Jumatatu, 21 Novemba 2022

MAHAKAMA IMEFANYA UBORESHAJI WA HUDUMA KATIKA MAENEO MENGINE SI MAJENGO PEKEE: JAJI MKUU

 Na Lydia Churi-Tume ya Utumishi wa Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amesema Mahakama ya Tanzania imefanya uboreshaji wa huduma zake katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.

Akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga leo wakati wa ziara ya Tume ya Utumishi wa Mahakama mkoani humo, Jaji Mkuu alisema maboresho ya huduma za Mahakama yaliyofanywa na Mhimili huo ni mengi na siyo ujenzi wa majengo ya Mahakama peke yake.

Jaji Mkuu alitaja aina ya uboreshaji wa huduma za Mahakama uliofanyika kuwa ni pamoja na mapinduzi makubwa ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika shughuli za Mahakama Pamoja na utoaji wa huduma za kimahakama kwa uwazi na kwa ufanisi.

Alisema uboreshaji mwingine wa huduma za Mahakama uliofanyika licha ya ujenzi wa majengo ya Mahakama ni mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa na ukiukwaji wa maadili kwa watumishi wa Mahakama.

“Hili ni eneo ambalo tunajipima na kujitathmini sana, malalamiko katika eneo hili yamepungua kwa kiasi kikubwa”, alisema Jaji Mkuu.

Aidha, Jaji Mkuu amewataka watumishi wa Mahakama kuyafanya maboresho na mafanikio yaliyopatikana kuwa endelevu kwa kusoma na kujifunza yale yanayoendelea ili kukabiliana na changamoto kubwa ya nchi zinazoendelea ya kuanzisha mambo mazuri lakini hayawi endelevu.

Kuhusu matumizi ya Tehama ndani ya Mhimili wa Mahakama, Jaji Mkuu amewataka watumishi kujiandaa kuingia kwenye matumizi ya kidigitali katika utoaji wa huduma. Alisema Mahakama ya Tanzania inaandaa mtaala mpya wa mafunzo ambapo watumishi wake wote watapata mafunzo ya namna ya kutoa huduma kidigitali.

Naye Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye pia ni Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi amewataka watumishi wa Mahakama kutojivuta katika kuingia kwenye matumizi ya Tehama kwa kuwa tayari uwekezaji mkubwa umefanywa na Mahakama ya Tanzania.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel akifafanua kuhusu upungufu wa watumishi wa Mahakama alisema matumizi ya TEHAMA yatasaidia kwa kiasi kikubwa kutatua tatizo la upungufu wa watumishi.

Aidha, alitoa wito kwa kila Kanda ya Mahakama Kuu ya Tanzania kuona namna ya kuangalia ni maeneo yapi yatahitaji kutumia Tehama ili kurahisisha kazi za utoaji haki na pia kutatua changamoto ya upungufu wa watumishi.

Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wako kwenye ziara ya siku nne katika mikoa ya Shinyanga na Simiyu yenye leo la kutangaza shughuli za Tume hiyo na pia kukutana na wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama ngazi ya Mkoa na wilaya pamoja na wadau wa utaoji haki.

Makamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wakifuatilia jambo wakati wa Mkutano kati yao na Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Shinyanga leo mkoani humo 
Watumishi Mahakama kuu kanda ya Shinyanga wakimsikiliza Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alipokuwa akizungumza nao leo mkoani humo 

Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza wakati wa Mkutano wa Tume na Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga leo mkoani Shinyanga.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye pia ni Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama  Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi akizungumza wakati wa Mkutano wa Tume na Watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga leo mkoani Shinyanga.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni