Jumamosi, 30 Septemba 2023

JAJI EBRAHIM AFANYA UKAGUZI GEREZA LA WILAYA YA LINDI

Na. Hilary Lorry – Mahakama Lindi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe.Rose Ebrahim hivi karibuni amefanya ziara ya kikazi katika gereza la Wilaya ya Lindi.

Akizungumza na mahabusu na wafungwa katika gereza hilo Wilaya ya Lindi Mhe. Ebrahim aliwataka wafungwa na mahabusu watakapo toka gerezani hapo kuwa mabalozi wazuri wakupinga vitendo viovu pindi watakaporudi uraiani. Vilevile aliwaasa vijana kutumia muda wao mwingi vizuri katika kujikita katika shughuli za kuichumi na siyo kutenda mambo maovu.

“Nasikitika sana kusema Kanda hii ya Mtwara imekuwa na kasumba ya matukio mengi ya ukatili wa kijinsia hasa matukio ya ubakaji hii inafanya taifa kupoteza nguvu kazi, hivyo nawaomba  kama Mama na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda hii mtakapo toka hapa gerezani mkawe mabalozi wazuri wakupinga matendo maovu”, aliongeza Jaji Ebrahim.

Mhe. Ebrahim aliendelea kwa kutoa pongezi kwa Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Lindi pamoja na watumishi wenzake kwa juhudi kubwa za kuwahudumia wateja wao ambao ni wafungwa na mahabusu katika gereza hilo. vilevile aliwapongeza  kwa jitihada wanazofanya katika kuhakikisha gereza la  Wilaya ya Lindi linakaa katika hali ya usafi muda wote.

Jaji Ebrahim aliwataka Mahakimu wa ngazi zote kuendelea kusaidiana kwa karibu na timu ya haki jinai kuendesha mashauri kwa haraka ili kuepusha mashauri ya mlundikano (backlog cases). Aidha aliwapongeza Mahakimu wa Mkoa wa Lindi kwa kutozalisha mashauri ya mlundikano na kwa jitihada za kutoa nakala za hukumu na mienendo ya mashauri kwa wakati.

“Nafahamu Mkoa wa Lindi hauna mashauri mengi ya muda mrefu, naomba jitihada zilizopo ziboreshwe ili tusizalisha mashauri ya muda mrefu (backlog cases) ikiwa ni pamoja na kutoa nakala za hukumu na mienendo ya mashauri kwa wakati. Aidha natambua mpango tuliojiwekee kama Kanda na Mkoa wa Lindi wakutoa nakala za hukumu na mwenendo mara tu shauri linapofika tamati naomba mpango huu uendelee kutiliwa mkazo ili tusije kuwakwamisha hawa ndugu zetu wakati wa kukata rufaa” alisema Jaji Ebrahim.

Aidha, wakizungumza kwa nyakati tofauti Mkuu wa Gereza la wilaya ya Lindi ASP.Dominic Byamungu, wafungwa na mahabusu wameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa hatua kubwa waliyoipiga katika masuala ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHEMA) yaani Mahakama Mtandao (video conference) kwakurahisha zoezi la usikilizaji wa mashauri kwa wakati.

“Awali ilikuwa lazima mahabusu, mfungwa au hata shahidi kufika katika mahakamani lakini kutokana na Mahakama kuboresha mifumo ya TEHAMA sasa tunaweza tukawa na mahabusu na wafungwa  mwenye mashauri  ya rufaa Mahakama Kuu, Mahakama ya Rufani au Mahakama yoyote hapa nchini na wakasikilizwa wakiwa  gerezani…,

…hii imepunguza suala la mashauri kuchukua muda mrefu bila kusikilizwa na imepunguza gharama kwa Serikali na Magereza, imerahisisha upatikanaji wa haki kwa wakati na pia imeongezea serikali kipato kwa kulinda nguvu kazi kusafiri umbali mrefu”, alisema Mkuu wa gereza hilo.

Katika ziara hiyo  Jaji Mfawidhi Kanda ya Mtwara aliongozana na  Mahakimu, Viongozi waandamizi wa Mahakama kwa kanda ya Mtwara na Lindi pamoja na  timu ya haki jinai kwa Mkoa wa Lindi.

Ziara ya Jaji Ebrahim ni mwendelezo wa ziara yake katika Kanda ya Mtwara na Mkoa wa Lindi, Ziara yake katika Gereza la Wilaya ya Lindi imelenga zaidi kusikiliza na kuangali namna bora ya kutatua changamoto zinazo wakabili wafungwa na Mahabusu katika gereza hilo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe.Rose Ebrahim (mwenye skafu) akiwa kwenye picha ya pamoja na Maafisa waandamizi wa Gereza Kuu la Wilaya ya Lindi alipofanya ziara ya ukaguzi hivi karibuni.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe.Rose Ebrahim (mwenye skafu kulia) akiwasili  gereza Kuu la Wilaya ya Lindi na kupokelewa na mwenyeji wake Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Lindi  ASP. Dominic Byamungu.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe.Rose Ebrahim (mwenye skafu kulia) akibadilishana mawazo na mwenyeji wake Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Lindi  ASP. Dominic Byamungu  alipowasili  gerezani hapo. 

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe.Rose Ebrahim (mwenye skafu) akiwa katika picha ya Pamoja na Maafisa waandamizi wa magereza pamoja na timu ya Haki jinai Mkoa wa Lindi.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni