Alhamisi, 4 Mei 2023

JAJI MFAWIDHI MWANZA AHIMIZA UTUMISHI KADA ZAIDI YA MOJA

Na Stephen Kapiga-Mahakama, Mwanza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. Dkt. Ntemi Kelekamajenga amewahimiza watumishi katika Kanda hiyo kufanya kazi katika kada zaidi ya moja, hatua itakayosaidia kupambana na upungufu wa rasilimali watu sehemu za kazi.

Mhe. Kelekamajenga alitoa wito huo jana tarehe 3 Mei, 2023 alipokuwa anaendesha kikao cha menejimenti ya Mahakama katika Kanda hiyo inayojumuisha Mikoa ya Mwanza na Geita katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mwanza.

“Tatizo la uhaba wa watumishi ni kilio kwa kila Mahakama zilizowasilisha taarifa zao za utendaji na kuonesha changamoto ya upungufu wa watumishi, hivyo mkifanya kazi zaidi ya moja kutasaidia kupambana na tatizo hili badala ya kuegemea kwenye kada moja tu,” alisema.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi aliwahimiza wajumbe wa kikao hicho kujitahidi kila wakati kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA katika kazi zao za kila siku kwani kwa sasa ndipo Mahakama inapoelekea kwenye Mahakama Mtandao.

Mhe. Dkt. Kelekamajenga pia alizungumzia suala la motisha kwa watumishi. Aliwaomba wajumbe hao wa menejimenti kama viongozi kwenye maeneo yao kutoa motisha kwa watumishi waliochini yao, hatua itakayoongeza morali ya kufanya kazi.

“Napenda pia muone umuhimu wa kutoa motisha kwa watumishi ambao wapo chini yenu ili kuweza kuwajengea morali ya kazi. Kuna aina nyingi za motisha kama ambavyo wenzetu wa Ukerewe katika taarifa zao wameonesha namna walivyoweza kutembelea mbuga za wanyama za Serengeti na Ngorongoro, hii inaweza kuinua molari ya watumishi katika maeneo yenu,” alieleza.

Katika hatua hatua nyingine, Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza imebuni fomu laini maalumu itakayokuwa inatumika kurejesha taarifa ya huduma anayopatiwa mteja katika Mahakama hiyo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza, Mhe. Monica Ndyekobora aliwaeleza wajumbe wa kikao hicho namna fomu hiyo itakavo fanya kazi.

“Fomu hii tumeipa jina la “please rate me” ambayo mteja atatoa mrejesho wa huduma aliyopewa na mtumishi na kuweza kuonesha kama ameridhishwa na huduma au la na nini ushauri wake juu ya mtumishi aliyempatia huduma hiyo,” alisema.

Mhe. Ndyekobora alifafanua kuwa wanategemea kuanza kuutumia mfumo huo watakaponunua kishikwambi ambacho kitakuwa katika dirisha la kutolea huduma ndani ya Mahakama hiyo.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. Dkt. Ntemi Kelekamajenga(katikati) akieleza jambo kwa wajumbe wa kikao cha menejimenti kilichofanyika jana tarehe 3 Mei 2023 kwenye ukumbi wa mikutano katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mwanza. Kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Mhe. Chiganga Mashauri na kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Mwanza Bw. Tutubi Mangazini.

 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza, Mhe. Chiganga Mashauri akieleza jambo wakati wa uchangiaji wa mawasilisho ya taarifa za utendaji kazi kutoka katika Mahakama mbalimbali za Kanda hiyo.

 

Sehemu ya wajumbe wa kikao cha Menejimenti Mahakama Kanda ya Mwanza (juu na picha mbili chini) wakifuatilia kwa makini mawasilisho ya taarifa za utendaji kazi kutoka katika vituo mbalimbali vya Mahakama zilizopo katika Mikoa ya Geita na Mwanza.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni