Jumatano, 28 Septemba 2022

WANACHAMA CHAMA CHA MAJAJI NA MAHAKIMU TANZANIA KUTOKA SHINYANGA, SIMIYU WATINGA BUNGENI

Na Emmanuel Oguda – Shinyanga

Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (JMAT) kutoka Mikoa ya Shinyanga na Simiyu hivi karibuni walitembelea Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhudhuria kipindi cha maswali na majibu na kujifunza shughuli mbalimbali za kibunge.

Katika ziara hiyo, wanachama hao walifarijika kuona namna Bunge linavyoendeshwa. Afisa Uhusiano wa Bunge, Bw. Deogratius Simba aliwapitisha katika maeneo mbalimbali ikiwemo ukumbi wa zamani wa Bunge unaojulikana kwa jina la Ukumbi wa Pius Msekwa pamoja na maeneo mengine na kutoa fursa kwa wanachama hao kuuliza maswali kuhusiana na shughuli za uendeshaji wa Bunge.

Wakati huo huo, wanachama hao walipata fursa ya kutembelea Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania linaloendelea kujengwa na kujionea ukubwa wake ambapo ujenzi wake unatarajiwa kukamilika Desemba mwaka huu.

Akitoa maelezo ya mradi huo, Mhandisi Qeen Mduma aliwaeleza wanachama hao kuwa jengo hilo linajumuisha Mahakama ya Juu (Supreme Court), Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu (Masijala Kuu) pamoja na Ofisi za Utawala (Head Quarters). Kadhalika, jengo hilo litakuwa na maeneo mbalimbali ikiwemo viwanja vya mpira. Aliongeza kuwa ukubwa wa eneo ni ekari 45 na jengo hilo ni la sita (6) kwa ukubwa duniani.

Nae Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe Dkt Adam Mambi aliwapongeza wanachama hao kwa ziara yao ya kutembelea Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kupata fursa ya kutembelea mradi wa ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

“JMAT Dodoma tunalo la kujifunza kutoka kwenu, nina imani pia wanachama wa JMAT Kanda ya Dodoma wataiga mfano huu kutoka kwa JMAT Shinyanga,”  alisema.

Wanachama wa JMAT Shinyanga na Simiyu (juu na picha mbili chini) wakifuatilia kipindi cha maswali na majibu Bungeni Dodoma.


Wanachama wa JMAT wakiwa katika ukumbi wa zamani wa Bunge  unaoitwa Ukumbi wa Pius Msekwa (juu na chini) wakimsikiliza Afisa Uhusiano (hayupo katika picha) wakati walipotembelea Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Afisa Uhusiano wa Bunge Bw. Deogratius Simba (mwenye beji ya bluu) akiwatembeza wanachama wa JMAT katika maeneo mbalimbali ya Bunge.
Muonekano wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania linaloendelea kujengwa Jijini Dodoma.
Mhandisi Qeen Mduma (wa kwanza kushoto) akitoa maelezo ya mradi wa ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania wakati wanachama wa JMAT walipotembelea mradi huo.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe Dkt. Adam Mambi (wa pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wanachama wa JMAT waliotembelea mradi wa ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama.

 Picha ya pamoja ya wanachama wa JMAT Shinyanga, Simiyu na Dodoma walipotembelea jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni