Jumatatu, 26 Septemba 2022

MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA ATOA USHAURI MUHIMU KWA VIONGOZI MAHAKAMANI

Na Faustine Kapama-Mahakama

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amewasihi viongozi wa Mahakama kutambua nafasi walizonazo kwa jamii na ndani ya Mhimili huo wa utoaji haki na kufanya uamuzi sahihi kwa usahihi ili kumsaidia Mtanzania kupata haki anayostahili kwa wakati.

Prof. Ole Gabriel ametoa wito huo leo tarehe 26 Septemba, 2022 alipokuwa anafungua mafunzo ya siku tatu kuhusu uongozi bora yanayotolewa kwa wajumbe wa menejimenti ya Mahakama ya Tanzania inayojumuisha wakuu wa idara na vitengo mbalimbali yanayofanyika katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki cha Masuala ya Familia Temeke jijini Dar es Salaam.

“Elewa hautakumbukwa kwa sababu ya nafasi yako, utakumbukwa kwa mchango wako katika kuboresha uamuzi unaofanywa. Hakikisha uamuzi unaofanya unamsaidia Mtanzania wa ngazi yoyote ambaye anatafuta haki yake. Onyesha thamani yako, ndiyo utakayokufanya kukubukwa na siyo rangi yako, sura yako wala hata vyeti vyako. Utakumbukwa kwa mchango wako katika jamii,” alisema.

Amesema lengo kubwa la kuandaa mafunzo hayo ni kuhakikisha viongozi hao wanaongea lugha moja, hasa katika kuwatumikia wananchi kwa vile mchango wao katika mchakato mzima wa utoaji wa uamuzi ni muhimu na wenye tija, kwani maendeleo yanayoonekana na yale yanayotarajiwa ndani ya Mahakama hayawezi kupatikana bila wao.

“Haiwezekani Mtendaji Mkuu, Msajili Mkuu hata Jaji Mkuu na Jaji Kiongozi tukawa na mafanikio yoyote bila kuhakikisha kuwa nyinyi ambao ni sehemu ya menejimenti tunaongea lugha moja, tunakwenda kwenye kasi inayofanana na tunakwenda kwenye masafa na mwelekeo unaofanana,” alisema.

Mtendaji Mkuu huyo aliwaambia washiriki wa mafunzo hayo kuwa mafanikio yote yanayoonekana ndani ya Mahakama yanatokana na mchango wao mkubwa. Kwa mujibu wa Prof. Ole Gabriel, kuzungumzia uongozi bora katika taasisi yoyote ni kuona kwamba mambo yanafanyika kwa usahihi unaotakiwa, hivyo ni matamanio yake kuona viongozi hao wanafanya mambo sahihi kwa usahihi.

“Nyinyi sio bomba la kupeleka mambo kwa viongozi wenu, bali ni watu wa kusaidia kuchakata na kuyapeleka na maoni na mapendekezo ili kufanya uamuzi. Mfano, kama wewe ni mkuu wa idara au mkuu wa kitengo, haitapendeza kuwa mtu wa kupokea mambo na kufikisha kwa kiongozi bila wewe kuweka thamani yako kwenye mchakato wa kufanya uamuzi. Usipoweka thamani yoyote hufai na huna thamani yoyote,” alisema.

Kadhalika, Prof. Ole Gabriel aliwaomba viongozi hao kuzingatia Mpango Mkakati wa Mahakama na maelekezo mazuri yanayotolewa na Jaji Mkuu Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ili kuhakikisha haki yenye tija inapatikana kwa uwazi na kwa wakati.

“Hatuwezi kwenda vizuri bila nyinyi, nyinyi hasa ndiyo mataili yaliyobeba mafanikio ya Mahakama. Kila mtu kwenye idara yake afikirie hiyo, lazima ujiulize una thamani gani kwa ngazi yoyote ile, Mkurugenzi Msaidizi, Mkuu wa Kitengo, hata mimi Mtendaji Mkuu lazima nijiulize nina thamani gani ndani ya Mahakama,”alisema.

Akawashauri pia kuwa sehemu ya majibu na majawabu katika kufanya uamuzi na siyo kuwa sehemu ya matatizo. “Ndiyo maana wale Wachina wakasema haijalishi rangi ya Paka, mweusi, mwekundu, maadamu anakamata Panya ni Paka. Nasi tunaseme kwenye uongozi bora haijalishi kwamba upo kwenye nafasi gani, maadamu unatatua tatizo wewe ni kiongozi,” alisema Mtendaji Mkuu huyo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu alisema mafunzo hayo ya siku tatu yanalengo la kuwajengea viongozi hao uwezo katika nyanja mbalimbali ili waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu. “Tunatarajia mafunzo haya yatawasaidia viongozi hawa kuleta mabadiliko ya kifikra na kuwapa weledi katika kutekeleza kazi zao,” alisema.

Katika mafunzo hayo, wajumbe hao wa menejimenti watapitishwa na wazeshaji mahiri akiwemo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Iringa, Mhe. Dkt. John Utamwa kwenye mada mbalimbali, ikiwemo kuelewa utamaduni wa Mahakama, fikra za kimkakati na usimamizi wa mabadiliko na jinsi ya kukabiliana na msongo wa mawazo.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akisistiza jambo alipokuwa anafungua mafunzo kuhusu uongozi bora yanayotolewa kwa wajumbe wa menejimenti ya Mahakama ya Tanzania leo tarehe 26 Septemba, 2022 jijini Dar es Salaam.
Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki cha Masuala ya Familia, Mhe. Ilvin Mugeta (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho kabla ya ufunguzi wa mafunzo hayo. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na kushoto ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma.
Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu akitoa maneno ya utangulizi kabla ya ufunguzi rasmi wa mafunzo hayo.
Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia mambo mbalimbali yaliyokuwa yakijiri kabla ya ufunguzi wa mafunzo. Kutoka kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Dkt. John Utamwa, Mtendaji Mkuu wa Mahakama Kuu ya Tanzania,  Prof. Elisante Ole Ganriel, ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye ufunguzi wa mafunzo hayo na Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Ilvin Mugeta.
Meza kuu ikifuatilia utambulisho wa washiriki wa mafunzo hayo, ambao ni menejimenti ya Mahakama ya Tanzania (hawapo kwenye picha). 
Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo (picha ya juu na chini) ikifuatilia  hotuba ya ufunguzi iliyokuwa ikitolewa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.

Picha ya pamoja ikiwaonyesha Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania wa sasa, Mhe. Sharmillah Sarwatt (katikati) na watangulizi wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Dkt. John Utamwa na Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Ilvin Mugeta. 
Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wanawake wa mafunzo.

Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wote wa mafunzo.







Hakuna maoni:

Chapisha Maoni