Jumapili, 30 Oktoba 2022

MFUKUZA UPEPO KINARA SHIMIWI APOKELEWA KISHUJAA MAHAKAMANI MOROGORO

Na Evelina Odemba – Mahakama Morogoro 

Mcheza wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Juster Tibendelana juzi alipokelewa kishujaa alipowasili katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro anapofanyika kazi baada ya kushiriki katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yaliyofanyika huko jijini Tanga hivi karibuni na kuibuka mshindi wa kwanza kwenye riadha wanawake mita 3,000.

Justa hakuamini macho yake alipowasili katika Kituo hicho baada ya kulakiwa na umati mkubwa wa wafanyakazi wenzake wakiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe na viongozi wengine waandamizi na kupewa heshima zote za kishujaa, ikiwemo kukabidhiwa keki maalumu iliyokuwa imeandaliwa kwa ajili ya kumpongeza kwa ushindi huo mkubwa alioupata.

Binti huyo mdogo mwenye sifa ya MMM, yaani, Mpole, Mcheshi na Mwelevu ambaye ni Mwembamba wa wastani, Mrefu wa wastani na Mweusi wa wastani, mwenye umbo fulani hivi na macho ya kuvutia, alibaki akiwapungia mikono watumishi wenzake huku akimwaga tabasamu murua la karne ya 21, hatua iliyoibua furaha kila kona katika viunga vya Kituo hicho.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Ngwembe ambaye alikuwa mgeni rasmi alisema kuwa ni jambo la kujivunia kwa mtumishi huyo mwaminifu kupata ushindi huo na kusisitiza kuwa ushindi huo haukuwa wa Justa pekee bali ni wa Mahakama ya Tanzania kwa ujumla.

“Tunafurahia sana jinsi alivyotuwakilisha mtumishi mwenzetu Justa kwa kuwa mshindi wa kwanza katika mbio za mita 3,000 upande wa wanawake, hii pia imewezekana kutokana na juhudi alizozionyesha pamoja na ushirikiano mkubwa toka kwa watumishi wenzake, hongera sana,” Jaji Mfawidhi huyo alisema.

Mhe. Ngwembe alimvisha Justa medali ya dhahabu aliyoipata katika mashindano hayo ya SHIMIWI yaliyoanza tarehe 1 Octoba 2022 na kuhitimishwa tarehe 15 Octoba 2022. Katika mashindano hayo, Mahakama Sports iliwatimulia vumbi washiriki wengine kutoka taasisi mbalimbali kwa kuzoa makombe saba, ambayo kati ya hayo ilikabidhiwa manne.

Naye Mtendaji wa Mahakama wa Kanda, Ahamed Ng’eni alimpongeza shujaa huyo kwa mshindi mnono na kuwataka watumishi wengine kujituma kufanya mazoezi na kujiandaa vyema ili wakati ujao, Mahakama iweze kutoa washindi wengi zaidi.

Akipokea pongezi hizo, Justa alionekana kuhemewa na furaha na kusema kuwa anashukuru kwa ushirikiano mkubwa alioupata kwa viongozi wa Mahakama na watumishi wenzake ambao ulichagiza ushindi wake. Vilevile alifikisha salamu za ushindi wake zilizotolewa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.

Mapokezi hayo pia yaliambatana na kumkaribisha Jaji mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Gabriel Malata ambaye amewasili katika Kituo hicho hivi karibuni kwa ajili ya kuwahudumia wananchi katika Kanda hiyo ya Morogoro. Mhe. Malata aliahidi kutekeleza majukumu yake ipasavyo huku akiomba ushirikiano wa dhati toka wa watumishi na wadau wa Mahakama.

Justa Tibendelana (aliyeshika keki katikati) akifurahia zawadi hiyo katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro. Kulia kwake ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Morogoro, Mhe. Maua Hamduni.

Justa Tibendelana akiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Morogoro, Ahmed Ng'eni (kulia) na Kaimu Msajili, Mhe. Japhet Manyama (kushoto) baada ya kukabidhiwa keki ya pongezi.
Keki tamu kwelikweli.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe akimvisha medali ya ushindi Justa Tibendelana.

Hongera sana kwa ushindi.

Justa Tibendelana akiwa katika harakati za kuunyakua ushindi baada ya kuwatimulia vumbi washiriki wengine kwenye mashindano ya SHIMIWI Tanga.
Viongozi na watumishi wa Mahakama Kanda ya Morogoro wakigonga chiazi pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Gabriel Malata (katikati), kama ishara ya kumkaribisha katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki mkoani hapo.

Mhe. Malata akimlisha keki Jaji wa Mahakama Kuu Morogoro, Mhe. Messe Chaba wakati wa hafla ya kumkalibisha katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro.

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni