 na kwa mwaka 2022 kuanzia Januari mpaka Machi kuna mashauri 42.

Kuhusu mauaji, Mhe. Ngwembe amesema kuwa kwa mwaka 2021 kulikuwepo na mashauri 95 na kwa mwaka 2022 kuanzia Januari hadi Machi kuna mashauri 26 ambayo tayari yameripotiwa mahakamani.

 Alibainisha kuwa miongoni mwa kundi kubwa la mahabusu na wafungwa waliopo katika magereza ya Mkoa huo ni vijana wenye umri chini ya miaka 35, hali ambayo ni hatari kwa taifa, kwani kundi hilo ndio lenye nguvu ya kufanya shuguli za uzalishaji.’

Aidha, Mhe. Ngwembe alikemea tabia ya jamii ya kuwaficha wahalifu, huku akitolea mfano kuwa kilimo cha dawa za kulevya aina ya bangi kinafanyika hadharani na jamii inaona na kukaa kimya badala ya kutoa taarifa kwa vyombo husika.

Akichangia mazungumzo hayo, Mchungaji Sauli Kajula kutoka Kanisa la Moraviani alishauri elimu ya dini mashuleni iwe somo la lazima kama yalivyo masomo mengine na kuahidi kuwa wao kama viongozi wa dini watawalea vijana katika dhamira njema na matumaini yao ni kuhakikisha matukio ya ukosefu wa maadili yanapungua kama sio kumalizika kabisa.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro aliishukuru Mahakama kwa kuweka bayana masuala mbalimbali yanayojitokea katika jamii na kuahidi kuwa yote yaliyosemwa wameyapokea kama serikali na ameahidi kutoa ushirikiano.

Mhe. Shigela aliwaomba viongozi wa dini na jamii kwa ujumla kukaa katika misingi inayokubalika kiimani ili kupunguza makosa yanayojitokeza ambayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na jamii kukosa hofu ya Mungu.

Mahakama ya Tanzania Mkoa wa Morogoro imekuwa na utaratibu wa kuwafikia wananchi ili kuwapa elimu ya sheria kuhakikisha wanapunguza mashauri yanayojirudia mara kwa mara.

Awali, elimu hiyo ilikuwa ikitolewa upitia vyombo vya habari mkoani humo kuanzia Novemba 2021 na baadae ilianza kutolewa kwa wananchi wanaofika katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki na takwimu zinaonyesha tangu huduma hiyo ianze kutolewa mwezi machi 2022, wananchi takribani 2,723 wamenufaika na elimu hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa dini. Waliokaa kutoka kulia ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro,  Bi Lucy John, Jaji Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Martin Shigela.
Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wanasheria wa serikali na wa kujitegemea.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (mwenye tai nyekundue) akiongoza msafara baada ya zoezi la upandaji miti.

Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Morogoro wakifuatilia mjadala wakati wa kikao kilichoandaliwa na Mahakama na kuwashirikisha wadau na viongozi wa dini mkoani humo.

Wadau (picha ya juu na chini) wakifatilia mjadala.

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe Martin Shigela akipanda mti wa matunda katika eneo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mkoani Morogoro baada ya kikao.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni