Jumatatu, 16 Mei 2022

JAJI KIONGOZI : TOENI HUDUMA YA KARNE YA 21 KUKIDHI USHINDANI

 

Na Magreth Kinabo- Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani amewataka watumishi wote wa mahakama nchini, kuendelea kuwatumikia Watanzania kwa juhudi na maarifa yanayoendana na mazingira ya karne ya 21.

Hayo yamesemwa na Jaji Kiongozi wakati akizungumza kwenye mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu Masijala Kuu, ambao ni wa mara ya kwanza kufanyika,  uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita mkoani Morogoro, ambapo alisema karne hiyo ni ya ushindani katika utoaji wa huduma bora.

‘‘Ni lazima wafanyakazi tujibadilishe sio tu kifikra bali tufanye kazi katika namna ambayo itawezesha wale wale tunaowahudumia kuridhika. Ni kwa kufanya hivyo tu, tutakuwa na haki ya kuendelea kuwahudumia. Sasa kwa wafanyakazi wa mahakama, sera na mwelekeo wetu ni kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji haki,’’ alisema Jaji Kiongozi.

Aidha Jaji Kiongozi alisema mafunzo mbalimbali yametolewa na yataendelea kutolewa katika eneo hilo, hivyo kila mtumishi bila kujali kada yake, atambue, kuwa anao wajibu wa kuhakikisha azma hiyo inatimia.

Alifafanua kwamba kila mtumishi anapaswa kujua kuwa lengo letu ni kuhakikisha kuwa watu wote wanaokuja kubisha hodi katika milango ya mahakama, wanapata haki kwa wakati na yoyote atakayekuwa kikwazo katika kufikia lengo hilo, hafai kuwa mtumishi wa karne ya 21.

Jaji Kiongozi huyo aliongeza kazi ya msingi ya Mahakama ni kutoa haki kwa kupokea na kusikiliza mashauri mbalimbali.Mahakama inafanyakazi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kutimiza jukumu hilo, Mahakama ina Mpango Mkakati ambao ni budi kila mmoja wetu kuujua na mradi wa maboresho unaoendelea.

‘‘Kwa kuwa watumishi ndio watekelezaji wa yote yanayoamuliwa na uongozi ikiwemo mradi wa maboresho, ni rai yangu kwamba mabaraza kama haya sio tu yajadili maslahi ya wafanyakazi, lakini yatumike pia kama sehemu ya kukumbushana mipango mbalimbali na mambo ya msingi kazini ili mfanyakazi awe sehemu ya mafanikio ya taasisi,’’ alisitiza.

Kwa upande wake Katibu wa TUGHE wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Michael Masubo akiwakilisha hoja za wafanyakazi wa mahakama hiyo kwenye baraza hilo, alisema semina za watumishi zitolewe mara kwa mara ili kuwajengea uwezo katika kazi zao za kila siku, mishahara kuwa katika ngazi moja,utoaji wa elimu kuhusu maboresho ya Mahakama yanayoendelea  kwa watumishi ili waweze kuijua Mahakama yao, na suala la upandishaji vyeo.

Mahakama ya Tanzania umetekeleza Mpango Mkakati wa Miaka Mitano 2015/16 – 2019/20 na Maboresho ya Mahakama wa 2016/17-2021/22. Hivi sasa imeanza utekelezaji wa awamu ya pili ya Mpango Mkakati wa 2020/21- 2022/25 na Mradi wa Maboresho ya Mahakama wa Awamu ya pili wa 2022/23- 2024/25.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe.Mustapher Siyani,  akitoa hotuba yake ya ufunguzi wa  mkutano huo.

         Baadhi ya watumishi wa mahakama hiyo wakiwa katika mkutano huo.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe.Mustapher Siyani, (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya majaji na watumishi wa mahakama hiyo mara baada ya kufungua mkutano huo.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni