Jumatano, 28 Septemba 2022

MAHAKAMA SPORTS GARI LIMEWAKA

Na Faustine Kapama-Mahakama

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) jana tarehe 27 Septemba, 2022 imeanza mazoezi ya pamoja kwa kujumuisha wachezaji kutoka Mikoa mbalimbali nchini kujiandaa na mashindano yajao ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayotarajia kufanyika jijini Tanga kuanzia tarehe 1 Octoba, 2022.

Akizungumza katika Viwanja vya Shule ya Sheria kwa Vitendo (Law School) jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Mahakama Sports Robert Tende amesema wanamichezo wote walioitwa kutoka mikoani wameanza mazoezi ili kuwawezesha walimu kuchagua majina ya wale watakaoshiriki kwenye michezo mbalimbali katika mashindandano hayo.

Tende amekiri kuwa walimu watakuwa na kazi kubwa ya kuchagua wachezaji watakaoshiriki kwenye mashindano hayo kwa vile vijana wote mwaka huu wapo vizuri, wana ari kubwa na wote wanajituma katika mazoezi.

“Safari hii tunawachezaji wazuri sana kwenye kila mchezo, wote wanajituma na wanafanya vizuri kwenye mazoezi. Walimu wana kazi kubwa kupata wachezaji watakaopeperusha bendera ya Mahakama kwenye mashindano haya mwaka huu,” alisema.

Katibu Mkuu huyo amesisitiza Mahakama Sports imedhamilia kuchukua vikombe vyote vya mshindi wa kwanza kwenye michezo yote watakayoshiriki, hivyo amewahimiza wanamichezo wote kuzingatia programu zinazotolewa na walimu ili waweze kujiandaa vyema kushiriki kikamilifu kwenye mashindano hayo.

Amewakumbusha wanamichezo wote kuwa kwa mujibu wa kanuni za mashindano kila mshiriki anatakiwa kuwepo kwa kipindi chote kilichopangwa, hivyo akawatahadhalisha kujipanga vyema ili wasitolewe kwenye hatua za mwanzo na kuwafanya kuwa wasindikizaji wawashiriki wengine.

“Kanuni za mashindano SHIMIWI zinamtaka kila mshiriki kubaki kwenye kituo tangu siku ya kwanza hadi ya mwisho, hata kama umetolewa kwenye hatua za awali. Kwa hiyo, nawaomba wanamichezo wenzangu kujiandaa kikamilifu. Mwaka huu hatutaki kupoteza kitu,” alisema.

Michezo ambayo Mahakama Sports inatarajia kushiriki ni Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha Wanaume na Wanawake pamoja na Baiskeli.

Timu ya Mahakama ya Tanzania-Mahakama Sports-(picha ya juu na mbili chini) ikiwa katika mazoezi kujiandaa na mashindano yajao ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI). 



Mwalimu Spear Mbwembe (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wachezaji wa mpira wa miguu.
Sehemu nyingine ya wachezaji wa mpira wa miguu ikiwa katika picha ya pamoja baada ya mazoezi chini ya Mwalimu Spear Mbwembe. 
Mwalimu Spear Mbwembe (kushoto) akitoa maelekezo kwa vijana wake.
Sehemu ya wanamichezo wa Mahakama Sports ikimsikiliza Mwalimu Spear Mbwembe (hayupo katika picha).







Hakuna maoni:

Chapisha Maoni