Jumatano, 28 Septemba 2022

JAJI MFAWIDHI DODOMA ASISITIZA UELEWA KUHUSU UHALIFU WA KIMATAIFA

Na Arapha Rusheke-Mahakama, Dodoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu amesisitiza umuhimu wa kuongeza uelewa kwa Mahakimu kuhusu utakatishaji wa fedha haramu, ufadhili wa magaidi, biashara haramu ya wanyamapori kutokana na athari zake katika uchumi wa Taifa ili waweze kutoa uamuzi sahihi kukomesha uhalifu huo wa kimataifa.

Mhe. Mdemu alitoa wito huo hivi karibuni alipokuwa anafungua mafunzo kwa Mahakimu Wakazi wa Tanzania Bara kuhusu makosa hayo. Jaji Mdemu alibainisha kuwa ongezeko la kasi la utandawazi na mwingiliano wa shughuli za kifedha umefanya utakatishaji fedha kuwa miongoni mwa matatizo ya kimataifa.

"Kwa hiyo, hali hii inachagiza hitaji muhimu la kuwepo mikakati na juhudi za pamoja kupambana na makosa haya ya utakatishaji fedha. Nchi lazima zishiriki katika vita hivi,” alisisitiza.

Amesema ni kwa kutambua ukweli huo kwamba mashirika kadhaa ya kimataifa yameandaa mapendekezo na mbinu bora kusaidia nchi zote kuimarisha juhudi zao za kupambana na makosa ya utakatishaji fedha.

"Nyinyi mkiwa miongoni mwa maofisa wa Mahakama, ufahamu wa maarifa na ujuzi kuhusu makossa haya, kwa hakika, utaboresha uamuzi wenu kwa kutumia maarifa na ujuzi huo," Jaji Mdemu aliwaambia washiriki wa mafunzo hayo.

Alisema mafunzo hayo yamefanyika kutokana na changamoto na athari mbaya zinazotokana na utakatishaji fedha, biashara haramu ya wanyamapori na ufadhili wa ugaidi.

"Mnafahamu kwamba, athari za utakatishaji fedha kama uhalifu katika uchumi wa taifa haziwezi kupuuzwa. Kwa hiyo, haja ya kuongeza kiwango cha uelewa cha kutosha miongoni mwa Mahakimu inapaswa kutiliwa mkazo,” alisema.

Jaji Mdemu aliendelea kubainisha kuwa ni kwa njia ya utakatishaji fedha ambapo shughuli haramu za fedha zinahalalishwa na kuchangia kwa kiasi kikubwa kufanya uhalifu ulipe. Alisema utakatishaji wa fedha pia unachangia kudhoofisha uadilifu wa mfumo wa fedha, taratibu za soko na uchumi wa taifa zima.

"Utakatishaji fedha, biashara haramu ya wanyamapori na kufadhili ugaidi ni matokeo mabaya ya uchumi, haswa kwa nchi zinazoendelea kama uchumi wetu. Athari hizi kwa kawaida ni pamoja na ongezeko lisiloelezeka la mahitaji ya bidhaa na huduma ambazo zinaweza kutumika kuhalalisha kiasi kikubwa cha fedha zinazotokana na uhalifu,” alisema.

Ni matumaini yake kuwa mafunzo hayo yatawasaidia washiriki kuboresha ujuzi wao juu ya utakatishaji fedha, ufadhili wa ugaidi na mbinu haramu za biashara ya wanyamapori, mbinu zinazoweza kubuniwa na kutumiwa kushughulikia vitendo hivyo na namna bora ya kushughulikia mashauri yanayohusu makosa hayo watatu.

Washiriki wa mafunzo hayo ya siku tano yamewakutanisha Mahakimu Wakazi kutoka Mahakama Kuu Kanda za Dar es Salaam, Bukoba, Dodoma, Iringa, Mbeya, Moshi, Musoma, Mtwara, Mwanza, Songea, Morogoro na Sumbawanga.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo (picha ya juu na chini).


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu akifungua mafunzo hayo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni