Jumatano, 1 Februari 2023

JAJI SALMA: ATAKA UTAYARI WA WANANCHI KUTATUA MIGOGORO KWA NJIA YA USULUHISHI

           Na Magreth Kinabo -Mahakama

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi amesema kwamba utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi utawezekana pale ambapo wananchi wenyewe watakua tayari, kufuata taratibu za kimahakama na wadau wengine nje ya Mahakama kwa kuhudhuria pale wanapohitajika.

Kauli     hiyo imetolewa na  Jaji Salma wakati akiwa mgeni rasmi wa kilele cha Siku ya Sheria katika kanda hiyo, kilichofanyika leo tarehe 1 Februari, mwaka 2023 kwenye Viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Jijini Dar es Salaam, ambapo alisema hayo yote yatawezesha Mahakama na wadau hao kuwahudumia kwa wakati, na kwa ubora zaidi.

“Napenda kuchukua nafasi hii kutoa wito kwa kila mwananchi, kufahamu umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi una faida kubwa katika kukuza uchumi endelevu. Wananchi pia tujisomee sheria ili tuwe na uelewa angalau kidogo wa sheria. Tusiwaachie mawakili na wanasheria peke yao jukumu la kufahamu taratibu za sheria hizi za utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi.

“Tunapokuwa na jambo linalohusu sheria, mathalan ya madai, ndoa, mwenendo wa makosa ya jinai, sheria ya usuluhishi nje ya Mahakama hatua ya mwanzo kabisa ni mwananchi asome vifungu vya sheria husika yeye mwenyewe na apate uelewa kabla ya kufungua shauri Mahakamani, mwananchi ahakikishe kuwa anafahamu hatua zote kesi yake itapitia katika ngazi ya Mahakama zote hadi Mahakama ya Rufani. Hauhitaji elimu ya Sheria kujua hatua muhimu ambazo kesi zako zitapitia.

Aliongeza kwamba  kauli mbiu ya mwaka huu ni “Umuhimu wa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya Usuluhishi Katika kukuza Uchumi Endelevu: Wajibu wa Mahakama na Wadau”. Kazi ya kutatua migogoro inayohusisha wadau mbalimbali, wadau hao wakitimiza wajibu wao kwa wakati, wataiwezesha Mahakama kumaliza mashauri na wananchi kupata suluhu na haki zao kwa wakati.

Jaji Salma alisema utatuzi wa migogoro mahakamani na nje ya mahakama kwa njia ya usuluhishi unafaida nyingi ikiwa ni pamoja na; Serikali ni mdau muhimu na wezeshi kwa Mahakama katika kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi ili kukuza uchumi endelevu, upatikanaji wa haki kwa wakati kwa gharama nafuu, utatuzi wa migogro kwa njia ya ustaarabu, amani na kwa muda mfupi bila kufungwa na masharti ya sheria na taratibu za kiufundi.

Hivyo kuwawezesha wananchi kushiriki katika shughuli za kukuza \uchumi ikilinganishwa na njia ya kawaida ya usikilizaji/uendeshaji wa mashauri inayoweza kuchukua muda mrefu. Faida nyingine ni huzingatia maslahi ya wadaawa ili kulinda mahusiano yao ya kijamii na kiuchumi,Gharama hupungua kwa kila upande baina ya wadaawa na Mahakam  na  huhifadhi mahusiano ya kibiashara na ya kijamii kwa wadaawa.

Aliushukuru uongozi ya mkoa wa Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani kwa kuwa mstari wa mbele katika kusaidia kuleta maboresho yanayosukumwa na dhana ya kupeleka huduma za haki kua karibu na wananchi.”Ninachukua fursa hii kukushukuru wewe na uongozi wa serikali mnazoziongoza kwa kusaidia kupata maeneo ya ujenzi wa Mahakama kwa Mahakama ya Mwanzo Madale Wilaya ya Kinondoni, Mahakama ya Wilaya Ubungo, Mahakama za Mwanzo Gezaulole Wilaya ya Kigamboni, Chamanzi wilaya ya Temeke na Lubakaya-Wilaya ya Ilala kwa mkoa wa Dar es Salaam,” alisisitiza.

Kwa Mkoa wa Pwani umewezesha kupata maeneo ya ujenzi wa Mahakama Kuu Kibaha na Mkamba-Kisarawe.ambapo aliomba salamu hizo zifikishwe  kwa Mhe. Mkuu wa Mkoa wa Pwani.

Akizungumza kwa niaba ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Mwema  Punzi ambaye ni Mwanasheria wa Serikali Mkuu, alisema   katika jamii yoyote inayostawi utawala wa sheria unabaki kuwa nguzo katika kukua na kuendeleza Taifa, Mahakama huru na thabiti ni muhimu  kwenye utawala wa maendeleo ya kiuchumi kwa tafsiri adili na kwa wakati Pamoja na utekelezaji wa haki za uchumi vinasaidia kujenga stahiki yanayohitajika katika uwekezaji na ukuaji wa uchumi wetu.

“Ofisi yangu imewaidhinisha watoa huduma 494 za usuluhishi, majadiliano, na upatanishi wenye sifa. Idadi hiyo ni ndogo ukilinganisha na mahitaji halisi yan chi. Migogoro yenye  asili ya madai iliyopo kwenye Mabaraza ya Ardhi na Nyumba na Mahakama za Mwanzo yapo zaidi ya mashauri 15.000 ya madai ya aina mbalimbali hayajaisha katika Mahakama za  Mahakimu na zile za juu,” alisema  Mwema.

Mhe. Mwema alisema ofisi yake na Wakili Mkuu wa Serikali wataendeleakusimamia kwa niaba ya Serikali matakwa ya kisheria ya kutatua migogoro k wa njia ya usuluhishi.
Kwa upande wake Kiongozi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika Kanda ya Mzizima, Bi. Tike Mwambipile alisema   mawakili wa kujitegemea waanze kutumika ipasavyo kwa kutoa huduma hiyo ya utatuzi wa migogoro mbalimbali kwa suluhu  kwa kuwa wanawataalamu wa kutosha. Hivyo kushiriki kwao katika suala hilo itasaidia kupunguza migogoro ya ardhi, mirathi na ndoa.ikiwemo kuwapunguzia muda wanaoutumia wakuu wa mikoa na wilaya kushughulikia migogoro mbalimbali.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Kanda hiyo, Mhe.Elizabeth Nyembele alisema jumla ya wananchi 27,284 walipatiwa elimu ya sheria katika maeneo mbalimbali.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Dares Salaam, Mhe. Amos Makalla alisema yuko tayari kushirikiana na Mahakama katika kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi ili kuweza kuwasaidia wananchi kupata haki zao gharama nafuu na kuwawezesha kushiriki kwenye shughuli za uzalishaji mali na kujipatia kipato.

Sherehe hizo pia zilihudhuriwa na baadhi ya viongozi wa dini, ambao waliiombea Mahakamma iendelee kutoa haki kwa uadilifu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi(kulia) akiongoza maandamano ya wanataaluma ya sheria, kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es   Salaam Mhe. Amos Makalla katika kilele cha Siku ya Sheria Nchini iliyofanyika leo tarehe 01/02/2023 katika Viwanja vya Hakimu Mkazi Kisutu.


  Sehemu ya maandamano hiyo ikiendelea.

Gwaride maalum likiwa tayari kwa ajili ya ukaguzi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi (mbele) akiwa Pamoja na majaji wengine wakipokea salamu kutoka kwa gwaride hilo.

   Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi(kulia) akikagua gwaride hilo.


 Baadhi ya watumishi wa Mahakama pamoja na wageni waalikwa wakiwa katika sherehe hiyo.Shehe Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Alhadj Mussa Salum akiomba sala maalumu kwa ajili ya sherehe hiyo.

         Wanafunzi kutoka shule ya Msingi Lioness Mibulani wakitoa burudani. 

 Wakili wa Serikali Mkuu Mhe. Mwema Punzi akitoa hotuba kwa niaba ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

    Kiongozi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS)  Kanda ya Mzizima Bi. Tike Mwambipile akitoa hotuba kwa niaba ya Rais wa TLS .

  Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam  Mhe. Amos Makalla akitoa hotuba yake katika sherehe hiyo.

    Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Salma Maghimbi akitoa hotuba yake.

.   Meza kuu ikiwa katika picha ya Pamoja.

  Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi  wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Mojawapo ya Shauri la Usuluhishi likiendeshwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
(Picha na Tumaini Malima- Mahakama)

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni