Jumanne, 24 Januari 2023

SIMULIZI YA KUSISIMUA YA MZEE BINGWA WA KUTATUA MIGOGORO MTWARA

· Ni Mzee wa Kimakonde mwenye umri wa miaka 61

·Amerithi kipaji cha usuluhishi kutoka kwa babu yake

·Mbinu zake za utendaji zafananishwa na busara za Mfalme Suleiman

·Adai usuluhishi lazima ufanyike majira ya jioni kulinda usiri

Na Mwandishi Wetu

Wakati Wiki ya Sheria nchini yenye kauli mbiu “Umuhimu wa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya Usuluhishi: Wajibu wa Mahakama na Wadau” ikizinduliwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango, Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara imegundua uwepo wa mwananchi mwenye kipaji cha kipekee cha utatuzi wa migogoro nje ya Mahakama.

Mwanachi huyu ni Issa Mohamed Mkumba (61), Mkazi wa Kijiji cha Msimbati, Kata ya Msimbati katika Wilaya ya Mtwara.

Akiongea na Mwandishi wetu Mjini Mtwara, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Mh. Zainab Muruke anaeleza kuwa waligundua uwepo wa Mzee Mkumba baada ya kufanya ziara katika Mahakama ya Mwanzo Msimbati ambapo alielezwa uwepo wa kesi chache zilizofunguliwa mahakamani kutokana na migogoro mingi kusuluhishwa nje ya vyombo rasmi vya dola.

“Ilikuwa mwaka jana. Nilipotaka kujua zaidi kwa nini hali hii ipo hivyo ndipo nikatajiwa jina la Issa Mohamed Mkumba.  Watu wengi walimsifu kuwa anafanya kazi yake vizuri,” anaeleza Jaji Muruke.

Kama njia mojawapo ya kutambua mchango wake na kujifunza zaidi kuhusu kazi zake, Jaji Mfawidhi huyo anaeleza kuwa alimwalika Mzee Mkumba ofisini kwake siku ya Jumamosi tarehe 21 Januari, 2023 kwa mazungumzo na kubadilishana uzoefu.

Katika mazungumzo hayo yaliyohudhuriwa pia na Jaji wa Mahakama Kuu katika Kanda hiyo, Mhe. Dkt. Eliamani Laltaika, Naibu Msajili Amiri Msumi na Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda, Bw. Richard Mbamba, Jaji Mfawidhi anasema kuwa Mzee Mkumba alieleza kwa kirefu kuhusu changamoto na mafanikio ya kazi zake. 

Elimu na urithi

Jaji Mruke anamnukuu Mzee Mkumba akieleza kuwa yeye ana elimu ya darasa la nne aliyoipata katika shule ya Msingi Msimbati pamoja na elimu ya dini ya Kiislam (madrassa) aliyoipata akiwana na umri mdogo. Anasisitiza kuwa mbali na elimu hizo, amerithishwa maarifa mengi kutoka kwa wazee wake, hususan babu yake ambaye mara kwa mara aliambatana naye katika shughuli za usuluhishi.

“Babu yangu alikuwa akiamua migogoro. Baadaye alimuachia baba yangu nami nimerithi kwa baba,” Jaji Mdawidhi anamnukuu Mzee Mkumba akieleza.

Hekima za Mfalme Suleiman

Mzee Mkumba anabadilishana uzoefu na Viongozi Waandamizi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara kwa kusimulia kisa kimoja na namna alivyo kitolea unamuzi unofanana na simulizi za Mfalme Suleiman katika mgogoro wa wanawake waliokuwa wakigombea mtoto.

Mwanamke Mwenye Kuku ni Yupi?

Katika simulizi hiyo, Mzee Mkumba, kwa mujibu wa Mhe. Mruke, anaeleza kuwa wanawake wawili walifika kwake wakigombania kuku ambaye mmoja wao alikuwa akienda kumuuza sokoni. Kila mmoja kati ya wanawake hao aling’ang’ania kuwa ndiye mwenye kuku.

“Niliwaomba wakae nami mpaka jioni. Ilipofika jioni nikawaambia turudi mtaani kwao. Tukifika tutamuachia huyu kuku na kuona atakimbilia wapi. Mama mwenye nyumba atakapoelekea kuku ndiye atakuwa mmiliki,” ananukuliwa Mzee Mkumba akisimulia huku akionyesha kujiamini.

Huku akisisitiza, Mzee Mkumba anaendelea kunukuliwa akieleza, “Tulipomuachia tu yule kuku alikwenda moja kwa moja kwa yule mama aliyetaka kumuuza. Tukakubaliana kuwa yule mama aliyesingiziwa kuwa kaiba kuku alipwe fidia ya shilingi elfu kumi.”

Kwanini Kusuluhisha Jioni?

Mzee Mkumba anasisitiza kuwa kazi zake za usuluhishi hupendelea kuzifanya jioni kabisa mpaka saa sita za usiku.

Jaji Mfawidhi anamnukuuu Mzee Mkumba ambaye anasisitiza, “Kwa Kimakonde tunamsemo unaosema ‘Samaki hanoni usiku’. Vitu vigumu vinaweza kufanyika kirahisi usiku kwani kunakuwa na utulivu. Ni rahisi pia kuzungumzia mambo ya siri bila taarifa kuwafikia wasio husika. Usiku hulinda usiri,” anasisitiza Mzee Mkumba huku akitumia Nahau na Semi za busara za jamii yake ya Kimakonde.

Kumbukumbu ziandikwe

Akihitimisha mazungumzo hayo yaliyodumu kwa takribani saa tatu, Jaji Muruke alitoa wito wa kutunza kumbukumbu za busara za wazee kama Mzee Mkumba katika maandishi.

Mahakma Kuu Kanda ya Mtwara imepanga kuwafikia watu wa rika mbalimbali na kutoa elimu ya sheria, hususani suala la kumaliza migogoro kwa njia ya usuluhishi.

Wadau mbalimbali wamejipanga kushirikiana na Mahakama kutoa elimu kwa njia mbalimbali ikiwemo redio za jamii, pamoja na kutembelea maeneo kadhaa, ikiwemo shule za sekondari na msingi, magereza, utoaji wa msaada wa kisheria ikiwa ni pamoja na kusikiliza malalamiko na kuyatafutia ufumbuzi. 

Huyu hapa bingwa wa kutatua migogoro nje ya Mahakama, Mzee Issa Mohamed Mkumba (61), Mkazi wa Kijiji cha Msimbati, Kata ya Msimbati katika Wilaya ya Mtwara.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Mh. Zainab Muruke anamkubali kwa sana tu Mzee Issa Mohamed Mkumba.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni