Alhamisi, 4 Mei 2023

MAJAJI WATATU WA MAHAKAMA KUU WALIOAGWA WATOA USHAURI MUHIMU

Na Magreth Kinabo- Mahakama

Majaji watatu wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 4 Mei, 2023 wameaagwa kitaaluma baada ya kustaafu utumishi wa Umma kwa kujibu wa sheria, huku wakisisitiza watumishi wa Mahakama kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano, weledi, uadilifu na upendo ili kuweza kutekeleza jukumu la utoaji haki na kulinda uhuru wa Mahakama.

Majaji hao ambao wamestaafu waliotoa kauli hizo kwa nyakati tofauti ni Mhe. Beatrice Mutungi, Mhe. John Mgeta na Mhe. Sekela Moshi. Kwa pamoja wameishukuru Mahakama kwa ushirikiano walioupata katika utumishi wao na kuiacha Mahakama katika mikono salama.

Aidha, Majaji hao waliasa   kwamba jukumu la utoaji haki linahitaji uvumilifu na muda wa kujitolea kwa kiwango cha juu.

Kwa upande wake, Jaji Mutungi, ambaye amekuwa mtumishi kwa Mahakama kwa miaka 33 amehudumu katika ngazi mbalimbali, ikiwemo Hakimu Mkazi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania katika Kanda tofauti, zikiwemo Songea, Moshi na Dar es Salaaam.

Alisema mbali na kufanya kazi kwa kuzingatia mambo mbalimbali, uwezo wa kutoa hukumu na maamuzi mbalimbali umechangiwa na kuwa chini ya viongozi waelekezi na kupata mafunzo ya kitaaluma ndani na nje ya nchi.

“Haki isitendeke tu bali ionekane wazi na bila shaka inatendeka. Maana ya msemo huu ilinipasa kusikiliza kwa umakini ushahidi wote ulioletwa na pande zote katika mashauri, kusoma na kufanya utafiti ili niweze kufikia maamuzi yasiyokuwa na upendeleo. Rai yangu kulingana na ukuaji wa sayansi na teknolojia mambo mengi yanabadilika. Hapa nalenga kuwaasa kuwa Mahakama Mtandao ipewe kipaumbele,” alisema na kusisitiza watumishi kupatiwa semina na mafunzo.

Akimzungumzia Jaji Mutungi, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Juliana Masabo alisema anastahili kuigwa kwa uongozi wake mahiri, kuimarisha maadili ya watumishi na kuwasaidia watumishi na wadau katika kutatua malalamiko.

Kwa upande wake, Jaji Moshi ambaye amehudumu katika Mahakama kwa muda wa miaka 33 aliwasisitiza Mawakili wa Serikali na wale wa kujtegemea kuzingatia  shajara zao ili kuepusha mashauri mengi kwa wakati mmoja. Kadhalika, aliwaasa Mahakimu na Majaji kufanya ukaguzi katika masjala za Mahakama. Aliongeza kuwa kazi ya ujaji ni ngumu inahitaji muda wa ziada ya saa za kazi.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masajala Kuu, Mhe. Leila Mgonya, akimzungumzia Jaji Moshi alisema atakumbukwa kwa uongozi mahiri na mwepesi wa kuchukua hatua, usimamizi wa rasilimali watu, maono na ubunifu.

Naye Jaji Mgetta ambaye amehudumu katika Mahakama kwa kipindi cha miaka 32 ameshika nafasi mbalimbali kutoka Hakimu Mkazi na kuendelea kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu. Alipata kozi mbalimbali fupi ndani na nje ya nchi ambazo zilimsaidia kupata uzoefu, ikiwemo kuongeza thamani katika kazi yake.

“Ni muhimu kuzingatia utawala wa sheria na wakati huo huo unasimamia haki za wananchi kwa mantiki hiyo kunahitajika uharaka katika kutoa maamuzi na umakini wa ziada katika maudhui ya maamuzi hayo kwa kuhakikisha yanakuwa sahihi,” alisema.

Jaji Mgetta alisema mabadiliko ya sayansi na teknolojia yatumike vizuri ili kuhakikisha muda wa kusikiliza mashauri unapungua na imani ya wananchi juu ya Mahakama inaongezeka.

Akimzunguzia Jaji Mgetta, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Moses Mzuna alisena ni jasiri, alilinda taswira ya taaluma, mwanadiplomasia, mkweli, myenyenyekevu na mwenye bidii,

Mwakilishi wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ambaye ni Wakili Mkuu wa Serikali, Bw. Mark Mulambo alisema Majaji hao wana mchango mkubwa katika tasnia ya sheria kutokana na maamuzi waliyoyatoa.

Makamu wa Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Gloria Kalabamu aliwapongeza Majaji hao na kuahidi kuwa TLS itaendelea kushiriana nao katika kupata  ushauri, usaidizi katika tafiti na uzoefu.

Mhe. Sekela Moshi.
 Mhe. John Mgeta.
Mhe. Beatrice Mutungi.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (wa pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji watatu ambao leo wameagwa kitaaluma baada ya kustaafu utumishi wa umma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji watatu ambao leo wameagwa kitaaluma baada ya kustaafu (waliokaa kulia kwake) na Majaji wengine ambao bado wanaendelea na utumishi wa umma.

                              (PICHA NA INNOCENT KANSHA-MAHAKAMA)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni