Jumatatu, 7 Novemba 2022

JAJI MFAWIDHI DAR ES SALAAM ASHAURI NGUVU ZA PAMOJA KUPAMBANA NA UHALIFU WA KIFEDHA

Na Faustine Kapama – Mahakama

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma amewasihi wadau mbalimbali wa haki jinai duniani kuunganisha juhudi na nguvu kitaifa, kikanda na kimataifa ili kupambana kikamilifu na uhalifu wa kifedha, hususani katika makosa dhidi ya wanyamapori, ugaidi na utakatishaji fedha.

Mhe. Mruma ametoa wito huo leo tarehe 7 Novemba, 2022 alipokuwa anafungua mafunzo kuhusu makosa ya kifedha ya siku tano ambayo yanawaleta pamoja Majaji 14 na Mahakimu Wakazi 26 ili waweze kubadilishana uzoefu kwenye maeneo mbalimbali, ikiwemo sheria za kimataifa na kitaifa za biashara haramu kwenye makosa hayo.

Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo ambayo yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Taasisi ya Kikundi cha Kupambana na Utakatishaji Fedha cha Mashariki na Kusini mwa Afrika-The Eastern and Southern Africa Anti-Money Laundering Group (ESAAMLG) na Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ), Jaji Mfawidhi huyo alibainisha kuwa utakatishaji fedha, ufadhili wa ugaidi na biashara haramu ya wanyamapori ni makosa makubwa yanayohusisha makundi ya wahalifu waliojipanga.

"Hakuna nchi ambayo haijaguswa na uhalifu huu, ambao unaathiri bioanuwai, afya ya binadamu, usalama wa taifa, ongezeko lisiloelezeka la mahitaji ya bidhaa na huduma, uadilifu wa mfumo wa kifedha na maendeleo ya kijamii na kiuchumi huku ukiboresha vikundi vya uhalifu. Ni kupitia utakatishaji fedha ambapo shughuli haramu ya fedha inahalalishwa. Mafunzo haya yanafanyika kwani yanaongeza kiwango cha uelewa miongoni mwetu maafisa wa Mahakama, ni matumaini yangu wadau wengi wa sekta ya haki watafikiwa,” alisema.

Jaji Mruma alibainisha pia kuwa ongezeko la haraka la utandawazi na shughuli huria za kifedha bila shaka umefanya utakatishaji fedha kuwa mojawapo ya migogoro ya kimataifa. Amesema hali hiyo imepelekea umuhimu wa uwepo wa mikakati na juhudi za pamoja kwa ajili ya vita dhidi ya utakatishaji fedha, hivyo akasisitiza nchi lazima zishiriki katika vita hiyo.

Alisema kwa kutambua ukweli huo mashirika kadhaa ya kimataifa, ambayo ni mashuhuri zaidi katika mapambano dhidi ya utakatishaji fedha na ufadhili wa kigaidi duniani (The Financial Action Task Force (FATF), yameandaa mapendekezo na mbinu bora ili kusaidia nchi zote kuimarisha juhudi zao katika mapambano hayo.

Aliipongeza ESAAMLG katika kupambana na utakatishaji fedha kwa kutekeleza mapendekezo ya FATF. Jaji huyo alidokeza kuwa ESAAMLG imekuwa ikishirikiana na mashirika mengine ya kimataifa yanayohusika na kupambana na utakatishaji fedha, kuendeleza uwezo wa kitaasisi na rasilimali watu na kuratibu usaidizi wa kiufundi pale inapobidi.

“Napenda kuwahakikishia kuwa Mahakama ya Tanzania inafanya kazi kwa bidii katika kutoa huduma kwa gharama nafuu na kwa ufanisi ambao utaleta maendeleo endelevu kwa taifa letu. Vile vile tunawashukuru ESAAMLG na GIZ kwa kukubali ombi letu la kuendesha mafunzo haya kwa Majaji na Mahakimu na hasa utayari wao wa kusaidia mafunzo katika awamu mbili, moja kwa Mahakimu 40 na haya yanayoanza leo,” alisema.

Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo kwa niaba ya Mkuu wa Chuo cha IJA, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, Mratibu wa Mafunzo ya Mahakama IJA, Mhe. Eliya Baya alisema kuwa kufanyika kwa mafunzo hayo ni muendelezo mwingine kama hayo yaliyotolewa kwa kundi la kwanza la Mahakimu 40 mwezi Septemba mwaha huu.

Alipendekeza IJA, GIZ na ESAAMLG kuandaa na kuratibu mafunzo zaidi kwa maafisa wengine wa Mahakama na wadau wa haki jinai katika siku za usoni ili kujenga uelewa kuhusu tishio linalosababishwa na wahalifu wanaojihusisha na uhalifu, kutenda makosa yanayohusu utakatishaji fedha, ufadhili wa ugaidi, biashara haramu ya wanyamapori na uhalifu mwingine unaohusiana na hayo.

Wawezeshaji wa mafunzo hayo ni baadhi ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Ofisi ya Mashtaka ya Taifa, Wizara ya Maliasili na Utalii, wawezeshaji kutoka Mamlaka za Wanyamapori za baadhi ya nchi barani Afrika na wawezeshaji wabobevu kutoka mataifa mbalimbali duniani.

Katika mafunzo hayo washiriki watapitishwa kwenye maeneo mbalimbali, ikiwemo sheria za kitaifa na kimataifa zihusuzo makosa dhidi ya wanyamapori, ugaidi na utakatishaji fedha; madhara ya makosa hayo katika taifa na dunia; urejeshaji wa mali zilizopatikana kutokana na makosa hayo na wajibu wa maafisa wa Mahakama, wapelelezi na waendesha mashtaka katika uendeshaji wa mashauri yanayohusu makosa hayo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma akiongea wakati anafungua mafunzo kuhusu makosa ya kifedha yanayojumuisha Majaji na Mahakimu kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Mratibu wa Mafunzo ya Mahakama IJA, Mhe. Eliya Baya akieleza jambo wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma akiwasili katika ukumbi wa mkutano katika hoteli ya Ramada yanapofanyikia mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo (juu na chini).

Sehemu nyingine ya washiriki wa mafunzo (juu na chini).


Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma (katikati aliyekaa) ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe kutoka Kikundi cha Kupambana na Utakatishaji Fedha cha Mashariki na Kusini mwa Afrika-The Eastern and Southern Africa Anti-Money Laundering Group (ESAAMLG) wanaoshiriki katika mafunzo hayo.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma (katikati aliyekaa) ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Sekretarieti kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.
Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma (katikati aliyekaa) ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji wanaoshiriki katika mafunzo hayo.
Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma (katikati aliyekaa) ikiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wanaoshiriki katika mafunzo.



Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma (katikati aliyekaa) ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wote wa mafunzo hayo.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni