Alhamisi, 9 Machi 2023

MFUMO WA SEMA NA MAHAKAMA UPO TAYARI KUTUMIKA

·Afisa TEHAMA auchambua namna unavyofanya kazi

Na Faustine Kapama`– Mahakama, Morogoro

Mfumo wa Sema na Mahakama ambao ni mpya wa kielekroniki (e-complaint) wa kutoa na kupokea maoni, maulizo na malalamiko au mrejesho kutoka kwa wananchi umekamilika na upo tayari kuanza kutumika.

Hayo yamebainishwa na afisa kutoka Kurugenzi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Bw. Lazaro Sanga alipokuwa anawasilisha mada kuhusu mfumo huo unavyofanya kazi kwenye mafunzo yanayofanyika mjini hapa yakijumuisha maafisa wenzake waliotoka Kanda zote za Mahakama ya Tanzania.

“Mfumo huu umekamilika kwa asilimia 98 na unaweza kuanza kutumika. Tayari baadhi ya viongozi wameanza kupokea ujumbe mfupi kutoka kwa wananchi. Mfumo huu haujajengwa kwa ajili ya kupokea malalamiko pekee, bali pia mwananchi ana uhuru wa kutoa maoni, mrejesho, mapendekezo au pongezi,”alisema.

Amewaambia maafisa TEHAMA wenzake wanaoshiriki mafunzo hayo, ambayo yameingia siku ya nne, kuwa ili mwananchi aweze kutuma lalamiko, pendekezo au maulizo anatakiwa kuwa na simu ya mkononi (smartphone), kompyuta au kishikwambi (tablet).

Bw. Sanga alieleza kuwa mfumo huo unamwezesha mwananchi kutuma lalamiko wakati wowote na mahali popote ila tu anatakiwa kuwa na mtandao mzuri na humwezesha kutuma lalamiko lake kwa njia ya msimbo kwa kubonyeza *152*00#.

“Mfumo unaruhusu mwananchi kufungua akaunti ya Sema na Mahakama, anachotakiwa ni kujaza taarifa zake kwa usahihi ili aweze kupata mrejesho wa pale anapotuma lalamiko lake. Mfumo pia unatoa nafasi ya kutuma lalamiko bila kujulika. Ili uweze kupata mfumo anatakiwa kubonyeza https://sema.judiciary.go.tz,” alieleza.

Alitaja njia mbili ambazo zinaweza kutumiwa na mwananchi kujua lalamiko lake kama limepokelewa na kujibiwa au la. Njia hizo ni kwa kutumiwa ujumbe mfupi kupitia simu yake ya mkononi endapo alitumia akaunti yake ya Sema na Mahakama au alijaza taarifa zake pia kwa kutumia namba ya kitambulisho ya lalamiko kupitia tovuti ya Sema na Mahakama, Mobile App au Msimbo.

Kwa mujibu wa Afisa TEHAMA huyo, mfumo umegawanyika katika sehemu mbili ambazo ni sehemu ya wananchi kutuma malalamiko bila kujulikana, kutuma malalamiko kwa kuweka taarifa na kwa kufungua akaunti. Amesema sehemu ya pili ni kwa watumishi wanayoitumia kujibu malalamiko na mapendekezo ya wananchi.

Jana jioni tarehe 8 Machi, 2023, washiriki hao wa mafunzo walipitishwa kwenye mada inayohusu mabadiliko na jinsi ya kutawala mabadiliko yanayotokea ndani na nje ya mtu. Mada hiyo iliwasilishwa na Mhadhiri huru wa Vyuo vya Mafunzo ya Utawala Afrika Mashariki na Kusini, ambaye pia ni Mshauri Mtaalam Binafsi, Dkt. Endrew Msami.

Akiwasilisha mada hiyo, Dkt. Msami aliwashauri maafisa TEHAMA hao kwenda na mabadiliko kulingana na Mahakama ya Tanzania ilivyobadilika, kwani kwa kufanya hivyo wataweza kufanikisha malengo ya taasisi wanayoitumikia, hivyo kutoa huduma bora kwa jamii inayowazunguka.

“Anzeni kutengeneza mabadiliko ndani yenu ili mabadiliko ya nje yaweze kuleta matunda mazuri kupitia utendaji wenu wa kazi. Badilikeni ili muendelee kuwa watu bora kila siku, unapobadilika ili iwe mtu bora leo unatakiwa na kesho ubadilike ili uendelee kuwa mtu bora kesho kutwa,” alieleza.

Amewakumbusha washiriki hao wa mafunzo kuwa Mahakama ya Tanzania siyo ya jana kutokana na mabadiliko makubwa ambayo imeyafanya katika kuhakikisha jukumu lake kuu la utoaji haki linaendelea kutekelezwa kwa ufanisi unaotakiwa, hivyo na wao wanatakiwa kwenda na mabadiliko hayo ili wasiachwe nyuma.

Mfumo wa Sema na Mahakama wa kielekroniki (e-complaint) wa kutoa na kupokea maoni, maulizo na malalamiko au mrejesho kutoka kwa wananchi unavyoonekana (juu na chini) kwa sasa.

Afisa kutoka Kurugenzi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Bw. Lazaro Sanga akieleza jinsi mfumo huo unavyofanya kazi.

Mhadhiri huru wa Vyuo vya Mafunzo ya Utawala Afrika Mashariki na Kusini, ambaye pia ni Mshauri Mtaalam Binafsi, Dkt. Endrew Msami akiwasilisha mada kuhusu mabadiliko kwenye mafunzo ya maafisa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania.
Sehemu ya maafisa TEHAMA na watumishi wengine wanaohusika na kupokea malalamiko, mrejesho, maoni na mapendekezo kutoka kwa wananchi (juu na chini) wanaoshiriki mafunzo hayo.

Sehemu nyingine ya maafisa TEHAMA na watumishi wengine wanaohusika na kupokea malalamiko, mrejesho, maoni na mapendekezo kutoka kwa wananchi (juu na chini) wanaoshiriki mafunzo hayo.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni