Jumatatu, 16 Mei 2022

JAJI MKUU AANZA ZIARA YA MAHAKAMA KANDA YA TANGA

 Na. Faustine Kapama, Mahakama, Tanga.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 16 Mei, 2022 ameanza ziara ya kikazi ya siku nne katika Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Tanga, kukagua shughuli mbalimbali za kimahakama, ujenzi wa miundombinu pamoja na kuongea na watumishi na wadau mbalimbali.

Kakika siku yake ya kwanza, Mhe. Jaji Mkuu amemtembelea Mkuu wa Mkoa, Mhe Adam Malima na kufanya naye mazungumzo mafupi kabla ya kuelekea Pangani kukutana na Mkuu wa Wilaya hiyo, Mhe. Ghaibu Lingo. Baada ya hapo, Jaji Mkuu aliekelekea katika Mahakama ya Wilaya ya Pangani ambapo alipokea taarifa ya utendaji kutoka kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Joel Mguto.

Akiwa katika Mahakama hiyo, Mhe. Prof. Juma alipata fursa ya kuongea na watumishi kabla ya kuelekea Wilaya ya Muheza ambapo alikutana na Mkuu wa Wilaya hiyo, Mhe. Halima Bulembo na baadaye kuongea na watumishi katika Mahakama ya Mwanzo na Mahakama ya Wilaya ya Muheza.

Kabla ya kuongea na watumishi wa Mahakama hizo, Jaji Mkuu alipokea taarifa ya utendaji kutoka kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya hiyo, Mhe. Lilian Rutehangwa ambaye ameainisha mafanikio waliyofikia ikiwemo kusikiliza mashauri kwa wakati, kuendesha shughuli za kimahakama kupitia fedha za matumizi ya ofisi, kutoa nakala za hukumu kwa wakati kwa wadaawa na upatikanaji wa vitendea kazi, mfano komputa.

Ameelezea mikakati waliyonayo inayojumuisha kutokuwa na mludikano wa mashauri, kuboresha majengo kwa kufanya ukarabati mdogo kadri wanavyopokea fedha za matumizi, kulipa stahiki mbalimbali za watumishi na upatikanaji wa vitendea kazi kwa wakati na vya kutosha kwa Mahakama zote.

Akiongea na viongozi wa Serikali kwa nyakati tofauti, Mhe. Prof. Juma alisisitiza umuhimu wa wadau katika mnyororo wa utoaji haki kusoma hukumu mbalimbali zinazopatikana bure katika mtandao wa Mahakama ambazo zimesheheni masuala muhimu yanayosaidia kurahisisha utoaji wa haki kwa wananchi, husuani katika mashauri ya mirathi na dawa za kulevya.

Amewaeleza viongozi hao kuwa Kikao cha Mahakama ya Rufani kilichoketi Tanga hivi karibuni kimebaini mashauri yanayohusu dawa za kulevya ndiyo yanayoongoza katika Kanda hiyo ya Mahakama, hivyo akashauri vyombo vinavyohusika na upelelezi kufuata sheria na taratibu katika kushughulikia kesi hizo ili kuwezesha haki kutendeka zinapofikishwa mahakamani.

“Mkoa huu unachangamoto ya kesi za dawa za kulevya na changamoto kubwa tunazoziona ni namna gani ushahidi unavyokusanywa. Wakati mwingine kuna makosa ambayo yanayojirudiarudia katika ukusanyaji wa ushahidi, ambayo yanasababisha wakati mwingine wale wanaohusika kuachiwa huru. Hii wakati mwingine inafanya wananchi wasielewe. Hivyo, viongozi wasome zile hukumu ili waone maeneo ya changamoto hizo ambazo zimeonyeshwa,” alisema.

Akiwa katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mhe. Prof. Juma alipata taarifa za msiba wa mmoja wa madiwani katika halimashauri ya Manispaa ya Tanga, ambaye ni ndugu wa karibu na Jaji Mkuu mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman. Kutokana na taarifa hiyo, Jaji Mkuu aliamua kukatisha ziara yake kwa muda na kwenda kutoa pole kwa familia na wanaombolezaji waliokuwa kwenye msiba huo.

Katika ziara hiyo, Jaji Mkuu anatarajia pia kutembelea maeneo mbalimbali, ikiwemo Wilaya za Kilindi, Handeni, Lushoto na Korogwe kabla ya kuhitimisha ziara yake Tanga mjini.  Mhe. Prof. Juma ameongozana na viongozi mbalimbali kutoka Makao Makuu, wakiwemo Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Kevin Mhina, Naibu Msajili kutoka Kurugenzi wa Ukaguzi wa Huduma za Kimahakama, Malalamiko na Maadili, Mhe. Aidan Mwilapa na Mkurugenzi Msaidizi wa TEHEMA wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Machumu Essaba.

Wengine ni Katibu wa Jaji Mkuu Adrean Kilimi, Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjila Kuu, Bi Maria Itala, Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimali Watu na Utawala, Bw. Anatory Kagaruki, mwakilishi wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania, Mhe. Nemes Mombury, Mkuu wa Kitengo cha Uhandisi, Bw. Yohana Mashausi, Afisa Utumishi, Bw. Jeofrey Mnemba, Mpima Ramani Abdallah Nalicho, Mhandisi Peter Mrosso na Msaidizi wa Sheria wa Msajili wa Mahakama ya Rufaa, Mhe. Hassan Chuka.

Kwa upande wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga yupo Jaji Mfawidhi, Mhe. Latifa Mansoor, Naibu Msajili Beda Nyaki, Mtendaji Humphrey Paya, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Tanga, Mhe. Sofia Masati na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Tanga, Mhe. Ruth Mkusi.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Adam Malima akimkaribisha Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 16 Mei, 2022 alipoanza ziara ya kikazi ya siku nne katika Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Tanga.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiteta jambo na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Adam Malima.
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Adam Malima akisisitiza jambo.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimkabidhi Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Adam Malima taarifa ya utendaji ya Mahakama. 
Sehemu ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Tanga ikiwa katika ofisi ya Mkuu wa  Mkoa huo wakati wa ziara ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma. 
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma akiwasili katika ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Pangani.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma akisaini kitabu cha wageni.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma (katikati) akiwa katika msiba wa ndugu wa karibu na Jaji Mkuu mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma akitoa salamu katika msiba huo.
Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Mhe. Ghaibu Lingo akisistiza jambo mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma (hayupo kwenye picha).
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu wa Tanzania, Kanda ya Tanga, Mhe. Latifa Mansoor akifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma. Kushoto kwake ni Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Kevin Mhina.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma akiwasili katika Mahakama ya Wilaya ya Pangani.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma akisaini kitabu cha wageni.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu wa Tanzania, Kanda ya Tanga, Mhe. Latifa Mansoor (kulia) akiwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Pangani, Mhe. Joel Mguto.

Naibu Msajili wa  Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga, Mhe. Beda Nyaki (kulia) akiwa na Mtendaji Humphrey Paya.

Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimali Watu na Utawala, Bw. Anatory Kagaruki (katikati) akitoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizoibuliwa na watumishi. Kulia ni Naibu Msajili kutoka Kurugenzi wa Ukaguzi wa Huduma za Kimahakama, Malalamiko na Maadili, Mhe. Aidan Mwilapa na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjila Kuu, Bi Maria Itala.
Mkuu wa Wilaya ya Muheza, Mhe. Halima Bulembo akitoa neno mbele ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo katika picha).


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma (picha ya juu na chini) akiwasili katika Mahakama ya Wilaya ya Muheza.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis  Juma (katikati) na viongozi wengine wa Mahakama wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Wilaya ya Pangani (juu) na Wilaya ya Muheza (chini).

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni