Jumapili, 15 Mei 2022

MAHAKAMA SPORTS YAACHA GUMZO MAWAKILI BONANZA

·Yanyakua medali baada ya kushika nafasi ya pili

Na Faustine Kapama-Mahakama

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) jana terehe 14 Mei, 2022 iliacha gumzo kwenye Bonanza lililoandaliwa na Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) mara baada ya kuibuka washindi wa pili kwenye mchezo wa mpira wa miguu (Soka).

Bonanza hilo lilioshirikisha timu mbalimbali ikiwemo ya Mahakama Sports, Chuo kikuu cha Dar es salaam, TLS na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) lilifanyika katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Dar es salaam (Mlimani). Katika mchezo huo wa soka, timu shiriki zilicheza kwa mtoano ambapo timu iliyoshinda katika hatua hiyo itiingia moja kwa moja fainali.

Katika hatua ya mtoano, TLS ilipangwa kucheza na timu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania, huku Mahakama Sports ikamenyana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Ilikuwa timu ya TLS iliyofanikiwa kutinga fainali mara baada ya kuwabanjua TRA kwa goli moja kwa sifuri.

Kwenye mchezo uliozikutanisha  Mahakama Sports na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, timu ya Mahakama Sports walishinda kwa goli mbili kwa moja, hivyo kufanikiwa kutinga katika hatua ya fainali. Magoli ya Mahakama Sports yalifungwa na mshambuliaji hatari Robert Tende.

Kufuatia matokeo hayo, Mahakama Sports ilikutana na TLS katika hatua ya fainali ambapo ndani ya dakika 90 timu zote zilitoka kwa kufungana goli moja kwa moja na goli la Mahakama Sports likifungwa kwa mara nyingine na Robert Tende aliyeonekana kuwa mwiba kwa timu pinzani.

Baada ya kutoka sare ndani ya dakika hizo 90, Mwamuzi aliamuru kupigwa mikwaju ya matuta (penalty), ambapo  Mahakama Sports walipata magoli mawili huku TLS wakabahatisha magoli matatu, hivyo TLS kutangazwa kuwa mabingwa wa Bonanza hilo.

Wachezaji walioshiriki kwenye mchezo huo walikuwa Spear Mbwembwe, Florence Gisbert, Mohamed Migomba, Jamal Mkumba, Said Albea, Ghulam Katwila, Omari Mdakama, Rajabu Ally, maarufu kama Roja Kumbakumba, Fidelis Choka, Robert Tende na Antony Mfaume. Wachezaji wa akiba walikuwa Wilson Dede, Magesa Mgeta, Ferdinand Philip, Mohamed Burhan, Goodluck Mushi na Victor Zacharia Mchopa.

Akiongea baada ya mechi hiyo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amewapongeza wachezaji wote kwa kujituma na kufanya vizuri kwenye Bonanza hilo licha ya kupata mwaliko kwa muda mchache na kufanya mazoezi kwa muda mfupi.

“Niwapongeze vijana wangu kwa kufanya vizuri kwenye Bonanza hili ingawa tulipata mwaliko kwa muda mfupi. Hii ni salamu tosha kwa timu pinzani kwamba Mahakama Sports tupo vizuri. Tunatanguliza pia salamu zetu kwa wapinzani wetu kwenye mashindano yajayo ya SHIMIWI. Safari hii tunaenda kuwashangaza, hawataamini kitakachowakuta,” alisema.

Mbali na mwenyekiti huyo, viongozi wengine walioambatana na timu ni Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Mhasibu Rajabu Dihwa, Meneja wa Timu Anthony Mfauke na Mtunza Vifaa Thedy Morgan.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) wakijifua kabla ya kuanza kwa Bonanza lililoandaliwa na  Chama cha Mawakili Tanganyika.
Timu Meneja wa Mahakama Sports Antony Mfaume (kushoto) akimkabidhi zawadi mchezaji Victor Zacharia baada ya kuonyesha mchezo mzuri ikiwemo kutoa pasi murua zilizosababisha kupatikana kwa magoli mawili.
Mshambuliaji matata Robert Tende (kushoto) akipokea zawadi kutoka kwa Timu Meneja Antony Mfaume baada ya kufunga mabao mawili. 
Baadhi ya wachezaji wa Mahakama Sports  (picha ya juu na chini) wakionyeshe medali zao baada ya kushika nafasi ya pili.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni