Jumatano, 2 Novemba 2022

HUDUMA ZA MAHAKAMA ZITAMFUATA MWANANCHI: JAJI MRUMA

Na Innocent Kansha - Mahakama

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Amir Mruma amesema Mahakama ya Tanzania itahakikisha huduma zake zinamfuata mwanachi alipo na si mwanachi afuate huduma hizo umbali mrefu, kwani kwa kufanya hivyo muda wa uzalishaji mali utapungua na malengo ya taasisi ya kufikia mapinduzi ya nne viwanda yataathirika.

Akifungua rasmi jengo la Mahakama ya Mwanzo Chanika lililojengwa Kata ya Zingiziwa Wilaya ya Ilala jana tarehe 01 Novemba, 2022, Jaji Mfawidhi huyo alisema Mahakama itaendelea kushirikiana na Serikali na wadau wengine wote ili kufikia malengo yake ya kikatiba ya utoaji haki. Amesema jitihada   zilizofanyika kupatikana kwa huduma za kimahakama Chanika hazitaishia hapo bali zitakuwa hata katika maeneo mengine.

“Mfano Mahakama ya Mwanzo Ukonga iko katika jengo lisilokuwa la Mahakama na haina eneo hapo. Niwaombe viongozi wenzangu mtupatie ushirikiano wa kupata eneo. Mahakama ya Mwanzo Ukonga ni ya kwanza kwa wingi wa mashauri katika Wilaya yetu na inaweza kuwa kati ya Mahakama za Mwanzo tatu zinazopokea mashauri mengi zaidi nchini. Mahakama hii ina wastani wa Mashauri 4,153 kwa Mwaka”, alisema Jaji Mruma.

Jaji Mfawidhi huyo aliongeza kuwa, Mahakama inatambua juhudi zinazofanywa na viongozi wa Serikali na Mahakama kwa kushirikiana pamoja kusaidia upatikanaji wa maeneo yatakayowezesha ujenzi wa majengo mazuri ya Mahakama za Mwanzo Buguruni na Ukonga. Alisema Mahakama inatambua kuwa juhudi hizo bado hazijazaa matunda, hivyo akawaomba viongozi kujitahidi kufanikisha upatikanaji wa maeneo hayo.

“Ninaamini kwa juhudi za Jaji Mkuu wa Tanzania, ikiwa tutapata maeneo hayo tunaweza kupewa kipaumbele cha kujengewa majengo hayo kupitia Mpango Mkakati wa Mahakama wa uboreshoji wa Mahakama unaoendelea nchi nzima na kuifanya Mahakama ya Tanzania kwenda na kasi ya Dira ya Maendeleo ya Taifa na Serikali mtandao”, alisema.

Jaji Mfawidhi alisema ni faraja kwa Mahakama kuona kuwa, mwananchi atapata huduma za kimahakama katika Mahakama hiyo ya Mwanzo Chanika ambapo uwepo kwa Mahakama hiyo utasaidia kuepusha gharama na usumbufu kwa wananchi kufuata huduma hizo kwa umbali mrefu. Amesema ni dhahiri kuwa wananchi wa Kata takribani sita ambazo zinazozunguka eneo hilo, wataitumia Mahakama hiyo na uwepo wake utawasidia wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi, hivyo akawashauli waendelee kuilinda na kuitunza ili iendelee kuwahudumia.

Mhe. Mruma akawakumbusha wadau kuwa, Mahakama imepeleka sehemu ya nguvu kazi iliyokuwepo katika Mahakama za Dar es Salaam kufanya kazi katika Mahakama hiyo, akawaomba kuwapa ushirikiano ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na uaminifu mkubwa.

“Msiwashawishi kuingia katika vitendo vilivyo kinyume na maadili yao ya kazi. Na kwa watumishi mliopangwa katika Mahakama hii, mnao wajibu mkubwa wa kulinda heshima ya Mahakama ya Tanzania na kuwahudumia wananchi hawa kwa unyenyekevu na weledi mkubwa ili wananchi waliosubiri huduma hii kwa muda mrefu, waifurahie”, alisisitiza Jaji Mfawidhi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam (Kisutu), Bi. Athanasia Kabuyanja alisema kuwa mradi wa ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Chanika, ulianza tarehe 18 Aprili, 2021 na kukamilika tarehe 01 Julai, 2022 ambapo mradi ulikabidhiwa ujenzi huo umetekelezwa na Mkandarasi Becyma Quality Construction LTD na Msimamizi Mkuu wa mradi alikuwa ni Wakala wa MajengoTanzania (TBA).

Mtendaji Kabuyanja akaeleza kuwa, gharama ya utekelezaji wa mradi huo ni shilingi 438,938,294.42 ambazo tayari zimekwishalipwa kwa Mkandarasi. Gharama nyingine ni shilingi 8,513,000.00 zilizotumika kuchimba kisima kirefu cha maji na shilingi 6,252,000.00 zilizotumika kujenga mnara wa kuwekea matanki ya maji pamoja na kununua matanki. Hivyo thamani halisi ya utekelezaji wa mradi ni sawa na shilingi 453,703,294.42

Mtendaji huyo alisema jengo hilo la Mahakama ya Mwanzo Chanika lina ukubwa wa mita za mraba 364, likiwa na kumbi mbili (2) za Mahakama, ofisi mbili (2) za Hakimu, Ofisi sita (6) za watumishi wengine na vyumba viwili (2) vya kuhifadhia nyaraka na vielelezo. Vingine ni jiko na vyumba kwa ajili ya mahabusu ya wanaume na wanawake. Ujenzi wa jengo hilo pia ulijumuisha kazi za ujenzi wa choo cha umma cha nje, kuchimba kisima cha maji na ujenzi wa mnara wa kuwekea matanki ya maji.

Naye, Diwani wa kata ya Zingiziwa, Mhe. Maige Selemani Maganga akitoa salama kwa niaba ya wananchi alisema, niwakumbushe wakuu wangu na wajumbe kupeleka taarifa kwa wananchi kwamba Kata ya Zingiziwa imepata Mahakama na kazi yake kubwa ni kutenda haki bila kujali hali ya mtu, lakini mjue kuwa Mahakama ni chombo huru kinachofanya shughuli zake bila kuingiliwi katika maamuzi, jambo hilo ni muhimu sana wananchi wa eneo hili wakafahamishwa na kulielewa kwa ufasaha.

“Kwa maana kuna muda maamuzi yatatoka Mahakamani kuja kwa Diwani wakati sio sehemu sahihi ya kuyashughulikia, kwani hata Diwani mwenyewe anaogopa na kuheshimu maandishi mekundu, Mahakama inataratibu zake za kushughulikia mambo yote yaliyoamriwa kisheria”, alisema Mhe. Diwani huyo. 

Mhe. Maganga akawaasa wananchi kuwa, Kutokana na changamoto ya panya rodi na mambo mengine ya kiuhalifu na uvunjifu wa amani unaolikumba eneo hilo ni wajibu wa viongozi kwenda kuwaambia vijana kuachana tabia zenye viashiria vya kiuhalifu, na pengine kutojihusisha na vitendo hivyo na kuacha kukaa sehemu zisizokuwa na usalama kwani sasa chombo cha haki kipo na kinatenda kazi. 



Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Amir Mruma akikata utepe kuashiria uzinduzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Chanika lililojengwa Kata ya Zingiziwa Wilaya ya Ilala jana tarehe 01 Novemba, 2022, wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Obadia Bwegoge (wa pili kulia), Katibu Tawala wa Wilaya ya Ilala Bi. Charangwa Selemani Makwiro (wa kwanza kulia) na Diwani wa Kata ya Zingiziwa, Mhe. Maige Selemani Maganga (kushoto)


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Amir Mruma akitoa hotuba wakati wa uzinduzi wa jengo la kisasa la Mahakama ya Mwanzo Chanika lililojengwa Kata ya Zingiziwa Wilaya ya Ilala jana tarehe 01 Novemba, 2022.


Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam (Kisutu), Bi. Athanasia Kabuyanja akitoa taarifa ya mradi wa ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Chanika, ulianza tarehe 18 Aprili, 2021 na kukamilika tarehe 01 Julai, 2022


Diwani wa kata ya Zingiziwa, Mhe. Maige Selemani Maganga akitoa salama kwa niaba ya wananchi wakati wa uzinduzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Chanika lililojengwa Kata ya Zingiziwa Wilaya ya Ilala jana tarehe 01 Novemba, 2022


Sehemu ya wananchi waliofika kushuhudia uzinduzi wa jengo jipya la Mahakama ya Mwanzo Chanika wakimsikiliza mgeni rasmi (hayupo pichani)
Sehemu ya wananchi waliofika kushuhudia uzinduzi wa jengo jipya la Mahakama ya Mwanzo Chanika wakimsikiliza mgeni rasmi (hayupo pichani)


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Amir Mruma (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala mara baada ya uzinduzi wa jengo la kisasa la Mahakama ya Mwanzo Chanika, wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Obadia Bwegoge (wa pili kushoto), na Diwani wa Kata ya Zingiziwa, Mhe. Maige Selemani Maganga (kulia)


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Amir Mruma (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wananchi waliohudhuria kwenye hafla ya uzinduzi wa jengo la kisasa la Mahakama ya Mwanzo Chanika, wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Obadia Bwegoge (wa pili kushoto), na Diwani wa Kata ya Zingiziwa, Mhe. Maige Selemani Maganga (kulia)


Jengo la kisasa la Mahakama ya Mwanzo Chanika lililojengwa Kata ya Zingiziwa Wilaya ya Ilala.
  

 

Sehemu ya waimbaji wa Kwaya ya Mahakama ya Tanzania, (Mahakama Nq'aring'ari) wakitoa burudani katika hafla ya uzinduzi wa jengo la kisasa la Mahakama ya Mwanzo Chanika.

PICHA NA : Innocent Kansha - Mahakama

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni