Jumanne, 17 Mei 2022

JAJI WILBARD MASHAURI AAGWA KITAALUMA MWANZA

 Na Mwandishi wetu

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani hivi karibuni aliongoza viongozi mbalimbali wa Mahakama kumuaga kitaaluma Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Wilbard Mashauri.

Akizungumza katika sherehe hizo zilizofanyika viwanja vya Mahakama Kuu Mwanza, Mhe. Siyani alimwelezea Jaji mstaafu Mashauri kuwa mtu makini na madhubuti katika masuala nyeti na alisimama kama mtu mwenye mtazamo huru, alimsikiliza kila mtu na hakuwa na uvumilivu na watu wasiokuwa na uadilifu.

Jaji Kiongozi alitoa mfano wa shauri la rufaa namba 1/2021- kati ya Eliada Phinias Machumu dhidi ya Christian Mau, ambalo lilikuwa limesheheni udanganyifu uliokuwa umetengenezwa kwa umahili wa hali ya juu, ambapo mume wa mrufani aliuza nyumba na akampa talaka mrufani.

“Mara baada ya kuuza nyumba alifungua shauri katika Baraza la Ardhi la Wilaya akidai nyumba hiyo kwa kutumia jina la mtalaka wake (mrufani) ambapo alishindwa na kuleta rufaa Mahakama Kuu ndipo mrufani(mtalaka) alipata taarifa na kuiandikia barua Mahakama na kueleza kuwa hakuwahi kufungua shauri lolote bali ni udanganyifu umefanyika kwa kughushiwa saini yake na mtalaka wake akiwa na nia ya kupora nyumba ambayo alikuwa ameiuza,” alieleza Mhe. Siyani.

Pia Jaji Kiongozi alieleza kuwa Mhe. Mashauri alikuwa makini na ujanja wa mawakili ambao walikuwa na tabia ya kuzuia upatikani wa haki kwa wakati kwani hakuwapa nafasi na hali hiyo iliweza kuthibitishwa pia katika shauri la Omega Fish Ltd dhidi ya Zakayo Kabali, Maombi namba 91/2018, hivyo alitamani mashauri yote yaendeshwe kwa mujibu wa sheria.

Kwa upande wake, Jaji mstaafu Mashauri alisema kuwa katika utendaji kazi wake hawezi kusau shauri alilopangiwa kuliendesha baada ya kuhamishiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu lililokuwa linawahusu viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kwani ni shauri lililokuwa na changamoto nyingi, ikiwemo ukosoaji na tuhuma nyingi kuwa hakuwa na uwezo wa kusikiliza shauri hilo.

Alieleza kuwa wakosoaji wake walikuwa wakidai kuwa alikuwa akifanya kazi kwa shinikizo la watu ambao hawakuweza kutajwa na mara nyingi alitishiwa kuuawa baada ya kukataa kujitoa katika shauri hilo, msukumo ambao haukutoka kwa watu wa mbali tu bali hata baadhi ya watu wake wa karibu walimuomba ajitoe.

Baadhi ya Majaji wengine wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria sherehe hizo ni Majaji wote wa Mahakama Kuu Mwanza, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania. Mhe. Sharmillah  Sarwatt.

Sherehe hizo za kumuga zilianza kwa Wakili wa Serikali Mwandamizi, Bw. Mamti kuiomba Mahakama iweze toa amri ya kuendelea kwa shauri hilo,ombi ambalo liliungwa mkono  na Wakili wa Kujitegemea, Bw. Steven Kitale, ambaye ni Mwenyeketi wa Chama cha  Mawakili  Tanganyika, Kanda ya Mwanza.

Jaji Mashauri aliteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania mwaka 2019 nafasi aliyoshikilia hadi kustaafu kwake. Kwa kipindi chote akiwa Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Mashauri ametoa uamuzi mbalimbali katika mashauri ya jinai, madai na migogoro ya kazi na ardhi.

Jaji Mtaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Wilbard Mashauri.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mhe. Mashauri.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria sherehe za kumuaga Jaji Mashauri (wa kwanza kushoto kwa Jaji Kiongozi).


Jaji Mashauri na mkewe akikata keki baada ya sherehe hiyo. Kushoto ni Jaji Kiongozi Mhe. Mustapher Siyani akisherehesha tukio hilo.
Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na viongozi wengine wa Mahakama waliohudhuria sherehe za kumuaga Jaji Mashauri.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni