Alhamisi, 2 Februari 2023

SHAMRA SHAMRA ZATAWALA KILA KONA MAADHIMISHO YA WIKI YA SHERIA

Na Mwandishi wetu-Mahakama, Dodoma

Siku ya Sheria jana tarehe 1 Februari, 2023 imeazimishwa katika maeneo mbalimbali chini huku wananchi wakihimizwa kutatua migogoro yao kwa njia za usuluhishi kabla ya kukimbilia mahakamani, hatua ambayo itachangia ukuaji wa uchumi, amani na kupunguza gharama na mlundikano wa mashauri.

Mwandishi wetu Ahmed Mbilinyi – Mahakama, Bukoba anaripoti kuwa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Bukoba, Mhe. Imakulata Banzi amewasihi wananchi kutumia njia mbadala katika utatuzi wa migogoro ili kutumia muda mwingi katika shunguli za uzalishaji wa kipato.

Akizungumza katika maadhimisho wa Siku ya Sheria, Mhe Banzi alielezea kauli mbiu ya mwaka 2023 inayohusu umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi na kubainisha kuwa ni jambo lisilopingika kwamba huwa hakuna suluhu kama shauli litamalizika kwa njia ya kawaida kwa wadaawa kusikilizwa mahakamani.

“Mmoja kati ya wadaawa hushinda na mwingine kushindwa, hivyo hakuna kutoka suluhu kama ilivyo katika michezo, mfano mpira wa miguu. Matokeo hayo ya mdaawa kushinda na mwingine kushindwa hupelekea chuki na kutokuelewana baina ya pande hizo mbili hasa upande ulioshindwa,” alisema.

Amebainisha faida lukuki zinazopatikana wakati wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi katika kukuza uchumi endelevu zikiwemo, kimarisha undugu na mshikamano katika jamii na kuongeza mshikamano katika jamii kwa pande zilizokuwa zinahasimiana kwa muda marefu.

“Utatuzi wa migogoro kwa njia ya kawaida huchelewesha kesi kumalizika kutokana na wingi wa mashauri, lakinmi njia ya usuluhishi huwezesha migogoro kumalizika mapema kati ya pande mbili na kuepusha Mahakama kulazimika kutumia taratibu za kiufundi ambazo husababisha gharama kubwa,” alisema.

Mhe. Banzi alibainisha kuwa njia ya usuluhishi husaidia pande zote kufikia muafaka kwa haraka na kumpa mdaawa nafasi ya kufanya kazi na kuinua uchumi wake na uchumi wa nchi kwa ujumla, huokoa gharama za uendeshaji wa mashauri na kupunguza mlundikano mahakamani.

 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Bukoba, Mhe. Imakulata Banzi akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria.
Mgeni Mwalikwa, Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Mhe Albert Chalamila akisalimia wananchi katika sherehe hizo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Bukoba, Mhe Immaculata Banzi akikagua gwaride katika maadhimisho hayo.
Mahakimu pamoja na Mawakili wa Serikali na wale wa Kujitegemea wakifuatilia matukio wakati wa maadhimisho hayo.

Kwaya ya Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba wakitoa burudani ya wimbo wa matumizi bora ya Tehama mahakamani ili kuboresha huduma.

Kutoka Mahakama Mara, Kandana Lucas anaripoti kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya amewaasa wananchi wa Mkoa huo kutumia njia ya usuluhishi ili kumaliza migogoro mbalimbali ya muda mrefu, hasa ya ardhi na ndoa, inayopelekea watu kutumia muda mwingi kwenda mahakamani kufuatilia mashauri yao huku wakiacha shughuli zao muhimu za uzalishaji mali.

 “Utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi ni mwarobaini wa migogoro yote, na basi la usuluhishi ni usafiri sahihi kuliko basi la migogoro,” alisema. Kadhalika. Jaji Mtulya ametoa rai kwa wadau wa Mahakama hasa, Mawakili wa Kujitegemea kuwa tayari na kuwashauri wateja wao kufikia suluhu kwani upatanishi au suluhu ni maelekezo ya Mungu kwa dini zote na kwamba kupitia upatanishi kazi hufanyika kwa amani na maendeleo hupatikana.

Kwa upande wake, mgeni wa heshima, Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Mhe. Moses Kaegele ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mara kutoa salamu za serikali, alihimiza umma kutumia usuluhishi ili kupunguza uwezekano wa visasi na uadui unaoweza kusababisha makosa ya jinai kutendeka.

Katika hafla hiyo, Mwanasheria wa Serikali na Chama cha Mawakili Tanganyika walipata nafasi ya kutoa salamu ambapo wameiasa jamii kubadili fikra ili njia ya usuluhishi iweze kutumika kutatua migogoro kwani lengo la kufanya hivyo ni kuimarisha upendo. Vilevile viongozi hao walitoa rai kwa maafisa wote wa Mahakama kutokuwa chanzo cha ugumu wa kutatua migogoro kwa njia ya suluhu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya akisisitiza jambo kwenye maadhimishio ya Siku ya Sheria.

Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Mhe. Moses Kaegele ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mara akitoa salamu za serikali.

Naye Catherine Francis wa Mahakama Kuu- Songea anaripoti kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina ametoa rai kwa wadau wote wa Mahakama kuendelea kuelimisha jamii kwa usahihi juu ya matumizi ya usuluhishi katika kutatua migogoro kabla haijafikishwa mahakamani ili kuendelea na utaratibu wa kawaida wa usikilizai wa mashauri.

Alisema kuwa mbali na umuhimu wa kutumia njia ya usuluhishi katika kutatua migogoro, Mhe. Mlyambina aliainisha baadhi ya changamoto wanazokutana nazo Mahakama wakati wa usuluhishi ambapo mara nyingi wamekuwa wakitumwa wawakilishi wa taasisi au kampuni ambao siyo wasemaji wa mwisho, jambo ambalo linapelekea usuluhishi kuahirishwa na kuchukua muda mrefu.

Alishauri inapotokea jambo kama hilo wakafika wasemaji wa mwisho kwa pande zote mbili za wadaawa ili kuweza kuokoa muda. Mbali na hilo, Jaji Mfawidhi huyo alisema kuwa changamoto nyingine ni mazingira ya kufanyia usuluhishi siyo rafiki.

Amefafanua kuwa baadhi ya wadaawa hawavutiwi kwa kuwa mazingira yanayotumika ni yaleyale ambayo huendeshea mashauri ya kila siku, hivyo jamii inapaswa kukubaliana na changamoto hiyo iliyopo na kuendelea kufanya usuluhishi.

Mhe. Mlyambina alinukuu usemi wa aliyekuwa mshauri wa masuala ya kiutawala na mwandishi wa vitabu Peter Drucker usemao, “Jambo muhimu Zaidi katika mawasiliano ni kusikia kile ambacho hakijasemwa”.

Alisema kuwa katika usuluhishi wadaawa wanapojadiliana juu ya mgogoro wao ni rahisi kugundua kile ambacho hakikusemwa na pengine ndiyo sababu ya mgogoro wao, tofauti na kwenye taratibu za kawaida ambapo Mahakama hujikita katika yale yaliyoainishwa.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina akikagua gwaride maalumu lililoandaliwa kwa heshima yake.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina akifafanua kauli mbiu ya Siku ya Sheria.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. Dkt.Yose Mlyambina (mwenye joho) akiwa pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mhe. Kanali Labani Thomas (mwenye kaunda suti) wakipokea maandamano ya sherehe ya Siku ya Sheria nchini.

Watumishi na wadau wa Mahakama wakiandamana kuelekea viwanja vya Mahakama Kuu Songea kusherehekea Siku ya Sheria nchini.

Kutoka Mahakama Mbeya, Ibrahim Mgallah anaripoti kuwa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya leo tarehe 01 Februari 2023 imefanya maadhimisho ya siku ya sheria nchini kwa mwaka 2023.  Sherehe za maadhimisho hayo zimefanyika katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Mbeya. Siku ya sheria huadhimishwa kila mwaka kuashiria kuanza rasmi kwa shughuli za Mahakama. Katika sherehe hizo

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe.Rose Ebrahim ambaye alikuwa mgeni rasmi amewashauri wananchi kutumia usuluhishi kama nyenzo muhimu ya utatuzi wa migogoro nje ya taratibu za kisheria za kimahakama ili kuokoa muda na gharama.

“Iwapo watu wengi wataamua kumaliza migogoro yao kwa njia za usuluhishi ni wazi zitasaidia Mahakama kupunguza mashauri ya mlundikano yaliyokaa kwa muda mrefu na zitapunguza muda na gharama zitakazotumika katika kusikiliza mashauri hayo. Badala yake muda huo utatumika katika uzalishaji jambo litakalopelekea kuchochea ukuaji wa uchumi na kuvutia uwekezaji,” alisema.

Akitoa salamu zake, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Juma Homera ambaye alikuwa mgeni wa heshima ameipongeza Mahakama Kanda ya Mbeya kwa kazi nzuri inayofanyika ya kusikiliza na kuamua mashauri kwa wakati.

Kdhalika, ameishauri Mahakama iendelee na utoaji wa elimu ya sheria kwa wananchi ili kuwajengea uelewa zaidi wa masuala ya kisheria. “Ninakupongeza Jaji Mfawidhi, Mahakimu na timu yako yote kwa kazi kubwa ya kushughulikia mashauri kwa wakati,” alisema.

Baada ya hafla hiyo, wadau na viongozi mbalimbali walialikwa kusikiliza shauri la uzinduzi lililofanyika katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Mbeya.

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe.Juma Homera akitoa salamu zake katika maadhimisho ya Siku ya sheria nchini.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Rose Ebrahim  akitoa hotuba yake katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Rose Ebrahim akikagua gwaride la heshima katika maadhimisho ya Siku ya sheria nchini.

Naye Eunice Lugiana kutoka Mahakama-Kibaha anaripoti kuwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge ameiomba Mahakama ya Tanzania kuendelea kuwaelimisha wananchi kuhusu usuluhishi bila kuhesabu gharama kwa vile njia hiyo katika kutatua migogoro ina faida nyingi.

Amemshukuru Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma kwa kuanza mchakato wa ujenzi wa Mahakama Kuu katika Mkoa wake, hatua itakayowezesha upatikanaji wa haki kwa urahisi. Amesema ujenzi huo pia utapamba Mji wa Kibaha kwakuwa jengo hilo ni la ghorifa.

Akimkaribisha Mkuu wa Mkoa kuzungumza na wananchi, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Mhe. Nickson John alifurahishwa na Mahakama ya Tanzani kuja na Kauli Mbiu ya mwaka 2023 kuhusu utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi na kubainisha kuwa imekuja muda muafaka ambapo migogoro mingi ya Mkoa wa Pwani ianzie kwenye usuluhishi.

Naye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Kibaha, Mhe. Joyce Mkhoi, akizungumza katika maadhimishi ya Siku ya Sheria alisema kukosa wataalamu wa usuluhishi katika Mahakama kunasababisha mashauri mengi kutatuliwa kwa njia ya kawaida ya kusikiliza baada ya kushindwa kufikia makubaliano kwa vile Wasuluhishi waliopo hawana mbinu za usuluhishi.

Ameomba mafunzo yafanyike kwa maafisa wa Mahakama ili mashauri yaishie kwenye usuluhishi.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge akihutubia katika sherehe za Siku Yya Sheria nchini iliyofanyika katika Viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha Pwani.
Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha Pwani, Mhe. Joyce Mkhoi akihutubia katika sherehe za Siku ya Sheria.

Maandamano ya watumishi wa Mahakama na wadau wa Mahakama yaliyoanzia viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Mailimoja na kuhitimishwa katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha.

Kwa upande wake, Charles Philipo Ngusa anaripoti kutoka Mahakama Geita kuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, Mhe. Cleofas Waane amesema lengo la kauli mbiu ya mwaka huu 2023 ni kuwakumbusha wananchi juu ya umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi bila kufikisha mashauri yao mahakamani.

Amesema kauli mbiu hiyo inawakumbusha wadau wote na wananchi kwa ujumla kuwa tayari kwa ajili ya usuluhishi na kuondokana na dhana ya kumaliza migogoro yao mahakamani.

Aidha amesisitiza kuwa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi unasaidia upatikanaji wa haki kwa wakati na kwa gharama nafuu zaidi, hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi kwa kasi zaidi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela, ambaye alikuwa mgeni rasmi aliipongeza Mahakama kwa kupanua wigo wa utoaji wa elimu ya kisheria ili kuwafikia wadau wengi zaidi, ikiwemo kutumia vyombo vya habari kama redio.

Mkuu wa Mkoa ameomba kuwa elimu hiyo isiishie katika kipindi cha Wiki ya Sheria bali uongozi wa Mahakama uweke utaratibu wakati wateja wakiwa wanasubiri kuingia mahakamani waendelee kupewa elimu hiyo.

Aidha amevishauri vyombo vinavyohusika na usuluhishi kama vile Mawakili kuweka utaratibu wa kujipima ili hadi kufikia mwakani waje na takwimu zinazoonesha walitatua migogoro mingapi bila kufika mahakamani.

Katika hafla hiyo hotuba mbalimbali ziliwasilishwa kutoka katika taasisi kadhaa zenye maudhui ya Siku ya Sheriam zikiwemo ofisi ya taifa ya mashtaka na Mawakili wa Kujitegemea.

Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela akiwasilisha hotuba yake katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.
Watumishi na wadau mbalimbali wakisikiliza hotuba mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa katika hafla hiyo.
Hakimu Mkazi Mfawidhai wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, Mhe. Cleofas Waane akiwasilisha hotuba yake.

 Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi kwenye jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita ambapo ndipo maazimisho haya yalifanyika.

 (Habari hizi zimekusanywa na kuhaririwa  na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni