Jumatatu, 31 Oktoba 2022

BONANZA LA MICHEZO MAHAKAMA KANDA YA ZIWA LAFANA JIJINI MWANZA

 

·Jaji Mfawidhi Kanda ya Musoma afunika kwenye soka

Na Stephen Kapiga-Mahakama, Mwanza

Mahakama ya Tanzania katika Kanda ya Ziwa tarehe 29 Octoba, 2022 iliendesha bonanza maalumu la michezo lililowashirikisha watumishi wa kada mbalimbali wakiwemo Majaji, Naibu Wasajili, Mahakimu na Watendaji kutoka katika Mikoa ya Mwanza, Mara na Shinyanga.

Akifungua bonanza hilo lililofanyika katika Uwanja wa Nyamagana, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. John Kahyoza aliwapongeza watendaji wote kutoka Mahakama zilizoshiriki kwa kutoa ushirikiano kufanikisha jambo hilo.

“Kwanza niwapongeze watumishi wote mliosafiri na kuja Mwanza kwa ajili ya bonanza hili. Bonanza hili lina baraka zote za viongozi wa Mahakama, kwani ni sehemu ya mazoezi ambayo ni afya. Nawapongezeni wote kwa kuifanya siku hii ya pekee kuwa ni yenye furaha kwa kila moja wetu aliyehudhuria na kushiriki,” alisema.

Mhe. Kahyoza alielezea masikitiko yake kufuatia watumishi wa Mahakama kutoka Kanda ya Bukoba kushindwa kuhudhuria bonanza hilo baada ya kuchelewa kupata taarifa. “Niwasilishe salama za masikitiko kutoka kwa wenzetu wa Kanda ya Bukoba ambao walipenda kuwepo katika bonanza hili lakini walishindwa kufanya maandalizi kwa ajili ya safari ya kuja Mwanza kwa vile hawakupata taarifa kwa wakati,” alisema.

Jaji Mfawidhi huyo alitumia nafasi hiyo kuwaomba waratibu wa bonanza hilo kuandaa ratiba mapema na kuiwasilish kwa wenzao wa Bukoba ili waweze kujiandaa kwa ajili ya kushiriki.

Naye Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Tutubi Maganzini aliwashukuru viongozi wenzake kwa kuwawezesha watumishi kusafiri na kupangilia kila jambo kwa jinsi inavyotakiwa.

“Nawapongeza watendaji wenzangu kwa kuweza kufanikisha hili japo pamoja na maandalizi kuwa ya muda mfupi. Pamoja na faida za kiafya kwa watumishi pia bonanza hili linawezesha kufahamiana baina yetu, kwani hata mtumishi akihamishiwa Kanda nyingine kati ya hizi tatu tulizokutana hatakuwa mgeni,” alisema.

Bonanza hilo lilihusisha michezo ya riadha, mpira wa pete, kukimbiza kuku, kuvuta kamba, mpira wa miguu, mbio za magunia na mchezo maalumu wa aina yake wa kunywa soda.

Katika mchezo wa riadha uliowashirikisha Majaji, Naibu Wasajili na Watendaji, mshindi wa kwanza alikuwa Mtendaji Kanda ya Mwanza, Tutubi Mangazini ambaye alifuatiwa na Mtendaji Kanda ya Musoma, Festo Chonya na mshindi wa tatu alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, huku mshindi wa nne akiwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania kutoka Kanda hiyo hiyo, Mhe. Frank Mahimbali.

Kwenye mpira wa pete, timu ya Mahakama Kanda ya Mwanza iliigaragaza Kanda ya Musoma kwa vikapu 36-7. Katika shindano la kukimbiza kuku, Mhe. Mahimbali aliibuka mshindi kwa upande wa wananume, huku Editha Haule kutoka Kanda ya Shinyanga akichukua ushindi kwa upande wa wanawake. Mchezo huo pia uliwashirikisha watumishi wenye umri wa kuanzia miaka 50 ambapo ushindi ulienda kwa Michael Maduhu kutoka Kanda ya Shinyanga.

Katika mchezo wa kuvuta kamba kwa upande wa wanaume, timu kutoka Kanda ya Musoma iliwaburuza Mwanza na kwa upande wa wanawake timu ya Kanda ya Mwanza ikawakamua Kanda ya Musoma.

Mahakama Kanda ya Musoma iliwachapa Mwanza magoli 2-1 katika mchezo wa mpira wa miguu, huku goli la ushindi likifungwa kiufundi na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya. Katika mchezo huo, timu ya mpira wa miguu Kanda ya Shinyanga ilizifunga timu kutoka Kanza za Musoma na Mwanza kwa goli 1-0 kila mmoja.  

Kwenye shindano la kunywa soda pamoja na mkate kwa upande wa wanaume, mshindi alikuwa Leopord Ngowi kutoka Kanda ya Shinyanga na kwa upande wa wanawake mshindi alikuwa Amina Mlasi kutoka Kanda ya Musoma.

Kwa upande wa mbio za magunia wanaume, Donald Sondo  kutoka Kanda ya Musoma aliibuka kinara na kwa upande wa wanawake mshindi alikuwa ni Rose  Daudi kutoka Kanda ya Shinyanga.

Baada ya michezo hiyo iliyonza saa tatu asubuhi hadi saa kumi na moja jioni, watumishi wote wenyeji na wageni ambao walikuwa na nafasi walijumuika pamoja katika “Get Together Party’’ iliyofanyika katika Hotel ya Taiwan kwa lengo la kupongezena na kuondoa uchovu.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. John Kahyoza (picha juu) akizungumza wakati wa ufunguzi wa bonanza lililoshirikisha wanamichezo kutoka Kanda za Mwanza, Musoma na Shinyanga. Picha chini ni sehemu ya wanamichezo hao.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. John Kahyoza akikagua timu za mpira wa miguu kutoka Kanda ya Mwanza (picha juu) na Kanda ya Musoma (picha juu).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya akimhadaa mlinda mlango wa timu ya Kanda ya Mwanza kabla ya kuukwamisha mpira kwenye kamba na kuiandikia timu yake bao la pili na la ushindi.

Timu za mpira wa miguu Kanda ya Musoma na Mwanza zikiwa katikapicha ya pamoja kabla ya kumenyana kwenye bonanza hilo.

Timu ya Mpira wa Pete kutoka Kanda ya Mwanza kabla ya mpambano.

Timu ya Mpira wa Pete kutoka Kanda ya Musoma kabla ya mpambano.





Washindi katika mchezo wa riadha. Mshindi wa kwanza alikuwa Mtendaji Kanda ya Mwanza, Tutubi Mangazini (wa pili kushoto), mshindi wa pili alikuwa Mtendaji Kanda ya Musoma, Festo Chonya (wa pili kulia), mshindi wa tatu alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (kushoto) na mshindi wa nne akiwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania kutoka Kanda hiyo hiyo, Mhe. Frank Mahimbali (kulia).

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Frank Mahimbali akinyanyua kuku kama ishara ya ushindi baada ya kushinda mchezo wa kukimbiza kuku huyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni