Jumatatu, 31 Oktoba 2022

KITUO JUMUISHI TEMEKE CHANG’ARA MWAKA MMOJA TANGU KUANZISHWA

·Wadau wafunguka, hawaamini yanayotokea

Na. Mujaya Mujaya – IJC Temeke

Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke kilichopo jijini Dar es Salaam hivi karibuni kilisherekea mwaka mmoja tangu kianze kutoa huduma za utoaji haki kwa wananchi kwenye mashauri mbalimbali ya kifamilia yanayohusu watoto, ndoa, talaka na mirathi kwa kuadhimisha wiki ya huduma kwa mteja.

Maazimisho ya wiki hiyo yalianza tarehe 25 Oktoba 2022 ambayo ni mwaka mmoja kamili tangu Kituo hicho kilipoanza kutoa huduma zake rasmi tarehe 25 Oktoba 2021 na kukamilika tarehe 28 Octoba, 2022, huku wananchi wakipongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri, huduma bora na ushirikishwaji wa wadau wa haki madai ya mirathi na ndoa.

Katika maadhimisho hayo, wananchi waliofika mahakamani walipata fursa ya kupata huduma maalumu zilizolenga kuharakisha upatikanaji haki kwa wakati ambapo viongozi wa ngazi za juu walihusika moja kwa moja katika wiki nzima kuhudumia wateja kwenye dawati la mapokezi, kujibu simu za nje kutoka kwa wateja wanaofuatilia mashauri yao na kutoa elimu kuhusu huduma zinazotolewa.

Katika kipindi cha mwaka mmoja, Kituo Jumuishi Temeke kimehudumia watu 135,437, ambapo kati yao 71,915 ni wanawake, sawa na asilimia 53.1 na 63,522 ni wanaume ambao ni sawa na asilimia 46.9 ya watu wote walio hudumiwa.

Akizungumza kuhusu tukio hilo kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Kituo hicho, Mhe. Ilvin Mugeta, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Modesta Opiyo, alisema, "Kila mahali huwa naitabulisha Mahakama hii kama Mahakama ya wananchi. Asili ya watu tunaowahudumia wengi wanakuwa wameshaumia kwa namna moja ama nyingine, kwa hiyo huduma zetu huanza kurudisha faraja kwao. Utaona watu wameathirika kisaikolojia, tunajitahidi kuwarudishia tabasamu.”

Mhe. Opiyo aliendelea kufafanua, “Tungekuwa na urasimu kwa wananchi hawa, machungu yangeongezeka mara mbili, lakini mtu akija na kupata faraja anapata unafuu. Kwa mfano, katika Mahakama ya Mwanzo kwenye kituo hiki mtu ana andikisha shauri na kuonana na Hakimu siku hiyo hiyo, hii ndiyo dhana halisi ya haki sawa kwa wakati.”

Alisema kuwa Kituo hicho kitaendelea kuboresha huduma ili kutatua changamoto ambazo zitabainika. Kwa mujibu wa Jaji Opiyo, wametumia wiki hiyo ya huduma kwa mteja kujitafakari kila mmoja wao ili kuona wapi wanatakiwa kuboresha kwenye utendaji wao wa kazi.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Temeke, Mhe.  Martha Mpaze alizungumzia mashauri yaliyosajiliwa na kuamuliwa katika kipindi hicho cha mwaka mmoja na kueleza kuwa jumla ya mashauri 7,825 yanayohusu mirathi na ndoa yalifunguliwa katika ngazi zote za Mahakama, yani Mahakama Kuu, Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo.

Alibainisha kuwa hadi kufikia tarehe 25 Oktoba 2022, jumla ya mashauri 6,140 sawa na aslimia 78% ya mashauri yote yamemalizika na mashauri 1,685 bado yanaendelea kusikilizwa.

Naye Mtendaji wa Mahakama hiyo, Bi. Mary Shirima aliwapongeza watumishi wote kwa kufanya kazi wa kujituma na kutoa huduma bora zinazomlenga mwananchi, hatua iliyochagiza mafanikio hayo.

"Kwa takwimu tulizokusanya kutoka kwa wateja 4,414 kuhusu huduma zetu, 4,397 ambao ni sawa na asilimia 99.62% walisema huduma ni nzuri huku 17 pekee, sawa na asilimia 0.38% wakionesha kutokuridhiswa na huduma zetu. Bado tunafanya mawasiliano na wateja hao ili kupata maoni yao, tujue maeneo ya kuboresha," alisema.

Mama mmoja ambaye hakupenda jina lake litajwe alitoa ushuhuda wa namna alivyohudumiwa baada ya kuwasilisha shauri lake katika Kituo linalohusu masuala ya ndoa ambapo alionyesha kuridhika na huduma alizopata.

"Nilileta maombi ya talaka, jamaa akaitwa akaja, tukapangiwa tarehe na kusikilizwa, leo alikuwa anajitetea, kesho tunaenda kumaliza utetezi kisha hukumu. Yani ndani ya miezi miwili jambo linaisha. Sikutarajia kupata huduma nzuri mahakamani kama ninavyoona hapa Temeke, hadi najiuliza hivi Mahakama zote zipo hivyo?” alisema mteja huyo.

Naye Katibu wa Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania (BAKWATA) Wilaya ya Temeke, Ustadhi Mudhihir Mchoye amepongeza kuanzishwa kwa Kituo hicho kwani wamepata fursa ya kushirikiana na taasisi nyingine kama ustawi wa jamii, watu wa msaada wa kisheria au dawati la jinsia ili kuwahudumia wananchi kwa ukamilifu.

"Tunashukuru kwa uwepo wa taasisi mbalimbali zinazosaidia watu kisheria bila gharama yoyote au kwa gharama nafuu. Uwepo wetu umesaidia kuongeza uelewa katika mashauri yoyote ambayo yanahitaji ufafanuzi wa sheria ya dini ya kiislamu,"alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kituo cha Msaada wa Sheria kwa Wanawake (WLAC), Wakili Theodosia Nshala alieleza namna anavyoshangazwa na kasi iliyopo katika Kituo hicho katika kushughulikia mashauri yanayowasilishwa na wananchi.

“Mashauri huchukua muda mfupi hasa yale ambayo hayana changamoto za kisheria kwani mteja anaweza kupata msaada au huduma anayohitaji hapo hapo mahakamani bila kusafiri umbali mrefu. Pia mahusiano baina ya wadau wa haki mirathi na ndoa yameimarika kutokana na kufanya kazi kwa pamoja. Hatua hii inaharakisha upatikanaji wa haki na kumpunguzia gharama mwananchi,” alisema.

Kituo cha Masuala ya Familia Temeke kilianzishwa kupitia Gazeti la Serikali Na. 640 la mwaka 2021 kikijumuisha ngazi tatu za Mahakama ambazo ni Mahakama Kuu, Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo. Mahakama hizi zimepewa mamlaka kupitia Gazeti la Serikali Na. 641 na 639 kusikiliza mashauri ya ndoa na mirathi katika mkoa wa Dar es salaam.

Matangazo ya kuanzishwa Mahakama hiyo yalichapishwa katika Gazeti la Serikali la tarehe 27 Agosti 2021. Ngazi tatu za Mahakama tajwa na ofisi za wadau hutoa huduma ndani ya jengo moja, hivyo kuunda dhana ya Kituo Jumuishi cha Mahakama.

Meza kuu katika picha ya pamoja. Katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania anayehudumu katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Modesta Opiyo, Wengine ni Naibu Msajili, Mhe. Martha Mpaze (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama katika Kituo hicho, Bi. Mary Shirima (kulia).

Meza kuu (walioketi) katika picha ya pamoja na makarani wa Mahakama.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania anayehudumu katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Modesta Opiyo akimlisha keki Afisa Ustawi wa Jamii, Bi. Happyness Nyange kwa niaba ya wadau wa haki madai ya mirathi na ndoa katika zoezi la kuhitimisha wiki ya kuadhimisha mwaka mmoja wa Kituo hicho.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania anayehudumu katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Modesta Opiyo akimlisha keki Hakimu Mkazi, Mhe. Hamis Mlaponi kwa niaba ya watumishi na wateja wa Kituo Jumuishi Temeke wakati wa kuhitimisha wiki ya maadhimisho wa mwaka mmoja.

 

Watumishi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Kifamilia Temeke wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa kuhitimisha wiki ya kusherekea mwaka mmoja tangu kuianzishwa kwa Kituo hicho.

(Picha na Mujaya Mujaya – IJC Temeke)





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni