Ijumaa, 22 Septemba 2023

KIKAO CHA KUSUKUMA MASHAURI CHAHIMIZA UPELELEZI KUHARAKISHWA

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro iliyopo katika Jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki jana tarehe 21 Septemba, 2023 ilifanya kikao cha kusukuma mashauri ya jinai na kuhimiza upande wa upelelezi kutekeleza wajibu wao kwa kukamilisha upelelezi kwa wakati.

Kikao hicho kilichoendeshwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Livini Lyakinana kilibainisha kuwa kuna mashauri 34 katika ngazi ya Mkoa ambayo yamefikisha siku 100 bila kusikilizwa na Mahakama inasubilia upelelezi na ushahidi ili iendelee kutekeleza majukumu yake.

Hivyo, kikao kimeazimia mamlaka zinazohusika kutekeleza majukumu yao kwa wakati kwenye mashauri hayo, huku upande wa Mahakama ukiahidi kuyasikiliza mfululizo na kufikia tarehe 20 Novemba, 2023 yawe yameondoshwa na taarifa yake kusomwa katika kikao kijacho.

Hata hivyo, Mhe. Lyakinana aliwaeleza wajumbe wa kikao hicho kuwa mashauri 13 kati ya 22 yaliyojadiliwa katika kikao kilichopita kwa kukaa zaidi ya siku 100 yameshatolewa maamuzi, huku tisa yaliyobaki yakisubiria mamlaka husika zimalize kazi yao ili Mahakama ifanye kazi yake ya kutenda haki.

Kikao hicho kilichowashirikisha wajumbe mbalimbali ambao ni wadau wa Mahakama, wakiwemo Waendesha Mashtaka, Mawakili wa Kujitegemea, TAKUKURU, Wapelelezi toka Jeshi la Polisi, Afisa uangalizi na maafisa wa Mahakama, kilijadili mambo mbalimbali, ikiwemo namna ya kupambana na Mawakili bandia, maarufu kama vishoka.

Hoja hiyo ilifafanuliwa na Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) Kanda ya Morogoro, Msomi Baraka Lweeka kwa kuiomba Mahakama kufanya uhakiki pale inapopata mashaka na mtu anayejitambulisha kama Wakili kwa kutumia mifumo iliyopo au kwa kuwasiliana na uongozi wa TLS Kanda ili kujiridhisha.

Kikao hicho pia kilijadili namna ya kutoa kipaumbele cha kuwasikiliza kwanza wenye mashauri yanayowahusu watoto, wazee, wagonjwa, mama wajawazito na walemavu, utoaji wa nakala za hukumu kwa wakati, huku Mahakama ikipongezwa kufanya vizuri katika eneo hili, utoaji wa adhabu ya vifungo vya nje na Wapelelezi kutekeleza majukumu yao kwa wakati ili kesi ziweze kuendelea.

 Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro, Mhe. Livini Lyakinana akiendesha kikao cha kusukuma mashauri ya jinai ngazi ya Mahakama ya Hakimu Mkazi.
Katibu wa kikao cha kusukuma mashauri ngazi ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro, Mhe. Renatus Barabara akichangia hoja wakati kikao kikiendelea.
Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), Kanda ya Morogoro Mhe. Baraka Lweeka (katikati) akinakili masuala yaliyokuwa yakijadiliwa wakati kikao.
Sehemu ya wajumbe wa kikao cha kusukuma mashauri ya jinai (juu na chini).

Sehemu nyingine ya wajumbe wakifuatilia wakati kikao kikiendelea, aliyekaa mbele ni Mwenyekiti wa kikao ambaye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mhe. Livini Lyakinana.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni