Ijumaa, 10 Machi 2023

MAFUNZO KUHUSU MFUMO WA SEMA NA MAHAKAMA YAHITIMISHWA

·Jaji Chaba ahimiza utekelezaji bora, ufanisi wa mfumo makazini 

·Aonya uzembe, ulevi, utovu wa nidhamu

Na Faustine Kapama`– Mahakama, Morogoro

Mafunzo ya siku tano yaliyokuwa yanafanyika mjini hapa, kuhusu mfumo mpya wa kielekroniki (e-complaint) wa Sema na Mahakama unaotumika kutoa na kupokea maoni, maulizo na malalamiko (mrejesho) kutoka kwa wananchi, yamehitimishwa leo tarehe 10 Machi, 2023.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messeka Chaba alihitimisha mafunzo hayo yaliyokuwa yanatolewa kwa Naibu Wasajili, Watendaji, Maafisa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na watumishi wengine wanaojihusisha na kupokea malalamiko kutoka Kanda zote za Mahakama nchini kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda hiyo, Mhe. Paul Ngwembe.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Chaba alielezea matarajio yake kuwa mafunzo hayo yamewawezesha kuutumia vema mfumo huo na kutoa huduma bora zaidi kwa wateja kwa kuzingatia matumizi sahihi ya muda, kwa maana ya kuyashughulikia malalamiko kwa wakati na kuhakikisha changamoto binafsi kama uzembe, ulevi, utovu wa nidhamu katika kuwajibika haziathiri utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Kuweni waalimu wazuri na mahili kwa wenzenu ambao hawajapata fursa ya kuhudhuria mafunzo haya na hasa mzingatie kuwa moja ya malengo ya mafunzo haya ni pamoja na kupata wakufunzi kwa watumishi wengine wa Mahakama ya Tanzania,” alisisitiza.

Amesema kuwa anafahamu maafisa TEHAMA ndio wenye jukumu kubwa la kwenda katika Kanda zao kuhakikisha mfumo unaanza kufanya kazi na wanawafundisha vizuri watakaokuwa wanautumia.

“Niwaombe mtakapokwenda katika vituo vyenu mkawe mstari wa mbele kuhakikisha mfumo wa kisasa wa kielektoniki wa Sema na Mahakama unafanya kazi kwa ufanisi kwa kuzingatia viwango vinavyokubalika,” alisema.

Akiwasilisha neno la shukrani kwa niaba ya washiriki wenzake, Bi.Catherine Francis kutoka Mahakama Kuu Songea aliushukuru uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kuandaa mafunzo hayo ambayo yamewawezesha kupata maarifa kwenye maeneo muhimu katika muktadha mzima wa utoaji haki, hususan mfumo wa Sema na Mahakama. Ameahidi kwa niaba ya wenzake kwenda kueneza elimu waliyoipata kwa watumishi wenzao katika vituo vyao vya kazi.

Kabla ya kuhitimishwa mafunzo hayo, washiriki walipitishwa kwa mara nyingine na Afisa kutoka Kurugenzi ya TEHAMA, Bw. Lazaro Sanga namna mfumo wa Sema na Mahakama unavyofanya kazi kabla ya kupokea “dozi” nyingine kutoka kwa Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Jumanne Muna.

Akiwasilisha mada kuhusu mbinu za ufundushaji Bw. Muna aliwaeleza kuwa watakapoenda kwenye vituo vyao watahitajika kuwafundisha watumishi wenzao ili wajue jinsi mfumo wa Sema na Mahakama unavyofanya kazi, hivyo wanapaswa kujua nini wanachokifundisha na namna ya kufikisha ujumbe unaotakiwa.

“Tunafanya hivi kwa lengo mahususi ya kuandaa wakufunzi watakaopeleka elimu waliyoipata kwa watumishi ambao ni wengi zaidi. Tukifuata utaratibu huu tutaweza kutumia fedha kidogo,” alisema na kuwakumbusha washiriki hao kuwa wanapaswa kutumia mbinu mbalimbali za kufundisha kulingana na mazingira.

Amesema kuwa utoaji wa mafunzo kwa wafanyakazi ni sehemu muhimu ya ukuaji na mafanikio katika taasisi kwani watumishi waliofunzwa vyema wana tija na huleta ufanisi zaidi katika majukumu yao, hivyo kutoa mchango mkubwa.

Afisa Utumishi huyo alibainisha kuwa aina tofauti za mbinu za ufundishaji huja na faida, changamoto na malengo tofauti.

“Kuna aina tofauti ya kujifunza kulingana na watu tofauti, kuna wale wanaoelewa polepole, wengine wanahitaji sauti ya juu na wengine wanahitaji mwalimu wa kuwaongoza. Ili wale mnaowafundisha waweze kukuelewa mnahitaji kuelewa mbinu ya kutumia kuwafundisha,” alisema.

Mahakama ya Tanzania imeanzisha mfumo mpya wa Sema na Mahakama ili kurahisisha njia za uwasilishaji wa maoni na kuongeza uwazi katika kushughulikia maoni, malalamiko na kuweza kukusanya taarifa sahihi kutoka kwa wananchi na wadau.

Mfumo huo ambao haujajengwa kwa ajili ya kupokea malalamiko pekee, bali pia mwananchi ana uhuru wa kutoa maoni, mrejesho, mapendekezo au pongezi umeletwa ili kuimarisha mawasiliano kati ya Mahakama na mwananchi kuhusu huduma zinazotolewa katika mchakato mzima wa utoaji haki.

Kwa kupitia mfumo huu, ambao umekamilika kwa asilimia 98 na unaweza kuanza kutumika, mwananchi anaweza kuwasilisha maoni, malalamiko au pongezi kwa Mahakama aidha kwa kutumia simu yake mwenyewe, kwa kuandika ujumbe mfupi au kwa kupiga na anaweza kwenda kwenye mfumo wenyewe kwa kupitia kompyuta yake au njia ya e-mail na kuliwasilisha.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba  akizungumza na washiriki wakati wa kufunga mafunzo ya mfumo wa Sema na Mahakama leo tarehe 10 Machi, 2023 katika Ukumbi wa Magadu mkoani Morogoro.


Naibu Msajili kutoka Idara ya Usimamizi na Ukaguzi wa Shughuli za Kimahakama na Maadili, Mhe. Kinabo Minja akimkaribisha Jaji Chaba kuhitimisha mafunzo hayo

Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Jumanne Muna akisisisitiza jambo alipokuwa anawasilisha mada kwa washiriki kabla ya mafunzo hayo kuhitimishwa.


Mwashiriki kutoka Mahakama Kuu Songea, Bi.Catherine Francis akitoa shukrani kwa niaba ya washiriki wenzake.

Afisa kutoka Kurugenzi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Bw. Lazaro Sanga akiwapitisha washiriki wa mafunzo namna mfumo wa Sema na Mahakama unavyofanya kazi.
Sehemu ya washiriki wa mafunzo (juu na chini) ikifuatilia uwasilishaji wa mada mbalimbali.

Sehemu nyingine ya washiriki wa mafunzo (juu na chini) ikifuatilia uwasilishaji wa mada mbalimbali.

Wajumbe wa Sekretarieti waliokuwa wanaratibu mafunzo hayo wakikamilisha kazi za mwisho mwisho.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba (katikati). Wengine ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Morogoro, Mhe. Augustina Mmbando (kulia) na Naibu Wasajili na Watendaji kutoka Kanda zote za Mahakama hapa nchini, Naibu Msajili kutoka Idara ya Usimamizi na Ukaguzi wa Shughuli za Kimahakama na Maadili, Mhe. Kinabo Minja.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo (juu na chini) wakikabidhiwa vyeti na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messeka Chaba.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni