Na Mary Gwera, Mahakama
Mkurugenzi wa Kanda ya Afrika anayeshughulikia Ukuzaji
wa Uchumi na Taasisi kutoka Benki ya Dunia (WB), Bw. Asad Alam amepongeza hatua
ya uboreshaji wa huduma za utoaji haki nchini huku akiahidi kuwa Benki hiyo
itaendelea kuunga mkono jitihada hizo kwa kuiwezesha Mahakama kuendelea kuhudumia
wananchi.
Akizungumza mara baada ya kuhitimisha ziara yake fupi
aliyofanya Mahakama leo tarehe 28 Septemba, 2022, Bw. Alam alikiri kuridhishwa na
hatua ambayo Mahakama imepiga hususani katika uboreshaji wa Miundombinu ya
majengo, uanzishwaji wa huduma za Mahakama inayotembea na matumizi ya Mkutano
mtandao ‘Video Conference’ katika uendeshaji wa mashauri.
“Hii ni mara yangu ya kwanza kutembelea Mahakama ya
Tanzania, lengo la kuja kwangu ni kujionea jinsi mnavyotekeleza Mradi wa
Uboreshaji wa Huduma za Mahakama, nina furaha kusema kuwa kwa taarifa
iliyotolewa na kutembelea jengo la Mahakama hii ya Temeke na kujionea
uendeshaji wa Mashauri kwa njia ya mkutano mtandao ninaweza kusema kuwa mmepiga
hatua na mnafanya vizuri, hivyo, Benki ya Dunia itaendelea kuwezesha uboreshaji
zaidi wa huduma,” amesema.
Mbali na pongezi, Mkurugenzi huyo alisema kuwa, kuna
haja ya kusogeza zaidi huduma za utoaji kwa wananchi waliopo katika maeneo ya
mbali zaidi huku akisisitiza kuhusu kutosahau kuzingatia usawa wa jinsia huku
akisisitiza kuwa ni muhimu pia kuwafikia wanawake.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania,
Prof. Elisante Ole Gabriel amemuhakikishia Mkurugenzi huyo wa Benki ya Dunia
kuwa, huduma zinazotolewa na Mahakama zinamlenga mwananchi na katika awamu ya
pili ya Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama unaofadhiliwa na Benki hiyo,
Mahakama imepanga kujenga Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki tisa (9) ili huduma ya
Mahakama iweze kuwafikia Watanzania wengi zaidi.
“Napenda kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania inayoongozwa na Rais wa awamu ya Sita, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa
kuiamini Mahakama na kuiwezesha kupata mkopo kutoka Benki ya Dunia, na katika
awamu hii ya pili tunatarajia kujenga Vituo vya Utoaji Haki tisa (9) na
tumepanga kujibana zaidi ikibidi tupate hata Vituo hivyo 12 ili tuweze kuwafikia
wananchi wengi zaidi,” ameeleza Prof. Ole Gabriel.
Mtendaji Mkuu ameishukuru pia Benki ya Dunia kwa
kuongeza kiwango cha fedha za Mradi ambazo ni Dola za Kimarekani Milioni 90 sawa
na Bilioni 210 za kitanzania zitakazosaidia
kuboresha zaidi huduma za kimahakama ikiwemo kuongeza idadi ya Mahakama zinazotembea
‘Mobile Courts’, majengo ya Mahakama, kuongeza matumizi ya mkutano mtandao ‘Video
Conference’ katika uendeshaji wa Mashauri na kadhalika.
Akiwasilisha Mada kwa Mkurugenzi huyo na Maafisa
alioambatana nao, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Maboresho, Mahakama ya Tanzania,
Bw. Daniel Msangi amesema kuwa, tangu kuanza kwa utekelezaji wa Mradi wa
Uboreshaji wa Huduma za Mahakama umesaidia kupatikana kwa mafanikio lukuki
ikiwemo kusogeza huduma karibu na wananchi huku akitoa mfano kuwa, upatikanaji
wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro umewapunguzia wananchi aza ya kusafiri
umbali mrefu kuja Dar es Salaam kupata huduma ya ngazi hiyo ya Mahakama.
Akizungumzia Kituo maalum cha Masuala ya Familia
Temeke, Bw. Msangi ameeleza kuwa tangu kuanzishwa kwake Mahakama hiyo maalum iliyoanza
kufanya kazi tarehe 25 Oktoba,
2022 imehudumia jumla ya wananchi 124,476 wanawake wakiwa 66,222 na
wanaume 58,254.
Ameongeza
kuwa, faida nyingine ni utoaji wa huduma kupitia Mahakama zinazotembea ambazo
kwa sasa zipo mbili (2) zinazotoa huduma Dar es Salaam na Mwanza, amebainisha
kuwa, kuanzia Januari hadi Agosti mwaka huu Mahakama hizo zimehudumia wananchi
wapatao 12, 810, kati ya hao Wanawake ni 7,236 na Wanaume ni 5,574.
Waambata wa Mkuu huo, nao kwa pamoja wamepongeza Uongozi wa Mahakama kwa kazi nzuri ya utekelezaji wa Mradi wa uboreshaji wa Huduma za Mahakama. Katika ziara yake fupi Mkurugenzi huyo alipata fursa ya kufanya mazungumzo na Prof. Elisante Ole Gabriel, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, kutembelea Kituo cha Taarifa cha Mahakama kilichopo katika eneo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam-Kisutu ambapo walishuhudia shauri likiendeshwa kwa Mkutano Mtandao ‘Video Conference’.
Alihitimisha ziara yake fupi kwa kutembelea na kukagua
Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia-Temeke, kukagua na kupata taarifa ya utendaji
kazi wa Mahakama Inayotembea ‘Mobile Court’ pamoja na taarifa ya Mradi wa Uboreshaji
wa Huduma za Mahakama unaofadhiliwa na Benki ya Dunia.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni