Na Faustine Kapama-Mahakama na Sade Soka (UDSM).
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe.
Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 05 Septemba, 2023 amezindua kitabu cha mkusanyiko wa mashauri ya ukatili wa kingono
kwa mtoto wa Ireland na Tanzania na kuhimiza wadau mbalimbali katika
mnyororo wa utoaji haki kuongeza matumizi ya vina saba (DNA) katika kukusanya ushahidi
ili kuwatia hatiani au kuwaachia huru wanaohusishwa
kutenda uhalifu dhidi ya watoto.
Mhe. Prof. Juma amesema kuwa kuna matumizi ya chini ya DNA katika makosa ya
ngono na imekuwa nadra katika Mahakama ya Rufani kusikiliza rufaa ambapo DNA
imetumika katika ukusanyaji wa ushahidi. “Tunashangaa kwa nini, huku sheria iko
wazi kabisa kwa sababu DNA inaweza kuwatia hatiani na pia kuwaondolea hatia
wasio na hatia.
"Je, siyo wakati na sisi pia kupata uzoefu kutoka Ireland jinsi
ushahidi wa DNA unavyotumika? Kuna mengi ambayo tunaweza kujifunza kutokana na Kitabu
hiki na lengo hapa liwe kubadili mtazamo wetu na hata kubadili namna ya
kuzitazama sheria tulizo nazo na kuzipa mwelekeo tofauti,” amesema.
Jaji Mkuu amesema kuwa Tanzania inapaswa pia kujifunza mbinu bora ya
kurekodi ushahidi wa mtoto kutoka Ireland, ambayo ina vifungu vya sheria vinavyoruhusu
ukusanyaji wa ushahidi kwa njia hizo.
Amesema hatua hiyo inaweza kuwa na manufaa kwa Tanzania, hasa pale ambapo
ni jambo la kawaida kwa Mahakama kusikiliza ushahidi wa watoto wahanga miaka
kadhaa baada ya kutendeka kosa na mtoto anaweza asiwe na kumbukumbu nzuri
anapohojiwa mahakamani.
“Kwa hivyo, kurekodi ushahidi mapema iwezekanavyo wakati mwingine
kunasaidia sana kupata haki. Haya ni mafunzo, ambayo nadhani tunapaswa katika
maboresho yetu, tuhakikishe tunaiga sheria za Ireland,” Prof. Juma amesema.
Akizungumza katika hafla hiyo, Naibu Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Bi.
Margaret Gaynor alipongeza mtazamo unaochukuliwa na Serikali ya Tanzania kuhusu
hatua za kupinga ukatili wa kijinsia, ikiwemo kutunga sheria na kuimarisha
uwezo wa utoaji haki kwa makosa ya jinai.
Naibu Balozi alisema kuundwa kwa kamati ya kuchunguza utendaji wa taasisi
za makosa ya jinai nchini ni hatua nzuri ambayo Serikali imeichukua na ripoti
iliyotolewa imezingatiwa na wote wanaohusika.
Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Baraza la
Uongozi la IJA, Mhe. Dkt. Gerald Ndika alisema kuwa Kitabu hicho kitakuwa nyenzo
muhimu siyo kwa maofisa wa Mahakama pekee, bali pia Mawakili, Waendesha Mashtaka,
Wapelelezi, Watunga Sera, Wasomi na umma kwa ujumla.
Awali katika salamu zake za ukaribisho, Mkuu wa IJA ambaye pia ni Jaji wa
Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo alisema uzinduzi wa Kitabu hicho
umewezekana kutokana na ushirikiano wa karibu kati ya Chuo hicho na Irish Rule of Law International (IRLI), shirika lisilo la kiserikali.
"Tuliingia makubaliano ya ushirikiano katika maeneo kadhaa katika
kushughulikia eneo zima la unyanyasaji wa kijinsia kwa watoto, ikiwemo kuandaa Mkusanyiko
wa kesi za namna hiyo kwa Tanzania na Ireland kwa sababu sote tunapata matatizo
yanayofanana," alisema.
Uzinduzi huo umefanyika
katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam na umeratibiwa na Chuo cha IJA kwa
kushirikiana na IRLI kupitia ufadhili wa ubalozi wa Ireland nchini Tanzania.
Hafla hiyo ya uzinduzi imehudhuriwa
na viongozi mbalimbali, wakiwemo Majaji Wafawidhi kutoka Mahakama Kuu Kanda ya
Dar es Salaam, Mahakama Kuu divisheni ya Kazi, Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha
Mirathi na Ndoa, Temeke, Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mahakama Kuu Divisheni
ya Biashara, pamoja na Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi.
Wengine ni Msajili wa Mahakama Kuu, wawakilishi kutoka Wizara ya Katiba na Sheria na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Mashtaka, Mratibu wa Dawati la Jinsia kutoka Jeshi la Polisi Tanzania na Mwakilishi kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF).
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni