Jumamosi, 9 Septemba 2023

JMAT DAR ES SALAAM YAWEKA HISTORIA

·Majaji, Mahakimu wafurika kwenye Bonanza

·Usiwachukulie poa, walichokifanya Gymkhana hatari

·Jaji Maruma kumbe naye yumo

Na Faustine Kapama-Mahakama

Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tawi la Dar-es-Salaam leo tarehe 9 Septemba, 2023 wameshiriki katika Bonanza la Michezo mbalimbali ambalo limefana kwa kiasi kikubwa kinyume na matarajio.

Majaji, Mahakimu na watumishi wengine wa kada mbalimbali wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam walianza kuwasilisha katika Viwanja vya Gymkhana mapema asubuhi ili kushiriki katika Bonanza hilo ambalo ni la kwanza tangu chama hicho kuanzishwe.

Dalili za kuchangamka kwa Bonanza hilo zilianza kuonekana baada ya mgeni rasmi, Jaji na Mlezi wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Augustine Mwarija kuungana na wanachama hao na kuanza pasha-pasha ya hapa na pale kabla ya kwenda kwenye mapumziko mafupi.

Baadaye, washiriki wa Bonanza hilo walijigawa katika makundi ya michezo mbalimbali ambapo kila mmoja alichangamkia nafasi yake, huku Majaji kutoka Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani wakionyesha umahiri mkubwa uliowashangaza wengi.

Michezo waliyoshiriki ni kukimbia mita 100 kwa wanawake na wanaume, kukimbia mita 400 kwa Wanawake na Wanaume, karata, draft, bao, kukimbiza kuku, mpira wa miguu na mpira wa pete, kuvuta kamba na kukimbia kwenye magunia.

Katika mchezo wa kukimbia mita 100 wanawake, Mhe. Barke Sehel wa Mahakama ya Rufani aliwatimulia vumbi wenzie, huku Naibu Msajili Mwandamizi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam, Mhe. Sudi Fimbo akikiwasha kisawasawa. Mshindi wa mbio hizo alikuwa Grace Hamis wa Mahakama Kuu.

Kwa upande wa mbio mita 100 wanaume, Majaji Sam Rumanyika na Zepharine Galeba wa Mahakama ya Rufani na Majaji Edwin Kakolaki, Musa Pomo na Gabriel Malata wa Mahakama Kuu ya Tanzania walitoa upinzani wa kufa mtu. Mshindi wa mbio hizo alikuwa Girshot Gentro kutoka Mahakama Kuu.

Katika mbio za mita 400 wanaume, Majaji wa Mahakama ya Rufani pia hawakuwa nyuma baada ya kuwahenyesha washiriki wengine. Mshindi wa mbio hizo alikuwa Sachore Adolfi kutoka Mahakama ya Rufani, huku upande wa wanawake, Grace Hamis aliibuka mshindi kutokea Mahakama Kuu.

Kwenye mchezo wa kukimbia kwa kutumia magunia, Aziza Mnete wa Mahakama ya Rufani aliibuka mshindi, huku upande wa wanaume, Mhe. Hassan Chuka, pia kutoka Mahakama ya Rufani akichomoza kama mbabe.

Kwa upande wa kukimbiza kuku wanaume, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina alifanikiwa kujinyakulia kitoweo hicho, huku Naibu Msajili Mahakama ya Rufani, Mhe. Sekela Mwaiseje akiibuka mshindi kwa upande wa wanawake.

Katika mchezo wa kuendesha baiskeli, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Sam Rumanyika alifanikiwa kuchanja mbuga kwa upande wa wanaume, huku Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Ilala, Mhe. Suzan Kihawa akiibuka kidedea.

Kuhusu kamba wanawake, Mahakama Kuu waliwakamua kamasi Mahakama ya Rufani na kwa upande wa wanaume Mahakama ya Rufani iliwapigisha chafya Mahakama Kuu. Majaji wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani walishiriki kikamilifu na kuonyesha ukakamavu wa hali ya juu ambao wengi hawakuamini kilichokuwa kinatokea.

Katika mchezo wa bao, kulikuwepo na mechi za utangulizi ambapo Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Jacobs Mwambegele alimgalagaza mtu baada ya kuibuka mshindi, huku Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Division ya Kazi, Jumanne Muna akimsambaratisha jamaa mmoja aliyejaribu kujitutumua.

Mchezo huo katika mashindano ulimuibua Mwanabibi Bakari kutoka Mahakama Kuu, ambaye alimpigisha chafya mshindani wake kutoka Mahakama ya Rufani na kwa upande wa wanaume, Hashim Rashid pia wa Mahakama Kuu aliibuka mshindi.

Katika mchezo wa mpira wa miguu wanaume, Timu ya Mahakama Kuu iliwachapa Mahakama ya Rufani mabao 2:1 kufuatia kabumbu safi iliyoonyeshwa na wachezaji wa timu zote mbili.

Mahakama Kuu walikuwa wa kwanza kuliona lango la wapinzani wao katika dakika ya 30 baada ya mshambuliaji wao hatari kuachia shuti kali lililomshinda kipa wa timu ya Mahakama ya Rufani, Spear Mbwembwe.

Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote mbili kushambuliana kwa zamu. Timu ya Mahakama ya Rufani ilifanikiwa kusawazisha bao dakika ya 20 ya mchezo na ku-‘level score board.’ Dakika chache kabla ya mchezo kumalizika, winga hatari wa timu ya Mahakama Kuu aliukwamisha wavuni mpira na kusababisha mechi hiyo kumalizika kwa timu yake kuibuka wababe.

Katika mchezo wa pete, Mahakama Kuu pia iliwabugiza Mahakama ya Rufani vikapu 25 kwa 11 huku Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Divisheni ya Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma akiibuka kinara wa kutupia vikapu golini. Hii iliwashangaza wengi na kuibua shangwe kila kona wakati alipokuwa anatupia tupia vikapu hivyo.

Mchezo wa ‘draft’ uliowakutanisha wanaume kutoka Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani, ulichezwa kwa ustadi mkubwa, huku mashabiki wa pande zote mbili wakianikiza na kuhamasisha ili wawakilishi waweze kupata ushindi. Hata hivyo, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Issa Maige alifanikiwa kumtoa kijasho chembamba Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Isaya Arufani na kuibuka mshindi.

Katika mchezo wa karata, timu ya Mahakama ya Rufani wanawake imeibabua Mahakama Kuu, huku upande wanaume timu ya Mahakama Kuu ikawabamiza Mahakama ya Rufani.


Jaji na Mlezi wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Augustine Mwarija (katikati) akishiriki kwenye mazoezi kabla ya kushiriki kwenye michezo mbalimbali kwenye Bonanza ambalo limeandaliwa na Chama cha Majaji na Mahakimu (JMAT) Tawi la Dar es Salaam. Bonanza hilo limefanyika leo tarehe 9 Septemba, 2023. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa JMAT Tawi la Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Bonanza, Mhe. Shaban Lila.
Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania (juu) na Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania (chini) wakipasha pasha.

Pasha pasha ikiendelea (juu na chini).

Pasha pasha imengoga sasa.
Majaji na watumishi wengine wa Mahakama wakichomoka kushiriki kwenye bio za mita 100. Picha chini, Majaji na watumishi wengine wakifukuza upepo.

Timu ya Kamba wanawake ya Mahakama Kuu (juu) ikiwakamua Mahakama ya Rufani (chini).

Timu ya Kamba wanaume ya Mahakama ya Rufani (juu) ikiwatoa jasho Mahakama Kuu (chini).

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe, Kevin Mhina (kushoto) akijaribu kumtoka mchezaji wa Timu ya mpira wa miguu ya Mahakama ya Rufani. Picha chini, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Gerson Mdemu (kushoto) akiwania mpira. Katika mchezo huo, timu ya Mahakama Kuu iliibuka mshindi kwa mabao 2:1.

Kipa wa Timu ya Mpira wa Miguu ya Mahakama ya Rufani Spear Mbwembwe (aliyekaa chini) akiwalaumu wachezaji wenzake baada ya kulambishwa nyasi kwa mara ya pili na Timu ya Mahakama Kuu.
Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Agnes Mgeyekwa (kulia) akijiandaa kurusha mpira kwenye mechi ya mpira wa pete. Picha chini, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahara Maluma (kushoto) akitupia kikapu kwenye gori. Katika mechi hiyo, Timu ya Mahakama Kuu imetupia vikapu 25:11.



Timu ya Netiboli ya Mahakama Kuu.
Timu ya Mpira wa Miguu Mahakama Kuu.
Timu ya Mpira wa Miguu Mahakama ya Rufani.
Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Jacobs Mwambegele (kulia) akimgalagaza mtu kwenye mchezo wa bao wanaume. Picha chini, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Issa Maige akimtoa jasho Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Isaya Arufani kwenye mchezo wa draft.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni