Ijumaa, 4 Novemba 2022

JESHI LA POLISI LATOA ELIMU KUHUSU USALAMA BARABARANI MAHAKAKANI MOROGORO

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Elimu ya usalama barabarani iliyoanza kutolewa kwa wateja wa Mahakama katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro kuanzia tarehe 1 Novemba, 2022 imeitimishwa jana tarehe 3 Novemba, 2022.

Mahakama ya Tanzania kupitia vipindi vya elimu ya sheria kwa wananchi wiki hii walitoa mualiko kwa jeshi la Polisi mkoani hapa kutoa mafunzo ya siku tatu kwa wananchi ili kujilinda na masuala mbalimbali ya usalama wawapo barabarani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo maalum, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe alisema kuwa Mahakama mkoani hapo haitosimama peke yake katika kuwapatiwa wananchi elimu, bali itashirikiana na taasisi mbalimbali ambazo ni wadau wa Mahakama ili kumsaidia mwananchi awe salama.

“Hatutasimama Mahakama peke yetu kwani Serikali ina mkono mrefu, hivyo tutawatumia wataalamu toka taasisi zingine kuwafikia wananchi hawa, ndio maana tunapoelekea mwisho wa mwaka tumewaalika jeshi la Polisi kitengo cha usalama barabarani watufundishe ili tuendelee kuwa salama na tumepanga kuwafikia wananchi zaidi ya mia tano ndani ya hizi siku tatu.” aliongeza.

Aidha Mhe. Ngwembe alieleza kuwa baada ya Mahakama kuanza kutoa elimu hiyo kumekuwa na mabadiliko makubwa kwa wananchi wa Mkoa huo ambapo kesi zinazopelekwa mahakamani ni zile zenye mantiki, kwa kuwa jamii imeelimishwa na kuepuka kutenda makosa kwa makusudi. Amesema elimu hiyo pia imepunguza malalamiko mengi kwani sasa wananchi wanauelewa katika masuala mbalimbali.

Akitoa elimu kwa wananchi, Mratibu Mwandamizi wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro Zauda Mohamedi alisema kuwa Jeshi la Polisi lipo tayari kushirikiana na raia wema wote ili kuhakikisha usalama unadumu, huku akipongeza jitihada za uongozi wa Mahakama kwa mkakati wake wa elimu na kuahidi kutoa ushirikiano kila mara watakapohitajika kufanya hivyo.

Kwa muda wa siku tatu wananchi walifundishwa mambo mbalimbali ikiwemo haki za abiria, umuhimu wa kuwa na bima, usalama barabarani na ulinzi wa mtoto, ambapo waelimishaji mbalimbali kutoka Jeshi la Polisi walikuwepo kutoa elimu hiyo, akiwemo Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi la Polisi mkoani hapa Emmanuel Kaboja pamoja na Inspekta Victoria Godrich kutoka Stendi Kuu ya Mabasi.

Naye mteja aliyefika mahakamani hapo, Bw. Rashid Omary kutoka Malinyi alitoa shukurani zake kwa uongozi wa Mahakama kwa kuwa na maono ya mbali ya kuwapatia elimu hiyo kwani inawasaidia kuepuka kutenda makosa na kuendelea kufanya shuguli za kuwapatia kipato.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha mafunzo hayo, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba aliwakaribisha wananchi waendelee kufika siku zijazo kwani wataalam mbalimbali watendelea kuja kutoa elimu. Kadhalika, Mhe. Chaba alilishukuru Jeshi la Polisi kwa ushirikiano waliouonyesha na kuomba wasisite tena kufika watakapoombwa kufanya hivyo.

Tokea kuanzishwa kwa elimu ya sheria kwa wananchi katika kituo hicho mwezi Machi 2022 kumekuwa na muitikio mkubwa wa wananchi ambao wengine hufika kwa ajili ya kusikiliza vipindi hivyo tu na mpaka sasa tathimini inaonesha wananchi zaidi ya 20,000 wamepata elimu hiyo, huku takwimu zikionyesha wananchi 150 mpaka 200 hufikiwa na elimu hiyo kwa siku.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (aliyesimama) akizungumza na wananchi wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya usalana barabarani yaliyotolewa na Jeshi la Polisi.
Maafisa wa Jeshi la Polisi (juu na chini) wakitoa elimu kwa wananchi. 

Jaji wa Mahakama kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba akiongea na wananchi wakati wa kuhitimisha elimu ya usalama barabarani iliyotolewa na Jeshi la Polisi.

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni