Jumatatu, 18 Septemba 2023

JAJI KIONGOZI AFUNGUA MKUTANO KUPITIA RASIMU MTAALA WA SHULE YA SHERIA TANZANIA

Na. Faustine Kapama-Mahakama

Timu ya Wataalam na Baraza la Sheria nchini wanakutana jijini Dar es Salaam kwa siku mbili kuanzia leo tarehe 18 Septemba, 2023 kupitia rasimu ya mtaala wa Shule ya Sheria kwa Vitendo Tanzania (Law School of Tanzania) kwa lengo la kupata mtaala mpya.

Akizungumza wakati anafungua mkutano huo unaofanyika katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani amesema ili taasisi yoyote iweze kupiga hatua ni lazima ifanye maboresho.

“Kuhuisha mtaala wa Shule ya Sheria ni moja kati ya maboresho makubwa ambayo inapaswa kuyafanya ili kuendana na zama tulizonazo. Ninaamini kwamba mtaala ambao umeandaliwa ili kukidhi mahitaji ya sasa utakuwa ni mapinduzi katika uboreshaji wa elimu ya sheria katika nchi yetu,” amesema.

Jaji Kiongozi, ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza la Sheria, amewaomba wajumbe wa mkutano huo kushiriki kikamilifu katika kubadilishana maarifa na mawazo na kuongeza au kuboresha mtaala unaopendekezwa, lengo pekee likiwa kuwa na mchakato wa uthibitishaji wa kujenga na wenye tija.

Amesema Shule ya Sheria kwa Vitendo Tanzania ilianzishwa kupitia Sheria ya Shule ya Sheria Tanzania No.18 ya mwaka 2007 na ilianza kutoa Stashahada ya Juu ya Mafunzo ya Sheria kwa Vitendo mwaka uliofuata na sasa ni zaidi ya miaka kumi ambayo imepita bila kuwa na mapitio ya kina ya mtaala wake.

Mhe. Siyani ameeleza kuwa mtaala uliopo haukidhi mazingira ya sasa ya kijamii na kiuchumi katika mazoezi ya kisheria ambayo yanaashiria mabadiliko makubwa hivi karibuni katika teknolojia ya habari na mawasiliano.

“Shule ya Sheria Tanzania na Mahakama ya Tanzania walidhamiria kwa pamoja kuongoza mageuzi yanayohitajika ili kupunguza pengo na pia kuhakikisha utoaji wa huduma bora za kisheria ambazo ni miongoni mwa malengo makuu ya Mahakama katika kufikia utoaji wa haki kwa wakati,” amesema.

Jaji Kiongozi amesema anafahamu mchakato wa mapitio umepitia hatua mbalimbali kuanzia zoezi la kuwashirikisha wadau na tathmini ya mahitaji ya utekelezaji wa mtaala uliopo, mapitio ya kina ya mtaala wa Shule ya Sheria Tanzania na baadaye uthibitishaji wa rasimu ya mtaala kwa wadau wa ndani na wa nje.

“Nachukua fursa hii kuwapongeza wale wote ambao wamejitolea muda wao na juhudi zao bila kuchoka katika kufanikisha kazi hii muhimu. Ninaamini kutokana na yale niliyoyapata kutoka kwenye rasimu hii, mtaala unatarajiwa kutimiza matarajio ya muda mrefu na yanayosubiriwa na jumuiya ya wataalamu wa sheria kwa ujumla,” amesema.

Awali, akimkaribisha Jaji Kiongozi kufungua mkutano huo, Kaimu Mkuu wa Shule ya Sheria kwa Vitendo Tanzania, Prof. Sisti Mramba alielezea mchakato mzima waliopitia katika kufikia hatua hiyo muhimu ambayo imehusisha ushirikishwaji wa wadau mbalimbali.

“Tulianza na mikutano ya kina ya mashauriano ambayo ilileta pamoja sauti na mitazamo ya watendaji, wasomi, wahitimu, wanafunzi na wanajamii. Ufahamu wao muhimu umekuwa na manufaa katika kutengeneza mtaala wetu,” amesema.

Prof. Mramba amesema pia kuwa rasimu hiyo ilipitiwa kwa kina na wafanyikazi wa ndani ambao utaalam wao na kujitolea kwao kumeonekana katika mchakato wote kwani walifanya kazi bila kuchoka ili kuhakikisha kwamba mtaala unalingana na dhamira na maono ya taasisi yao.

Kaimu Mkuu wa Chuo amesema kulikuwepo pia na mchango uliopokelewa kutoka kwa wadau wa nje ya taasisi ambapo mtazamo unaotokana na uzoefu na utaalamu wao mbalimbali umewapatia uelewa mpana zaidi. Amesema wanathamini wakati na maarifa waliyoyatoa, ambayo yameboresha mchakato wa kutengeneza mtaala huo.

“Hatulengi tu kufikia viwango lakini pia kuweka vigezo vipya vya ubora katika mafunzo. Mtaala tunaowasilisha unawakilisha maono yetu ya pamoja ya siku zijazo, ambapo wanafunzi wetu watapokea elimu iliyokamilika inayowapa ujuzi na maarifa muhimu ili kustawi katika ulimwengu unaoendelea kubadilika,” amesema.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani akizungumza wakati anafungua mkutano wa wataalam na Baraza la Sheria kupitia rasimu ya mtaala wa Shule ya Sheria kwa Vitendo Tanzania. Mkutano huo wa siku mbili unaofanyika katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Dar es Salaam umeanza leo tarehe 18 Septemba, 2023.
Kaimu Mkuu wa Shule ya Sheria kwa Vitendo Tanzania, Prof. Sisti Mramba akieleza mchakato waliopitia katika kufikia rasimu ya mtaala huo.
Katibu wa Baraza la Sheria, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Anold Kirekiano akiwatambulisha baadhi ya wajumbe wa mkutano huo.
Sehemu ya wajumbe wa mkutano (juu na chini) wakifuatilia mambo mbalimbali.

Sehemu ya wajumbe wa mkutano (juu) wakifuatilia mambo mbalimbali. Picha chini ni wajumbe wa Sekretarieti wakiwa kwenye mkutano huo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Baraza la Sheria wanaohudhuria mkutano huo. Wengine waliokaa ni Kaimu Mkuu wa Shule ya Sheria kwa Vitendo Tanzania, Prof. Sisti Mramba (kushoto) na Katibu wa Baraza la Sheria, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Anold Kirekiano (kulia).
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na timu ya wataalam ya kuandaa mtaala huo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wote wa mkutano.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Sekretarieti.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni